Serikali imesema iko katika hatua za awali za kuandaa mpango wa
uagizaji wa gesi ya mitungi (LPG) kwa pamoja kama ilivyo kwa mafuta ya
Petroli hali itakayosaidia kudhibiti masuala mbalimbali ikiwemo bei
ya gesi hiyo .
Akizungumza wakati wa semina kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Nishati na Madini iliyofanyika jijini Dodoma, Waziri wa Nishati,
Dkt Medard Kalemani alisema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha
kuwa, wananchi katika maeneo yote nchini wanafikiwa na huduma hiyo,
hivyo Serikali itaratibu usambazaji wa gesi hiyo badala ya kuwaachia
wauzaji wenyewe kuamua maeneo wanayotaka kupeleka gesi.
‘’ Serikali ikitangaza bei elekezi kulingana na soko, itawafanya
wauzaji wafuate bei hiyo badala ya wao kujipangia, hii itasaidia
wananchi kuuziwa gesi kwa gharama inayofanana katika maeneo mbalimbali
ambapo gesi hiyo itauzwa.”alisema Dkt. Kalemani.
Alieleza kuwa, suala la sasa la kila muuzaji kujiamulia sehemu
anayotaka kupeleka gesi inafanya maeneo mengine kukosa kabisa nishati
hiyo hivyo sasa Serikali itaweza kuwadhibiti wauzaji na kuhakikisha
kuwa maeneo yote nchini yanafikishiwa gesi.
Aliongeza kuwa, utaratibu wa kuagiza gesi inayotumika majumbani kwa
pamoja utasaidia Taifa kutambua kiwango halisi cha gesi
kinachohitajika nchini na kiasi cha gesi kinachoingizwa nchini na
hivyo kusaidia pia katika shughuli za ukusanyaji wa mapato.
Awali, akitoa taarifa kwa Wajumbe wa Kamati hiyo, Kaimu Mkurugenzi
Mkuu wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Erasto Simon
alisema kuwa, Wakala huo kwa sasa unafanya tathmini ya namna bora ya
kuanza uagizaji wa pamoja wa gesi ya mitungi (LPG) kwa kuzingatia
maoni kutoka kwa wadau mbalimbali.
Akizungumzia faida mbalimbali zinazotokana na uagizaji wa mafuta wa
pamoja, Simon alisema kuwa, ni kuweka mazingira sawa ya kibiashara
kwani gharama za uagizaji wa mafuta ziko sawa kwa makampuni yote na
kuondoa mianya ya rushwa katika uagizaji wa mafuta kwani ufunguzi wa
zabuni hufanyika kwa uwazi na washiriki wote huridhika na matokeo ya
zabuni.
Alitaja faida nyingine kuwa ni, Taifa kuwa na uhakika wa usalama wa
upatikanaji wa mafuta kwa muda wote na kuwezesha Serikali kuwa na
takwimu sahihi za mafuta zinazosaidia katika ukusanyaji wa mapato na
kupanga bei elekezi ya mafuta.
Aliongeza kuwa, mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja umewezesha nchi
kudhibiti ubora wa mafuta yanayoingia nchini na pia kuongezeka kwa
sehemu za kupokelea mafuta kama bandari ya Tanga na Mtwara, tofauti
na ilivyokuwa awali kwani Bandari ya Dar es Salaam ndiyo ilikuwa
ikitumika kwa shughuli hizo.
Kutokana na hilo, alisema kuwa, nchi mbalimbali barani Afrika kama
vile Malawi, Zambia na Msumbiji wamekuja kujifunza kuhusu mfumo huo wa
uagizaji mafuta ili waweze kuutumia katika nchi zao.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (kulia) akizungumza na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dunstan Kitandula wakati wa Semina ya Wabunge hao iliyohusu Sekta ya Nishati iliyofanyika jijini Dodoma.
Watendaji mbalimbali kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi hizo wakifuatilia taarifa zilizokuwa zikitolewa wakati wa semina ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliyohusu Sekta ya Nishati.
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakifuatilia taarifa iliyokuwa ikitolewa kuhusu Sekta ya Nishati katika Semina ya Wajumbe hao iliyofanyika jijini Dodoma.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja
(PBPA), Erasto Simon, akiwasilisha taarifa kuhusu Wakala huo kwa
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakati wa
Semina ya Wabunge hao iliyohusu Sekta ya Nishati.
No comments:
Post a Comment