HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 15, 2019

Serikali mbioni kuanza Mpango wa Uagizaji wa Gesi ya Mitungi (LPG) Kwa Pamoja

Serikali imesema iko katika hatua za awali za kuandaa mpango wa uagizaji wa gesi ya mitungi (LPG) kwa pamoja kama ilivyo kwa mafuta ya Petroli hali itakayosaidia kudhibiti masuala mbalimbali ikiwemo bei ya gesi hiyo .

Akizungumza wakati wa semina kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliyofanyika jijini Dodoma, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani alisema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa, wananchi katika maeneo yote nchini wanafikiwa na huduma hiyo, hivyo Serikali itaratibu usambazaji wa gesi hiyo badala ya kuwaachia wauzaji wenyewe kuamua maeneo wanayotaka kupeleka gesi.

‘’ Serikali ikitangaza bei elekezi kulingana na soko, itawafanya wauzaji wafuate bei hiyo badala ya wao kujipangia, hii itasaidia wananchi kuuziwa gesi kwa gharama inayofanana katika maeneo mbalimbali ambapo gesi hiyo itauzwa.”alisema Dkt. Kalemani.

Alieleza kuwa, suala la sasa la kila muuzaji kujiamulia sehemu anayotaka kupeleka gesi inafanya maeneo mengine kukosa kabisa nishati hiyo hivyo sasa Serikali itaweza kuwadhibiti wauzaji na kuhakikisha kuwa maeneo yote nchini yanafikishiwa gesi.

Aliongeza kuwa, utaratibu wa kuagiza gesi inayotumika majumbani kwa pamoja utasaidia Taifa kutambua kiwango halisi cha gesi kinachohitajika nchini na kiasi cha gesi kinachoingizwa nchini na hivyo kusaidia pia katika shughuli za ukusanyaji wa mapato.

Awali, akitoa taarifa kwa Wajumbe wa Kamati hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Erasto Simon alisema kuwa, Wakala huo kwa sasa unafanya tathmini ya namna bora ya kuanza uagizaji wa pamoja wa gesi ya mitungi (LPG) kwa kuzingatia maoni kutoka kwa wadau mbalimbali.

Akizungumzia faida mbalimbali zinazotokana na uagizaji wa mafuta wa pamoja, Simon alisema kuwa, ni kuweka mazingira sawa ya kibiashara kwani gharama za uagizaji wa mafuta ziko sawa kwa makampuni yote na kuondoa mianya ya rushwa katika uagizaji wa mafuta kwani ufunguzi wa zabuni hufanyika kwa uwazi na washiriki wote huridhika na matokeo ya zabuni.

Alitaja faida nyingine kuwa ni, Taifa kuwa na uhakika wa usalama wa upatikanaji wa mafuta kwa muda wote na kuwezesha Serikali kuwa na takwimu sahihi za mafuta zinazosaidia katika ukusanyaji wa mapato na kupanga bei elekezi ya mafuta.

Aliongeza kuwa, mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja umewezesha nchi kudhibiti ubora wa mafuta yanayoingia nchini na pia kuongezeka kwa sehemu za kupokelea mafuta kama bandari ya Tanga na Mtwara, tofauti na ilivyokuwa awali kwani Bandari ya Dar es Salaam ndiyo ilikuwa ikitumika kwa shughuli hizo.

Kutokana na hilo, alisema kuwa, nchi mbalimbali barani Afrika kama vile Malawi, Zambia na Msumbiji wamekuja kujifunza kuhusu mfumo huo wa uagizaji mafuta ili waweze kuutumia katika nchi zao.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (kulia) akizungumza na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dunstan Kitandula wakati wa Semina ya Wabunge hao iliyohusu Sekta ya Nishati iliyofanyika jijini Dodoma.
 Watendaji mbalimbali kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Taasisi hizo wakifuatilia taarifa zilizokuwa zikitolewa wakati wa semina ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliyohusu Sekta ya Nishati.
 Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakifuatilia taarifa iliyokuwa ikitolewa kuhusu Sekta ya Nishati katika Semina ya Wajumbe hao iliyofanyika jijini Dodoma.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Erasto Simon, akiwasilisha taarifa kuhusu Wakala huo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakati wa Semina ya Wabunge hao iliyohusu Sekta ya Nishati.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad