HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, May 6, 2018

WAZIRI KAIRUKI AKABIDHI VIFAA VYA DOLA 350,000 KWA OFISI ZA MADINI ZA KANDA


Na Veronica Simba – Dodoma
Waziri wa Madini Angellah Kairuki amekabidhi vitendea kazi mbalimbali vyenye thamani ya jumla ya Dola za Marekani 350,000 kwa Ofisi za Madini za Kanda mbalimbali nchini.
Akikabidhi vifaa hivyo kwa Makamishna Wasaidizi wa Madini wa Kanda hizo, jana Mei 4 2018 Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma; Waziri Kairuki aliwataka wahusika kuvitunza kutokana na gharama kubwa iliyotumika kuvinunua.
“Serikali imekopa kwa ajili ya kuhakikisha sekta ya madini inaendelezwa ili iweze kuchangia zaidi katika uchumi wa nchi. Tunaamini vitawasaidia sana katika utendaji wa majukumu yenu. Mvitunze.”
Akifafanua kuhusu vifaa vilivyotolewa, Waziri alisema kuwa ni pamoja na kifaa maalum kinachotumia teknolojia ya kisasa kung’amua uwepo wa aina ya gesi hatarishi kwa afya, chini ya Migodi ya Madini.
Alisema kuwa kifaa hicho kinamsaidia muhusika kutambua sehemu yenye hewa hiyo hatarishi na hivyo kuchukua hatua stahiki za kujiepusha na ajali inayotokana na kuvuta hewa ya aina hiyo.
Aidha, alitaja vifaa vingine kuwa ni kifaa maalum cha kukuza taswira za madini kinachojulikana kitaalam kama ‘Hand Lens’. “Kifaa hiki hutumika katika shughuli za uthaminishaji madini ya vito ambapo husaidia kuyakuza madini husika katika ukubwa unaotakiwa ili kukokotoa thamani yake halisi tofauti na unapotumia macho ya kawaida,” alifafanua.
Vingine ni pamoja na GPS zinazotumika kupima mipaka ya maeneo, ‘Printer’, viatu na sare maalum vinavyotumika migodini, Kompyuta, na vifaa vingine vya kijiolojia.
Kwa upande wake, Kamishna wa Madini ambaye pia ni Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, Prof. Shukrani Manya alisema kuwa vifaa hivyo vimetolewa kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Madini (SMMRP).
Alisema kuwa, zoezi la kugawa vifaa hivyo limefanyika katika awamu kadhaa, ambapo kwa awamu ya kwanza, Kanda za Madini zilizogawiwa ni Kanda ya Kusini (Mtwara na Nachingwea), Kanda ya Ziwa Nyasa (Songea, Njombe na Tunduru), Kanda ya Kusini Magharibi (Chunya) na Makao Makuu ya Wizara (Ofisi ya Ukaguzi wa Migodi, wachimbaji wadogo na utoaji leseni).
Nyingine ni Ofisi za Madini za Singida, Dodoma, Morogoro, Tanga, Handeni, Musoma, Bariadi, Mpanda, Kigoma, Mwanza, Geita, Bukoba, Arusha, Moshi, Mirerani na Tabora.
“Vifaa vilivyobaki ni kwa ajili ya Ofisi za Shinyanga, Kahama, Kituo cha Uongezaji Thamani Madini (TGC), Ofisi ya Biashara ya Madini na Ofisi ya Kamishna wa Madini, ambao ndiyo wanaopatiwa leo hii,” alifafanua Prof. Manya.
Akizungumza baada ya zoezi hilo la kukabidhi vifaa; Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof Idris Kikula alisema kuwa, ni jambo la kutia faraja kwa kupata vitendea kazi kwa Ofisi hizo za Madini, ambazo kwa mujibu wa marekebisho ya Sheria ya Madini yaliyofanyika mwaka 2017, sasa ziko chini ya Tume.
Alisema kuwa, upatikanaji wa vifaa hivyo vya kisasa utasaidia Tume kutimiza jukumu lake kubwa la kusimamia mapato stahiki ya Taifa yanayotokana na shughuli za madini.

  Waziri wa Madini Angellah Kairuki (kushoto) akikabidhi vitendea kazi mbalimbali kwa baadhi ya Makamishna Wasaidizi wa Madini wa Kanda, Makao Makuu ya Wizara Dodoma, Mei 4 mwaka huu.
 Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (mwenye mtandio-mbele), akiwa katika picha ya pamoja na Makamishna Wasaidizi wa Madini wa Kanda na watendaji wengine wa Wizara, baada ya zoezi la kukabidhi vitendea kazi lililofanyika Mei 4 mwaka huu, Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma. Kushoto kwa Waziri ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akifuatiwa na Kamishna wa Madini ambaye pia ni Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, Prof. Shukrani Manya. Kulia kwa Waziri ni Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof Idris Kikula.
 Kutoka kulia ni Waziri wa Madini Angellah Kairuki, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Meneja Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Madini (SMMRP) Andrew Eriyo, wakiangalia baadhi ya vitendea kazi kwa ajili ya Ofisi za Madini nchini, muda mfupi kabla ya Waziri kuvikabidhi kwa wahusika, Mei 4 mwaka huu, Makao Makuu ya Wizara Dodoma.
Waziri wa Madini Angellah Kairuki akizungumza na Waandishi wa Habari, baada ya zoezi la kukabidhi vitendea kazi kwa Ofisi za Madini za Kanda, lililofanyika Mei 4 mwaka huu, Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad