HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, April 24, 2018

GLOBAL EDUCATION LINK WATOA USHAURI NASAHA WA KITAALUMA KWA WANAFUNZI ILI KUTIMIZA NDOTO ZAO

Na Said Mwishehe, Globu ya jamii
KAMPUNI ya Global Education Link imeamua kutoa ushauri nasaha wa kitaaluma kwa wanafunzi wa shule za sekondari mbalimbali nchini ili kuhakikisha wanafunzi wanafanikiwa kutimiza ndoto zao.

Imefafanua imeamua kutoa ushauri huo baada ya kuona wanafunzi wengi nchini hawana taarifa rasmi kuhusu vyuo vikuu na imesababisha wengi wao kushindwa kuchagua nini asome ili afanikishe malengo yake na matokeo kusababisha soko la ajira kuwa gumu.

Pamoja na hayo kampuni hiyo imesema ipo haja kwa Serikali kuunga mkono juhudi ambazo wamezianzisha katika kuhakikisha wanafunzi tangu wanapokuwa shuleni za msingi na sekondari wanajua mahitaji ya Taifa na nini asome ili kuwa na uhakika wa ajira.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Global Education Link Abdulmalik Mollel wakati anazungumza na waandishi wa habari kuhusu uamuzi wa kampuni hiyo kutoa ushauri nahasa wa kitaaluma ambao wameanza na tano na kidato cha sita kwa shule za sekondari za Mkoa wa Dar es Salaam.

Amesema malengo yao ni kutoa ushauri huo kwa wanafunzi wote nchini kuanzia elimu ya msingi kwani ndiko ambapo watalaam wa Taifa hili wanaoanzia kuandaliwa.

"Tumeamua kuanzisha darasa ambalo lengo lake ni kutoa ushauri nasaha wa kitaaluma kwa wanafunzi ambapo tutawaalika watalaam wa fani mbalimbali waje kuzungumza nao.Tunachotaka ni kumfanya mwanafunzi atimize ndoto zake na ili afanikiwe anatahitaji ushauri na kumuandaa kimazingira,"amesema.

Amesema wapo wanaotoka kuwa madaktari au wahandisi lakini hajui ni udaktari au uhandisi wa aina gani asome na matokeo yake wengi wanasoma kitu cha aina moja na changamoto yake ni kukosa ajira kwani watalaam wengi wanakuwa wa aina moja.

"Unapozungumzia daktari wapo wa aina mbalimbali kwamfano kuna daktari meno, mifupa, macho, mambo akina mama na aina nyingine za udaktari lakini mwanafunzi anapokuwa sekondari utamsikia anasema nataka kuwa daktari na unapomuuliza wa nini hana jibu sahihi.Hivyo sisi tunataka kumsaidia kujitambua mapema,"amesema.

Ametoa ombi kwa Serikali kuunga mkono juhudi hizo kwa kuruhusu watalaamu wa fani mbalimbali na ikiwezekana makatibu waku nao wapate fursa ya kuzungumza na wanafunzi kama sehemu ya kuwaandalia mazingira ya kufanikisha ndoto zao na kufafanua nchi nyingi duniani mtoto anapoonesha anataka kuwa nani basi jamii inamsimamia kwenye hilo.

Mollel amesema kampuni yao ambayo ni mawakala wakuu wa vyuo vikuu kwa wanafunzi wanaotaka kusoma nje ya nchi, amesisitiza ushauri huo unatolewa bure kwa wanafunzi wote na hivyo ni ombi lake kwa shule za sekondari kuruhusu wanafunzi wao wahudhurie.

".Hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kuandaa mazingira wezeshi kwa wanafunzi kujua mapema atakuwa nani baada ya kumaliza masomo.

Kwa upande wa mtalaam wa Saikolojia Dk.Chris Mauk amesema ushauri huo nasaha wa kitaaluma ni muhimu ukatolewa kwa wanafunzi nchini na kufafanua pamoja na elimu ambayo inatolewa dasarani ipo haja ya kutolewa pia elimu ya ziada ambayo hiyo inapatikana kwenye jamii inayokuzunguka.

Amesema hata changamoto ya baadhi ya wasomi nchini kuuonekana kutokuwa na sifa licha ya kuhitimu elimu ya chuo kikuu si kwamba hawana uwezo bali tatizo wanakosa elimu ya ziada.

Ametoa mfano anaweza kupatikana msomi mzuri tu na anao uwezo wa kutosha kufanya kazi lakini ukifuatilia unaweza kukutana si muaminifu au hana uwezo wa kuishi vizuri na jamii aliyonayo, hivyo anapozungumzia elimu ya ziada ni elimu ambayo inatolewa nyumbani namna ya kuishi katika misingi sahihi, elimu ambayo darasani haipati.

Wakati huohuo, wanafunzi wa kidato cha tano na sita ambao wamepata nafasi ya kushiriki kwenye darasa hilo wamesema moja ya kitu ambacho wamejifunza na kukielewa ni namna gani ya kusimamia malengo yao ya kitaaluma na kuomba yawe yanatolewa mara kwa mara na kwanafunzi wengi zaidi.
 Mkurugenzi wa Global Education Link (GEL), Abdulmalik Mollel akizungumza na wanafunzi walio fika kwenye semina hiyo.
 Mwanafunzi wa Shule  Sekondari Pugu,Christopher lyengwa akiuliza swali katika semeni hiyo iliyo fanyika katika ukumbu wa (GEL).
 Mkurugenzi Mkuu wa Global Education Link (GEL), Abdulmalik Mollel akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam
Afisa  Elimu wa Mkoa wa Dar es salaam,Hamis Yusufu  Lissu akizungumza na waandishi wa habari katika uzinduzi wa semina za kiwajegea uwezo  wanafunzi  wa Shule za Sekondari iliyoandaliwa na  Global Education Link (GEL)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad