HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, October 15, 2023

NACTVET YAELIMISHA WAKAZI WA KIBAHA

 BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), limewaelimisha wakazi wa Kibaha juu ya kazi na majukumu mengine ya Baraza.


Waelimishaji kutoka NACTVET wametekeleza wajibu wakati wa Wiki ya Maadhimisho ya Kitaifa ya Elimu ya Watu wazima yaliyofanyika katika Viwanja vya Maili Moja Kibaha - Pwani kuanzia tarehe 9 – 13 Oktoba 2023.

NACTVET imetumia fursa hiyo kuwajengea uelewa wadau wake na wananchi kwa ujumla katika mwendelezo wa kampeni yake ya kutoa elimu kwa umma hususan wananchi na wadau walioyatembelea mabanda ya Maonesho ya kazi za taasisi za elimu na asasi za kiraia wilayani humo. Watumishi wa Baraza pia walitoa ufafanuzi juu ya tunu za Baraza na mambo mbali mbali yanayosimamiwa na kutekelezwa na Baraza miongoni mwake likiwepo jukumu la udahili wa wanafunzi kwa Vyuo vinavyotoa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi nchini.

Pamoja na hayo , NACTVET imepokea maoni na kuzichukua changamoto wanazokabiliana nazo wadau wake ili kuboresha utendaji kwa maendeleo ya Elimu nchini. Aidha, NACTVET imevikumbusha vyuo kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za usajili zilizowekwa kwa kutoa elimu yenye ubora na wahitimu wenye ujuzi na umahiri unaokidhi mahitaji ya soko la Ajira.

Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu wazima nchini huadhimishwa sanjari na maadhimisho kama hayo duniani kote kila mwezi Septemba, ambapo mwaka huu hapa nchini, tarehe 13, Oktoba ndiyo ilikuwa kilele cha maadhimisho hayo ambapo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda ndiye aliyekuwa mgeni rasmi.





No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad