Na. Jacob Kasiri - Iringa. 
Shirika
 la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kupitia Idara ya Mahusiano kwa 
Jamii (Ujirani Mwema) katika Hifadhi ya Taifa Ruaha imekabidhi vifaa 
vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 31 kwa ajili ya mradi wa 
maji safi na salama unaotarajia kuanza hivi karibuni ili kumtua mama 
ndoo kichwani na kumpunguzia hadha ya kutembea umbali mrefu kufuata 
huduma hiyo. Zoezi la kukabidhi vifaa hivyo limefanyika leo tarehe 
31.08.2023 katika kijiji cha Tungamalenga kilichopo Halmashauri ya 
Wilaya ya Iringa. 
Vifaa hivyo vilivyonunuliwa na TANAPA ni 
pamoja na mipira ya kupitishia maji (GS Pipe medium na Polly pipe 63 mm)
 kwa ajili ya kutandazia chini zaidi ya kilometa 2 na vifaa vingine vya 
mradi wote. Wanufaika wa mradi huo wamechangia nguvu kazi kwa kuchimba 
mitaro na shilingi milioni 3.2. Shirika linaamini mradi huo 
utakapokamilika unapunguza changamoto ya ukosefu wa maji katika kijiji 
hicho.
Akitoa taarifa ya mradi huo, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi
 Godwell Meng’ataki, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Ruaha alisema "ninayo 
furaha kubwa kutoa vifaa hivyo ikiwa ni faida inayotokana na utalii, 
hivyo naahidi kushirikiana nanyi hadi mradi huu utakapokamilika."
"Kwa
 takribani miaka 12 TANAPA imetekeleza miradi mingi sana. Kama shirika 
tumetekeleza miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 13 ikihusisha 
miradi zaidi ya 327 ya afya, elimu,maji na mpango wa matumizi bora ya 
ardhi kijiji cha Tungamalenga kikiwa ni miongoni mwa vijiji hivyo. Kwa 
mantiko hiyo tunawajibika kwa wananchi kutekeleza miradi ili 
kuwapunguzia adha", alisema Kamishna Meing’ataki.
Hata hivyo, 
Kamishna huyo aliongeza "tunapokabidhi vifaa hivi tujue msingi wake 
mkubwa ni uhifadhi. Tunaposhirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo 
wananchi hawa katika uhifadhi na kuibua miradi kama hii, tunapata faraja
 kama shirika kuona wananchi wanatambua thamani ya Maliasili zao".
Aidha,Naibu
 Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA Steria Ndaga, Mkuu wa Kanda ya Kusini 
aliwaambia wananchi hao licha ya kukabidhiwa vifaa kwa ajili ya mradi wa
 maji, kijiji cha Tungamalenga ni wanufaika zaidi wa miradi mingine ya 
ujenzi wa madarasa na nyumba mbili za walimu walizojengewa hivyo 
wailinde na kuitunza, pia aliwataka wawe mstari wa mbele kufichua 
vitendo vya ujangili vinavyoendelea katika hifadhi hiyo.
Akikabidhi
 vifaa vya mradi wa maji safi na salama kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya 
Iringa Mhe.Veronica Kessy, Katibu Tawala Bw. Michael Semindu alisema, 
"kukamilika kwa mradi huu utaondoa changamoto ya maji hapa. Najua tanki 
lililopo lina ujazo wa lita 60000 na lilijengwa takribani miaka 20 
iliyopita kipindi idadi ya watu ilikuwa ni chini ya 2500, kwa sensa ya 
watu na makazi ya mwaka 2022, kijiji hiki kina zaidi ya wananchi 3600. 
Niwashukuru Hifadhi ya Taifa Ruaha kwa kutambua adha hii"
Kulingana
 na taarifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Afya,mtu 
mmoja anatakiwa atumie maji lita 50 kwa mahitaji yake yote ya msingi kwa
 siku. Hivyo uwiano uliopo katika kijiji chaTungamalenga hakikidhi 
matakwa ya umoja wa Mataifa, hivyo TANAPA imeona ni vema kutekeleza 
mradi huo ili kutatua adha ya maji safi na salama.
Mmoja wa 
wanufaika Bi. Jennifer Joseph hakusita kuonyesha furaha na hisia zake 
aliposema " shida ya maji kwetu ni tatizo kubwa na la muda mrefu, 
unaenda kuteka maji umbali mrefu ukirudi nyumbani muda wa wanafunzi 
kurudi kula unakuwa umetimia na hujaanda chakula na kusababisha watoto 
kurudi shule bila mlo wa mchana. Tunawashukuru TANAPA kwa kutuondolea 
kero hii".
"Kwa hiki tunachokishuhudia leo cha kukabidhiwa vifaa 
hivi tunaahidi kuilinda Hifadhi ya Taifa Ruaha kwa nguvu zetu zote, kwa 
wale waliokuwa wanakula nyamapori na kuiita mchicha tutawasemea bila 
woga," aliongeza Bi. Jennifer.
Kijiji cha Tungamalenga ambacho 
wananchi wake ndio wanufaika wa mradi huo kiko takribani kilometa 20 
kutoka Lango kuu la Hifadhi ya Taifa Ruaha.
.jpeg)
 

 
 

.jpeg)

.jpeg)

 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment