HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, December 7, 2021

WAKULIMA WA MPUNGA WASHAURIWA KUTUMIA MBEGU BORA

 

Na Farida Saidy, MOROGORO.
WAKULIMA hapa nchini wametakiwa kutumia mbegu bora na zinazovumilia ukame ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi yanayojitokeza na kuleta athari katika sekta ya kilimo.

Hayo yamebainishwa na wataalamu pamoja na watafiti wa kilimo mjini Morogoro walipokutana kujadili namna bora ya kukuza kilimo cha mpunga na kuwaletea tija wakulima wa zao hilo.

Dakt Atugonza Biralo mtafiti kutoka Taasisi ya utafiti kilimo Nchini (TARI) amesema, kama wakulima watafuata ushauri unatolewa na waalamu pamoja na watafiti wa zao la mpunga hapa nchini uzalishaji wao utaongezeka.

Amesema TARI imezalisha mbegu mbalimbali zenye kukabiliana na kila aina ya udongo pamoja na mabadiliko ya tabia nchi,ambapo kupitia mbegu hizo mkulima anaweza kulima sehemu yeyote hapa nchini kwa kufuata ushauri wa wataalam.

Kwa upande wake Diomedes Kalisa Mratibu wa mradi wa kujenga uwezo na kubadilishana uzoefu katika zao la mpunga kutoka shirika la chakula Duniani FAO amesema FAO ipo tayari kushirikiana na serikali katika kuongeza tija katika sekta ya kilimo hususani katika zao la mpunga kupitia miradi mbalimbali.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa kilimo Adoph Mkenda Mkurugenzi wa taasisi ya kuthibiti ubora wa mbegu Tanzania TOSCI Patrick Ngwediagi ameleza namna serikali ilivyojipanga kukuza sekta ya kilimo hususani zao la mpunga hapa nchini.

Bwana Twalib Mkubwa Mmoja wa wakulima wa zao la mpunga kutoka mkoani Iringa anaeleza namna mabadiliko ya tabia nchi yalivyoathiri kilimo cha mpunga.

Aidha amesema wakulima wengi wamekuwa wakilima kilimo cha mazoea jambo linalosababisha zao la mpunga kukosa thamani na kuonekana kama zao la chakula tu na halifai kwa biashara.

Hivyo amewataka wakulima wa zao hilo kufuata ushari wa wataalamu ili kuongeza uzalishaji na kulifanya zao la mpunga kuingia katika mazao ya kibiashara.

Pamoja na hayo ameitaka serikali kuongeza wigo katika kutafuta soko la zao la mpunga ndani na nje ya nchi, kwani baada ya wakulima kupewa elimu na kufuata ushauri wa wataalamu uzalishaji utaongezeka mala dufu.

Ikumbukwe kuwa mpunga ni zao la pili la chakula kwa umuhimu linalolimwa sehemu nyingi nchini Tanzania, Umuhimu wa zao hili umeongezeka kuanzia muongo uliopita kutokana na jamii za mijini na vijijini kupendelea zaidi kula wali na kupunguza ulaji wa vyakula vingine na kulifanya zao hili kuwa la chakula na biashara.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad