Waziri
wa Habari Sanaa Utamaduni na Michezo Innocent Bashungwa, Naibu Waziri
wa Habari Sanaa Utamaduni na Michezo Mh. Pauline Gekul wakisikiliza
vifaa maalum vya ukalimani vilivyozinduliwa hivi karibuni.
*************************
(Na. Jovina Bujulu – BAKITA)
Hivi
karibuni, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Innocent
Bashungwa alizindua vifaa vya kisasa vya ukalimani ambavyo vitatumiwa na
Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) kufundishia wakalimani wa lugha
mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Hii ni hatua kubwa kwa BAKITA
katika kuhakikisha lugha ya Kiswahili inazidi kukua na kuenea kitaifa na
kimataifa, kwani wakalimani watapata ujuzi wa ukalimani na kuwa
mabalozi wazuri wa Kiswahili ndani na nje ya Tanzania.
Akizungumza
wakati wa uzinduzi huo, Waziri Bashungwa alisema kuwa wanaohitaji kujua
lugha ya Kiswahili wanapaswa kupata rasilimali mbalimbali ikiwemo
utaalamu wa ukalimani.
“Kuenea na kukubalika kwa Kiswahili
duniani kunadhihirisha na msemo wa ‘Chanda chema huvikwa pete’.
Watanzania tuna wajibu mkubwa wa kuwasaidia wengine wanaokitafuta.
Wanaohitaji kujua Kiswahili wanapaswa kupatiwa rasilimali mbalimbali
zitakazowawezesha kukielewa na kukitumia kwa ufasaha zaidi na moja ya
rasilimali hizo muhimu ni utaalamu huu wa ukalimani”, alisema Mhe.
Bashungwa.
Alibainisha kuwa Serikali imenunua vifaa hivyo ikiwa
ni utekelezaji wa malengo yanayohusiana na lugha ya Kiswahili yaliyomo
katika ahadi za Serikali Bungeni na pia malengo yaliyomo katika Ilani ya
Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020-2025. “Vifaa hivi vitaliwezesha
BAKITA kutoa mafunzo ya msasa na kuwasajili wakalimani watakaotumiwa
katika mikutano mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.
Waziri
Bashungwa alifafanua kwamba Kiswahili kwa sasa kinatumika katika
mikutano mbalimbali ya kimataifa kama vile katika Jumuiya ya Afrika
Mashariki, Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na Bunge
la Afrika na Umoja wa Afrika.
“Ili Kiswahili kiendelee kutumika
katika mikutano hiyo na mingine zaidi hapo baadaye, ni lazima kuwe na
wakalimani wa kutosha watakaokuwa wanatoa huduma ya ukalimani kwa
Kiswahili kutoka lugha mbalimbali za Kimataifa”, aliongeza Mhe.
Bashungwa.
Aidha, aliagiza BAKITA kutumia vifaa hivyo kwa ajili
ya kuwaandaa wakalimani wa kutosha ili nchi iwe na uwezo wa kuwapeleka
katika mikutano mbalimbali kulingana na mahitaji ya kimataifa.
Alitoa
wito kwa Watanzania wenye utaalamu wa ukalimani na wanaojua ligha za
kimataifa kama vile Kiingereza, Kireno, Kichina, Kifaransa, Kijerumani
na Kiarabu kwenda BAKITA kupata mafunzo ya msasa ya kutumia vifaa hivyo
na kusajiliwa ili Serikali iweze kutambua idadi yao na ili kuwatumia
katika kazi mbalimbali ikiwemo kuwapeleka katika mikutano ya kimataifa
pindi mahitaji hayo yatakapowasilishwa nchini.
Kwa upande wake,
Kaimu Katibu Mtendaji wa BAKITA, Consolata Mushi alisema uwepo wa vifaa
hivyo ni mafanikio makubwa sana katika taasisi hiyo hasa katika kipindi
hiki ambacho taifa linajishughulisha na ubidhaishaji wa Kiswahili kwani
Watanzania wenye weledi wa lugha ya Kiswahili wanaweza kupata fursa
zitokanazo na lugha hii kitaifa na kimataifa.
“BAKITA litavitumia
vifaa hivi kwa ajili ya kupima uwezo wa wakalimani tulionao nchini, na
watakaothibitika kuwa na ubora watasajiliwa katika kanzidata ili
Serikali na taasisi zake, asasi zisizo za Serikali pamoja na watu
binafsi waweze kuwatumia katika mikutano mbalimbali ya kitaifa na
kimataifa”, alisema Mushi.
Alivitaja vifaa hivyo kuwa ni pamoja
na chombo maalumu kwa ajili ya kuchagua lugha na kuzungumza, seva,
vipaza sauti, visikizi, spika, kikuza sauti na mashine ya mkalimani.
Vifaa
hivyo vina thamani ya shilingi milioni 187.5, ambapo Serikali kupitia
BAKITA imenunua kizimba cha ukalimani kwa shilingi milioni 5.1 ili
kuwezesha utendaji wenye ufanisi na pia Baraza limeandaa chumba maalumu
kilichofungwa vifaa hivyo.
“Vifaa hivi vitawezesha jumla ya lugha
nane kufanyiwa ukalimani kwa wakati mmoja na vinaweza kutumiwa na watu
30 kwa wakati mmoja,” aliongeza Mushi.
Pamoja na wakalimani
kunufaika na vifaa hivyo, pia vitatumiwa na vyuo vikuu vya hapa nchini
kwa ajili ya mafunzo ya ukalimani kwa vitendo na kuwawezesha kuimarisha
zaidi uwezo wa wanafunzi katika taaluma ya ukalimani jambo ambalo
litakuwa na faida kubwa kwa wanafunzi wenyewe, vyuo na taifa kwa ujumla.
Kaimu
Katibu Mtendaji wa BAKITA, alitoa wito kwa wakalimani wote nchini
waliopita kwenye mafunzo rasmi na wale wa nje ya mafunzo rasmi ambao
wanajishughulisha na ukalimani, kuwasiliana na BAKITA, kwa ajili ya
kufanikisha mpango huu madhubuti wa kuwapa mafunzo na kuwatambua.
Naibu
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul
amewahimiza BAKITA kuwa sasa ni wakati wao kufanya tafsiri ya kanuni na
miongozo mbalimbali ya kisheria kwa lugha ya Kiswahili ili kuwawezesha
Watanzania wengi kushiriki katika mambo yanayowahusu bila changamoto ya
uelewa wa lugha.
Monday, September 6, 2021
Home
HABARI
BARAZA LA KISWAHILI LA TAIFA LAZIDI KUIMARIKA, LAPATA VIFAA VYA KISASA VYA KUFUNDISHIA WAKALIMANI
BARAZA LA KISWAHILI LA TAIFA LAZIDI KUIMARIKA, LAPATA VIFAA VYA KISASA VYA KUFUNDISHIA WAKALIMANI
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment