Na. Farida Ramadhani na Ivona Tumsime, WFM, Dodoma
Serikali imezitaka Taasisi
zote za Umma kuhakikisha zinapata kibali cha Waziri wa Fedha na Mipango kabla
ya kuanzisha mfumo wowote wa kielektroniki wa usimamizi wa fedha za umma kama
ilivyoelekezwa katika Waraka wa Hazina.
Agizo hilo limetolewa na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James wakati wa hafla ya
kupokea ripoti ya tathmini ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato na
Usimamizi wa Fedha za Umma.
Bw. James alisema kuwa Wizara
ya Fedha na Mipango ndio yenye mamlaka ya kutoa muongozo wa uanzishwaji wa
mifumo ya usimamizi wa fedha za umma na kutoa angalizo kuwa wote watakaokiuka
agizo hilo watachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Nawasisitiza Maafisa Masuuli
wote kuhakikisha mnapata ridhaa ya Wizara ya Fedha
na Mipango kabla ya kufanya ununuzi, uundaji, usimikaji na utumiaji wa mfumo
wowote wa kielektroniki wa usimamizi wa fedha za umma katika mafungu au Taasisi
zenu kama ilivyoelekezwa katika Waraka huo”,
alisisitiza Bw. James.
Alisema
kuwa Serikali hufanya jitihada mbalimbali katika kuboresha na kuanzisha mifumo mbalimbali ya kielektroniki ili
kuongeza ufanisi katika ukusanyaji mapato na kusimamia matumizi ya Fedha za Umma.
Alisema mpaka
sasa Serikali imeshabuni na kutengeneza mifumo mikubwa ya kielektroniki minne
ambayo ni Mfumo
wa Ukusanyaji wa Mapato ya Kodi, Maduhuli, Tozo na Huduma Mbalimbali za
Serikali (GePG), Mfumo
wa Usimamizi na Udhibiti wa Matumizi na Malipo ya Serikali (MUSE), Mfumo wa Usimamizi wa Miradi ya
Maendeleo (NPMIS) na Mfumo wa Usimamizi wa Misamaha ya Kodi.
Bw. James alibainisha kuwa Mfumo wa MUSE unawezesha
Wizara, Idara zinazojitegemea, Sekretarieti za Mikoa, Halmashauri zote, Wakala
na Taasisi zingine za Serikali kusimamia na kudhibiti mapato,
malipo ya matumizi ya kawaida na
kulipa malipo kwa njia ya kiektroniki kupitia Benki Kuu na Benki za Biashara.
Akizungumzia Mfumo wa Usimamizi wa Miradi ya Maendeleo (NPMIS), Katibu Mkuu huyo
alisema mfumo huo ulianzishwa
ili kuiwezesha
Serikali na wadau wengine kupata taarifa sahihi
za miradi ya maendeleo kwa wakati.
Alisema
kuwa kila Taasisi inayotaka kutekeleza mradi
wowote wa maendeleo ni lazima ahakikishe kuwa inatumia mfumo katika kufanya
maombi na utekelezaji wa mradi. Hakuna malipo au mgao wa pesa za maendeleo
zitalipwa nje ya mfumo. Nazitaka taasisi zote zenye miradi inayotegemea pesa
kutoka Serikalini
kuhakikisha miradi yote iko kwenye kanzidata hii ya miradi”,
alisema.
Katibu Mkuu huyo alisema Mfumo wa GePG
ulianzishwa kwa lengo la kutatua changamoto mbalimbali za ukusanyaji mapato
ikiwemo ugumu wa kupata taarifa ya makusanyo
yanayofanyika kwa wakati huo huo, gharama
kubwa za miamala inayohusu makusanyo ya Fedha za Umma, utaratibu usio rafiki kwa Mlipaji wa
huduma za umma na machaguo
machache ya njia za kulipia (Benki, Mitandao ya simu za mkononi au Mawakala).
Alisema pia Mfumo wa Usimamizi na
Utoaji wa Misamaha ya Kodi ya Ongezeko la Thamani Serikalini umeanzishwa ili
kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizokuwepo Serikalini katika zoezi zima
la usimamizi na utoaji wa misamaha ya kodi ya ongezeko la thamani Serikalini
ikiwemo Wizara/Taasisi/Halmashauri kuwasilisha Wizara ya Fedha na Mipango
baadhi ya orodha za vifaa visivyokidhi vigezo vya kupata msamaha wa VAT.
Kwa upande
wake Mtafiti aliyefanya tathmini ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanya wa Mapato na Usimamizi
wa Fedha za Umma kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Prof. Joel Mtebe, alisema
kuwa, alifanya utafiti katika taasisi za Serikali 271 kwenye mikoa 11 na
kubaini kuwa mfumo umerahisisha ukusanyaji wa maduhuri ya Serikali kwa asilimia
87 kutokana na wananchi kutokwenda moja kwa moja katika ofisi kulipia huduma.
Naye Mhasibu Mkuu wa Serikali, Francis
Mwakapalila, alisema kuwa Mifumo ya Fedha iliyoanzishwa na Serikali ukiwemo
Mfumo wa Usimamizi na Udhibiti wa Matumizi na
Malipo ya Serikali (MUSE), umeokoa takribani Shilingi bilioni tano zilizokuwa zikitumika
kununua leseni za mifumo iliyokuwa ikitengenezwa nje ya nchi.
Kwa upande wa wanufaika wa mifumo
hiyo akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF),
Bw. Willium Erio, alisemakuwa Mfumo
wa Ukusanyaji wa Mapato ya Kodi, Maduhuli, Tozo na Huduma Mbalimbali za
Serikali (GePG), umesaidia kuongeza mapato kutoka Sh. bilioni 994 kwa miaka miwili
iliyopita hadi takribani Sh. trilioni 1.1 kwa sasa.
Alisema kuwa ongezeko la mapato hayo
umetokana na mifumo kuondoa mianya ya mapato kuvuja na kupungua kwa gharama za
miamala.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu
wa Serikali, Bw. Doto James akizungumza wakati wa halfa ya kupokea ripoti ya tathimini
ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa Mapato na Usimamizi wa Fedha za Umma,
ambapo amewaagiza Afisa Masuhuli wote nchini kutotengeneza mifumo yoyote bila
kupata kibali kutoka wizara hiyo, jijini Dodoma.
Meza Kuu ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na
Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James (wapili kushoto), wakifatilia
uwasilishwaji wa ripoti ya tathimini ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa
Mapato na Usimamizi wa Fedha za Umma, jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu
wa Serikali, Bw. Doto James akimsikiliza Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA), Dkt. Edwin Mhede baada ya kumaliza halfa ya upokeaji ripoti ya tathimini
ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa Mapato na Usimamizi wa Fedha za Umma,
jijini Dodoma.
Mhasibu Mkuu wa Serikali, Bw. Francis Mwakapalila, akizungumza
wakati wa halfa ya kupokea ripoti ya tathimini ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji
wa Mapato na Usimamizi wa Fedha za Umma, jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mkuu Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF),
Bw. Wiliam Erio akizungumza wakati wa halfa ya kupokea ripoti ya tathimini
ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa Mapato na Usimamizi wa Fedha za Umma,
jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mifumo ya Kifedha,
Bw. John Suasi akiteta jambo, Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimali Watu na Utawala,
Bw. Alfred Dede (kushoto) na Dkt. John Kalugendo baada ya halfa ya kupokea
ripoti ya tathimini ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa Mapato na Usimamizi
wa Fedha za Umma, jijini Dodoma.
Meza Kuu ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na
Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James (katikati), ikiwa katika
picha ya pamoja na baadhi ya Menejimenti ya wizara hiyo baada ya halfa ya kupokea
ripoti ya tathimini ya Mfumo wa Kielektroniki ya Ukusanyaji wa Mapato na Usimamizi
wa Fedha za Umma, jijini Dodoma.
(Picha na WFM – Dodoma).
No comments:
Post a Comment