HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 18, 2019

WANANCHI BUNJU WAIBA MAJI NA KUJITENGENEZEA BWAWA LA UMWAGILIAJI

Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) imeendelea na zoezi la ukaguzi wa miundo mbinu ya maji katika Mikoa ya  kihuduma ya DAWASA  ambapo katika mtaa wa Bunju A katika kata ya Bunju wamegundua uhujumu mkubwa wa miundombinu ya maji inayofanywa na wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya ukaguzi huo Meneja Mapato wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Edger Zawayo amesema kuwa zoezi la kupambana na watu wanaochezea miundombinu ya maji linaendelea na katika eneo hilo la Bunju A, wamekuta Bomba lililokuwa linaenda kwa mteja limehujumiwa katikati na maji hayo kutumika katika kilimo cha mbogamboga.

"Kama tulivyoona maji yaliyohujumiwa katikati kutoka kwenye bomba la mteja yameelekezwa katika bwawa na wanatumia pampu kumwagilia mchicha, nyanya na migomba kama tunavyoona hapa." ameeleza Zawayo.

Amesema kuwa mtandao wa DAWASA umesambaa katika jiji hilo hivyo ni vyema wakaenda kwenye ofisi husika ili wapate kuunganishwa na huduma hiyo na sio kuhujumu na kuwakosesha wananchi wengine huduma.

"Ofisi za DAWASA zimesambaa kila sehemu ndani ya jiji la Dar es Salaam hivyo ni vyema kila mwananchi mwenye uhitaji wa maji aje kulipia na atapata huduma hiyo, haipendezi kuhujumu huduma ya maji ambayo mteja ameilipia hali inayowapelekea wateja wengine  kununua maji baada ya wananchi wasio wema kuhujumu huduma hiyo." Amesema  Zawayo

Aidha amesema kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa kwa yeyote atakayebainika amehujumu miundombinu ya maji kwa namna yoyote ile.

Kwa upande wake Afisa mtendaji wa mtaa wa Bunju A katika kata ya Bunju Maombi Lameck amesema kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa sio waaminfu baada ya kuhujumu miundombinu ya DAWASA kwa kukata mabomba ya wateja na kuelekeza maji katika bwawa ambalo hutumika katika kilimo cha mbogamboga.

Maombi ametoa rai kwa wananchi wote wa Bunju A na Manispaa ya Kinondoni kwa ujumla kuacha mara moja tabia ya kuhujumu miundombinu ya DAWASA na miundombinu mingine ya Serikali kwa kuwa wanakwamisha maendeleo kwa kiasi kikubwa na yeyote atakayebainika anahujumu miundombinu hiyo kwa namna yeyote ile atachukuliwa hatua kali za kisheria.
  Meneja Mapato wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Edger Zawayo akionesha bwawa lililojanzwa na baadhi ya wananchi wa mtaa wa Bunju A kutoka kwenye Bomba la DAWASA kwa ajili ya umwagiliaji wa Mbogamboga zinazolimwa eneo hilo.
 Mtaalamu wa Mambo ya Mita kutoka Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Da es Salaam (DAWASA) Mohammed Mwakimila akionesha moja ya bomba lililokuwa linaenda kwa mteja likiwa limehujumiwa na maji hayo kwa kujaza bwawa na kutumika katika kilimo cha mbogamboga katika mtaa wa Bunju A kata ya Bunju jijini Dar es Salaam leo.
  Meneja Mapato wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Edger Zawayo akionesha bomba la pili lililokatwa na kuelekenzwa kwenye Bwawa kwa ajili ya kutunza maji ya kumwagilia Mbogamboga zinazolimwa na kumkosesha mwenye bomba hilo maji eneo hilo la Bunju A kata ya Bunju jijini Dar es Salaam .
 Baadhi ya mabomba yaliyokuwa yanatumika kuvutia maji kutoka kwenye bwawa hilo lililokuwa linatunzia maji ya Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA)
 Muonekano wa Bwawa la lililojazwa maji ya Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) mara baada ya wananchi wasiowaaminifu kukata bomba la Mamlaka hiyo na kulielekezea kwenye bwawa hilo kwa ajili ya umwagiliaji wa Mbogamboga zinazolimwa eneo hilo.
  Meneja Mapato wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) Edger Zawayo akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya ukaguzi wa kustukiza kwenye shamba hilo na kukuta wizi wa maji kwa kiasi kikubwa katika mtaa wa Bunju A kata ya Bunju jijini Dar es Salaam leo.
 Afisa mtendaji wa mtaa wa Bunju A katika kata ya Bunju Maombi Lameck akizungumza na waandishi wa habari pamoja na kuwaasa wananchi wa eneo hilo kuacha tabia za wizi wa maji kwani watashughulikiwa mara baada ya kujione wizi wa Maji ya DAWASA katika shamba hilo.
Shamba la Nyaya likiwa limestawi karibu na bwawa lililokuwa linahifadhi maji ya wizi ya Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad