HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, May 24, 2019

Jafo atoa Neno kwa Plan International

Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo(Mb) amelitaka Shirika la Plan International kutekeleza miradi yake hapa nchini kwa weledi na umakini ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kuendelea kupata ufadhili.
Waziri Jafo ameyasema hayo wakati wa kufunga warsha ya Shirika hilo iliyokuwa na lengo la kufanya tathimini na kuweka mipango ya Shirika iliyofanyika Jijini Dodoma.

Alisema kuwa ni vyema Shirika la Plan International kutekeleza majukumu na miradi yake kwa ufanisi mkubwa ili kushika nafasi ya kwanza kwa utendaji kazi kwa Nchi zinazotekeleza miradi yake mashariki na kusini mwa Africa (RESA).
“Ninyi wataalamu wa Shirikia la Plan International mnatakiwa kuchapa kazi kwa weledi wa hali juu ili kushika nafasi ya kwanza na kuwa katika nafasi nzuri ya kupata ufadhili wa utekelezaji wa malengo ya Shirika.”

Jafo aliongeza: “Ujue ufadhili ndio kila kitu katika Shirika, mkifanya kazi vizuri mtapata fedha za kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali na hapo mtaweza kuwafikia wanufaika wengi katika achi yetu na kuzidi kuwainua na kuleta matumaini mapya katika jamii yetu,” Alisema Jafo.
“mkizidi kupata ufadhili ndipo na nyie mtapata mishahara mizuri na marupurupu hivyo ufadhili sio kwa sababu ya wananchi pekee bali ni kwa faida yenu  kama watendaji wakuu wa shirika hili”

Aidha, Jafo alitumia fursa hiyo kuwapongeza Plan International kwa namna wanavyofanya kazi zao jambo ambalo linachangia utoaji wa huduma bora kwa jamii.
“Mimi nimefanya kazi Plan International na umahiri wangu na weledi katika utendaji kazi umetokana na kufanya kazi katika Shirika hili limenijenga katika misingi ambayo mpaka kazi imekuwa ni sehemu ya masiha yangu na wala sichoki kufanya kazi hii ndio Plan International”Alisema Jafo.

“Watu wengi wamekuwa wakinishangaa kwa kazi nyingi ninazozifanya kwa siku na bado nazifanya kwa umakini na umahiri mkuwa msingi huu niliupata Plan Internatioinal na bado  nawaelekeza watumishi wa Wizara yangu kufanya kazi kwa bidii wakati wote ndio maana unaona mabadiliko makubwa ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI.
Naye Meneja Ufadhili wa Plan International Nicodemus Gachu alisema kuwa mpaka sasa Shirika lina watoto rafiki elfu 30 ambao wanapata huduma mbalimbali kutoka Plan International.

Gachu alisema kwa sasa Plan Internationa imekuja na mpango wa kutoa Bima ya Afya iliyoboreshwa kwa watoto rafiki wa shirika hilo, ambao unatarajia kuzinduliwa hivi karibuni kwa kuwakabidhi watoto hao Bima za Afya katika kila Mkoa ambako wana watoto rafiki.
Gachu alitumia fursa hiyo kuanisha kazi ambazo Shirika limezifanya kuwa ni pamoja na kujenga miundombinu ya Afya katika baadhi ya hospital na vituo vya Afya kama Buguruni, ujenzi wa miundombinu ya Elimu, ujenzi wa  miundombinu ya Maji, kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo watoto kuzifahamu hazi zao.

Naye Neema Moris ambaye ni Meneja ya Uniti ya Kisarawe amesema kupitia warsha hiyo ya siku nne wameweza kujitathmini utendaji kazi wa shirika, namna ya kutatua changamoto wanazokabiliana nazo katika maeneo ya kazi na kuweka malengo ya utekelezaji wa kazi za Shirika.
Ikumbukwe kuwa Waziri Jafo alianzia kazi katika Shirika la Plan Internationa akiwa kama Meneja wa Uniti ya Kisarawe kabla ya kuwa Mbunge wa Kisarawe kisha kuteuliwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo (Mb) akifunga warsha ya Shirika la Plan International ya kufanya tathimini na kuweka mipango ya Shirika hilo inayofanyika Jijini Dodoma.
Meneja Ufadhili wa Plan International Nicodemus Gachu akitoa mada kwa washiriki wa warsha ya tathimini na mipango ya Shirika la Plan International.
 Wataalam wa Shirika la Plan International wakiendelea na warsha ya tathimini na kuweka malengo ya Shirika hilo inayofanyika Jijini Dodoma.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo (Mb) katika picha ya pamoja na Meneja wa Uniti ya Kisarawe katika warsha ya Shirika la Plan International inayofanyika Jijini Dodoma.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo (Mb) katika picha ya pamoja na wataalam wa shirika la Plan International wakati wa warsha ya tathimini na mipango.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad