HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 9, 2019

UJUMBE KUTOKA MAREKANI WATEMBELEA LIFE AND HOPE MKOA WA PWANI

Ujumbe kutoka Chama Cha  Kisaikolojia Marekani umetembelea Kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' kilichopo Bagamoyo Mkoa wa Pwani nchini Tanzania ili kujionea shughuli zinazofanywa na kituo hicho. Kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' kinajishughulisha na malezi ya watu walioathirika na aina zote za ulevi ikiwemo dawa za kulevya ambapo kipo mjini Bagamoyo.

Mratibu wa Safari hiyo, Dkt. Amanda Clinton kutoka  Chama Cha  Kisaikolojia Marekani, (American Psychological Association) amesema wamefurahishwa na hali waliyoikutam katika kituo hicho na kwamba wametoa ahadi ya kushirikiana na kituo hicho.m Alisema ni jambo la kufurahisha na kutia faraja kuona vijana wamekubali kukaa kwenye kituo ili kubadilisha tabia zao.

Aliongeza kuwa, nia thabiti huanza kwa muhusika wa tatizo kisha hatua inayofuata ni kupata mtu atakaemsaidia kuondoaa tatizo husika.lisema kwa mazingira aliyoyaona katika Kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' ana imani kuwa vijana hao watabadilika kitabia na hatimae kutimiza ndoto zao za kimaisha mara tu watakaporejea nyumbani.

Alifafanua kuwa, tayari nia imeonyeshwa na vijana hao, huku mtu wakuwasaidia yupo ambae ni Mkurugenzi wa kituo hicho cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' Al-karim Sadrudin Bhanji hivyo wana kila sababu ya kujivunia kutokana na maamuzi yao ya kujirekebisha kitabia. Aliendelea kusema kuwa tatizo la dawa za kulevya ni kubwa duniani hivyo jamii inapaswa kuchukua tahadhari na endapo athari imepatikana katika familia, na jamii kwa ujumla kila mtu ana wajibu wa kutoa msaada hata wa mawazo ili kusaidia wale walioathirika na dawa za kulevya.

Dkt. Amanda ambae ni mtaalamu wa saikolojia, alisema ili uweze kumsaidia mtu aliye athirika kisaikolojia kwanza unapaswa kumthamini na kumuona ni mtu muhimu katika jamii ili kile utakachomwambia aweze kukuelewa na kukubali mawazo yako. Msafara huo wa watu 15 kutoka Chama Cha  Kisaikolojia Marekani (American Psychological Association) umefurahia mazingira ya wanayoishi vijana hao na kusema hali hiyo inawanya wajione ni watu wenye thamani mbele ya jamii.

Awali akiwakaribisha wageni hao, Mkurugenzi wa kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' Al-karim Sadrudin Bhanji, amesema amefarijika na kufurahishwa kwa kufika ugeni huo ambao umefungua njia ya mafanikio ya kituo hicho. Bhanji alisema zipo changamoto kadhaa zinazokikabili kituo hicho ikiwemo ufinyu wa eneo na uelewa wa jamii kuhusu kituo hicho.

Alisema ili kufanikisha malezi ya vijana hao kituoni ushirikiano unahitajika kutoka kwa jamii, serikali na wadau mbalimbali ili kuwa kitu kimoja katika kusaidia vijana walioathirika na dawa za kulevya. Aidha, ametoa wito kwa wazazi na walezi kuacha kuwatenga vijana walioathirika na dawa za kulevya na badala yake wake nao chini kujadilinamna ya kuwasaidia kutoka hapo walipo.

Alisema Kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' kinatoa fursa kwa wazazi na walezi kufika kupata ushauri na kuona namna gani ya kuwasaidia vijana ili warejee katika hali yao ya kawaida na hatimae walitumikie taifa lao.

Kwa upande wao vijana wanaopata huduma ya malezi katika kituo hicho wamesema wana matumaini ya kurejea katika hali zao za kawaida na kurudi katika familia zao kuendelea na maisha ya kawaida kama ilivyo kwa watu wengine. Aidha, walitumia nafasi hiyo, kuwaasa vijana kuacha makundi yenye vishawishi vya ulevi kwa ulevi wa aina yoyote humpelekea mtu kupoteza kabisa thamani kwenye jamii.

Waliongeza kuwa, utumiaji wa dawa za kulevya humfanya mtu kila pesa anayopata haitoshi hali inayopelekea kuuza kila kitu chake na vitu vya wenzie ili tu afanikishe uvutaji wa dawa za kulevya. Wakiongea kwa uchungu vijana hao wamesema wapo walipoteza mali zao, kazi zao, familia zao kwasababu ya matumizi ya dawa za kulevya
Mkurugenzi wa kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' Al-karim Sadrudin Bhanji (kulia) akisalimiana na kiongozi wa msafara huo mara tu walipowasili katika kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' Dkt. Amanda Clinton (kushoto).
 Mmiliki wa Kituo cha uangaliazi maalum kwa watu walioathirika na matumizi ya dawa za kulevywa cha Bagamoyo mkoa wa Pwani Sober House, Al Karim Bhanji, akitoa taarifa fupi ya kituo hicho kwa wangeni kutoka Marekani  walipotembelea kituo hicho jana.
Mmoja  wa wameathiriwa na matumizi ya dawa za kulevya akitoa ushuhuda
 Mmoja  wa wameathiriwa na matumizi ya dawa za kulevya akitoa ushuhuda
 Picha ya pamoja kati ya Mkurugenzi wa kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' na wageni wake.
Mkurugenzi wa kituo cha Life and Hope ''Sober House Bagamoyo'' Al-karim Sadrudin Bhanji, akiwa katika picha ya pamoja vijana wake wanaopata huduma katika kituo hicho huku wakiwa na furaha.(Picha na Emmanuel Massaka, MMG)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad