HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, July 29, 2018

Muleba yaunganishwa rasmi umeme gridi ya Taifa

 Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Nyamagojo Wilayani Muleba Mkoani Kagera leo, wakati wa uzinduzi wa umeme wa gridi ya Taifa wa KV 33  ambapo sasa Wilaya ya Muleba, Biharamulo na Ngara zitakuwa zinatumia umeme huo.
 Waziri wa Niashati, Dk. Kalemani, akiwashukuru mafundi waliofanikisha ujenzi znjia za umeme wa gridi ya Taifa baada ya kukamilisha kazi hiyo kwa wakati. 
 Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, akikata utepe kuashiria uzinduzi wa umeme wa gridi ya Taifa Wilayani Muleba Mkoani Kagera leo.
 Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, akishangilia baada ya kuzindua umeme wa gridi ya Taifa katika Wilaya ya Muleba Mkoani Kagera leo.

Na MWANDISHI WETU-MULEBA
WAZIRI wa Nishati, Medard Kalemani, amezindua umeme wa gridi ya Taifa Wilaya ya Muleba, ambapo alisema kuwa hatua hiyo sasa inakwenda kuifanya wilaya hiyo kuwa na umeme wa uhakika.

Akizungumza leo kwenye uzinduzi wa umeme huyo wa gridi ya Taifa ulifanyika katika Kijiji cha Nyamagojo Wilayani Muleba, Dk. Kalemani, amesema kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania hasa wa maeneo ya vijijini wanapata umeme kwenye nyumba zao.

Amesema katika utekelezaji wa mradi huo wa ujenzi wa KV 33 wa umeme wa gridi ya Taifa kutoka Wilayani Chato, Rais Dk. John Magufuli, aliridhia na kutoa Sh milioni 778 ili kuweza kukamilisha kazi hiyo.

Kutokana na hali hiyo Waziri Dk. Kalemani, amesema kuwa mkakati wa Serikali kuunganisha Mkoa wa Kagera kwenye umeme wa gridi ya Taifa ambao ni wa uhakika katika kufanikisha uchumi wa viwanda kwa kjuwa na nishati ya uhakika na yenye usalama.

“Kuzinduliwa kwa umeme huu wa gridi ya Taifa sasa kuzifanya Wilaya za Muleba, Biharamulo na Ngara sasa kuwa na umeme wa uhakika wa hapa nchini kwetu. Tena umeme huu ni salama zaidi maana awali tulikuwa tunategemea umeme kutoka kwa wenzetu nchi ya Uganda jambo ambalo hata wakizima kule hatuna la namna ya kuuliza.

“Na ninafuraha kubwa kuwaambia kwamba mkataba wa kazi hii ya ulikuwa ni wa miezi miwili ambapo Juni 2, mwaka huu ulisaini na kuwekeana malengo kwamba hadi kufikia Agosti 2, mwaka huu kazi hii iwe imekamilika. Lakini leo (jana) ninafuraha kuona kazi hii imekamilika wiki moja kabla ya muda wa mkataba,” amesema Dk. Kalemani

Kutokana na hali hiyo, aliwataka wananchi wa Kijiji cha Nyamagojo, kuhakikisha wanatumia muda ambao wakandarasi wa wanaotekeleza REA III, kuunganisha umeme kwa gharama nafuu kwani lengo la Serikali ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma ya umeme hata ikiwa kwa lazima.

“Kati ya vijiji zaidi ya 600 vya Kagera ninafuraha kuwambia hadi sasa vijiji zaidi ya 400 vina umeme lakini kuna vijiji zaidi ya 100 navyo wakandarasi wapo site wanaendelea na kazi. Hivyo ni vema wananchi wakati muda huu wakandarasi wakiendelea na kazi ya kuunganisha vijiji umeme lipieni Shilingi 27,000 ili muweze kuunganishiwa huduma ya umeme ndani ya siku saba.

“…pia unaweza kulia hata kidogo kuanzia Shilingi 10,000  na kuendelea kulipa hadi utakapokamilisha Shilingi 27,000 unaunganishiwa umeme.

“Ninawataka maneja wa Tanesco nchi nzima kuhakikisha mnatafanyakazi hii ikiwamo kwenda kukagua miradi na yule ambaye hawezi kwenda na kasi hii tutamuondoa ili aweze kupisha waliokuwa tayari kufanyakazi,” amesema Dk. Kalemani

Awali kwa kiwasilisha taarifa kwa Waziri kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Richard Muyango, amesema hatua ya kuunganisha mkoa huo kwenye gridi ya Taifa, sasa kutaufanya mkoa huo kuwa na umeme wa uhakika.

“Tunawakaribisha wawekezaji waje kujenga viwanda vidogo na vikubwa hapa Muleba, sasa nasi tuna umeme wa uhakika ambao ndio suluhisho ya uhakika kwa uchumi wa kati na wa viwanda katika nchi yetu.

“Tunamshukuru sana Rais Dk. John Magufuli kwa kweli amefanyakazi kubwa kwetu wana Kagera kwa kuhakikisha wanapata maendeleo ya uhakika katika mkoa wetu, asante sana Rais Magufuli na tunaomba Mheshimiwa Waziri (Kalemani) utufikishie salamu zetu,” amesema DC Muyango.

Pamoja na hali hiyo pia aliwasha umeme katika vijiji vya Nyamagojo katika Jimbo la Muleba Kusini  na Nundu upande wa Muleba Kaskazini.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad