Waziri katika Afisi ya Makamo wa pili wa Rais, Mhe Mohamed Aboud Mohamed |
Na Salama Njani – Habari Maelezo Zanzibar
Serikali
ya Mapinduzi Zanzibar imesema itawachukulia hatua za kisheria wale wote
watakaobainiika kufanya uzembe uliosababisha kuzama kwa meli ya Spice
Islanders huko katika mkondo wa Nungwi hapo jana na kusababisha vifo vya
watu kadhaa.
Akizungumza
na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa Wizara ya Habari Utamaduni
Utalii na Michezo mjini Zanzibar , Waziri katika Afisi ya Makamo wa pili
wa Rais, Mhe Mohamed Aboud Mohamed amesema,kuwa kamati maalum itaundwa
ili kuchunguza juu ya ajali hiyo na ikibainika kuwa uzembe umepatikana
sheria itachukua mkondo wake.
Mhe
Aboud amesema kuwa Serikali hivi sasa imejikita zaidi katika suala la
uokoaji na kubainisha waliofariki ili watakaotambuliwa waweze familia
zao kwa mazishi na wale ambao hawatotambulika Serikali inachukua jukumu
la kuwazika.
Amesema
kuwa uchunguzi ni kitu cha lazima ili kujua ukweli ulivyo na kama
makosa yametokezea yaweze kurekebishwa na yale ambayo yakitokea kwa
uzembe uliofanywa basi hatua za sheria zitachukua mkondo wake na
Serikali haitosita kufanya hivyo.
Mhe
Waziri amesema kuwa tatizo kubwa la wazanzibari ni muhali, na amesema
ili utendaji mzuri uwepo, lazima suala hili la muhali liwekwe upande ili
nchi ipige hatua za maendeleo, na ikibainika kuna watu wanafanya uzembe
wa kikazi lazima hatua za kisheria zichukuliwe hapo hapo, na Serikali
hii itafanya hivyo .
Akijibu
swali kuhusu tatizo la usafiri na uwezekano wa Serikali kumiliki meli
zake ambazo zitahakikisha kuwa na usalama zaidi amesema, ni kweli tatizo
la usafiri lipo, lakini serikali kupitia mfumo wa Uchumi na biashara
huru, imetoa fursa ya watu binafsi kuanzisha na kumiliki vyombo vya
usafiri, ili kutoa fursa zaidi ya biashara na ukuaji wa Uchumi.
Hata
hivyo amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatafakari juu ya
suala hilo ili kuona vipi wanaweza kufanya vizuri katika kazi ya kuwa
na meli, kwani uzoefu umeonekana kuwa bado Zanzibar haijawa na wataalamu
wa kutosha kuliendesha Shirika la Meli, na Serikali kuogopa kuingia
katika suala hilo kwani Mashirika mengi yamekufa.
Kuhusu
Nahodha wa Meli hiyo amesema kuwa mpaka hivi sasa bado hajapatikana na
haieleweki kuwa yuhai au amefariki lakini muhandisi wake yuhai na
ameokoka na hivi sasa anachukuliwa Maelezo na vyombo vinavyohusika.
Akijibu
juu ya suala la jina na mmiliki wa kampuni hiyo amesema kuwa mpaka sasa
hawamjui mmiliki wa kampuni ya Meli hiyo,lakini atawapatia jina la
kampuni hiyo baada ya kuwauliza wahusika.na kutoa wito kwa waandishi hao
kuwasiliana na Wizara ya Miundo mbinu na Mawasiliano Zanzibar.
Akielezea
juu uokozi unavyoendelea amesema kuwa maiti tano zaidi zimepatikana hii
leo na kufanya idadi ya waliofariki kuwa 197 na kazi ya uokoaji
inaendelea.
Wakati
huo huo Serikali ya Jamhuhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa mchango
wake wa maafa wa shilingi milioni mia tatu ambapo pia shilingi kumi na
tatu milioni za msaada kama huo zimetolewa na Mfuko wa hifadhi ya Jamii
wa Tanzania (NSSF) na shilingi milioni kumi zimetolewa na Mfuko wa
hifadhi ya Jamii Zanzibar ZSSF) pia kampuni ya simu ya Tigo imetoa
chakula cha msaada chenye thamani ya shilingi milioni tano.
Aidha
shilingi laki tano zimetolewa na mwananchi ambae jina lake hakutaka
litajwe kwa ajili ya kusaidia maafa hayo.ambapo pia kesho jioni
kutakuwapo na kisomo maalum kilichotayarishwa na Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar cha kuwaombea dua waliofariki pamoja na waliofikwa na maafa
hayo hapo katika kiwanja cha Maisara Zanzibar.
No comments:
Post a Comment