Chakechake, Pemba – 24 Septemba 2025
MGOMBEA wa nafasi ya Rais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewahakikishia wananchi wa Pemba kuwa Serikali itaendelea kuweka uwiano sawa katika miradi ya maendeleo kwa Unguja na Pemba.
Akizungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali wa soko la Chakechake, Mkoa wa Kusini Pemba, Dkt. Mwinyi amesema miradi mbalimbali imekuwa ikitekelezwa kwa usawa ikiwemo sekta za miundombinu, elimu, afya na nyinginezo.
Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kulilinda na kuliimarisha soko la asili la Chakechake ili libakie na uasili wake, huku ikipanga kujenga soko jipya la kisasa.
Aidha, akigusia suala la uwezeshaji wananchi kiuchumi, Dkt. Mwinyi amesema katika awamu ijayo Serikali itaongeza mara dufu fedha za uwezeshaji ili kuhakikisha kila mjasiriamali anapata mkopo bila kuachwa nyuma.
Kuhusu kodi, ameeleza kuwa Serikali italifanyia kazi kwa kina suala la msururu wa kodi na kuweka utaratibu wa kodi nafuu kwa wafanyabiashara.
Dkt. Mwinyi amewataka wananchi wa Pemba kumpa ridhaa nyingine kupitia sanduku la kura ili aendelee kuwaletea maendeleo zaidi.
No comments:
Post a Comment