KAMPUNI ya Bakhresa Group (SSB) katika kuadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, imefanya upanuzi wa kiwanda chake cha vinywaji baridi cha Bakhresa Food Products Ltd (BFPL) kwa kufunga mitambo mipya ya kisasa ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya wateja wake.
Akizungumza na waandishi wa habari Juni 19, 2025, katika kiwanda hicho kilichopo Mwandege, mkoani Pwani, Afisa Ubora wa BFPL, Charles Hayola, amesema kabla ya upanuzi huo, kampuni ilikuwa na changamoto ya kuhudumia mahitaji yote ya wateja kutokana na uwezo mdogo wa uzalishaji.
“Awali tulikuwa tukizalisha kati ya katoni 150,000 hadi 200,000 kwa siku, lakini sasa baada ya kufunga mitambo mipya, tuna uwezo wa kuzalisha kati ya katoni 250,000 hadi 300,000 kwa siku,” alisema Hayola.
Amefafanua kuwa kampuni hiyo inazingatia viwango vya ubora tangu hatua ya upatikanaji wa malighafi hadi uzalishaji, kwa kuzingatia miongozo ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) pamoja na viwango vya kimataifa (ISO).
Kwa upande wake, Meneja Ubora wa Kitengo cha Matunda, Bi. Bakila Elson, amesema kampuni imekuwa ikiwaelimisha wakulima kuhusu aina na ubora wa malighafi wanaozihitaji. Malighafi hizo hupitia hatua mbalimbali za uchambuzi ili kuhakikisha bidhaa bora na salama.
Bakhresa Food Products Ltd imekuwa miongoni mwa kampuni zinazoongoza kwa kutoa ajira, ambapo zaidi ya watu 1,000 wameajiriwa moja kwa moja. Kampuni hiyo pia imekuwa mstari wa mbele katika kuongeza thamani ya mazao ya matunda yanayozalishwa nchini, hivyo kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.



























No comments:
Post a Comment