Jeshi la Polisi nchini limetenga siku 14 kwa ajili ya mpango maalum wa kukutana na kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya kijamii mkoani Geita ili kupunguza, kudhibiti au kutokomeza uharifu mkoani hapa.
Timu ya Jeshi la Polisi kitengo cha Polisi Jamii ikiongozwa na Kamishina wa Polisi Jamii Tanzania, Faustine Shilogile iliwasili mkoani Geita Aprili 03, 2025 na itakuwaepo kwa muda wa wiki mbili hadi Apili 17, 2025.
Shilogile amewasilisha mpango huo katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Geita na kueleza kuwa zoezi hilo limeratibiwa na Jeshi la Polisi kwa Ushirikiano na Kampuni ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML).
Shilogile ametaja miongoni mwa programu itakayofanyika ni kuzungukia na kuzungumza na wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi wa GGML ili wawe sehemu ya kuulinda mgodi huo wenye tija kubwa nchini.
Amesema pia watakutana na askari kata kutoka kata zote 122 za mkoa wa Geita ili kuendelea kuwajengea uwezo wa kuimarisha ulinzi na usalama sambamba na kuwachukulia hatua wale wanakengeuka.
Shilogile ameongeza kuwa, dhamira ya jeshi la polisi ni kupeleka polisi kata kwenye kata zote 3,956 za Tanzania bara pamoja na Shehia 384 kwa Zanzibar ili kudhibiti uharifu.
Ofisa Polisi Jamii Taifa, Elisante Ulomi amesema wameamua kuwekeza kwenye mpango wa polisi jamii kama njia ya kupunguza uharifu mkoani Geita kwani ni njia isiyo na gharama na inahusisha mfumo shirikishi.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita, Safia Jongo amesema mpaka sasa juhudi kubwa zimefanyika kupunguza uharifu kwa kuifanya jamii iamini polisi wanafikika, wanasikia na polisi wanatoa msaada.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Gombati amekiri mbali na juhudi zilizofanywa na mkoa, mpango huo utaongeza ari ya kudhibiti uharifu kwa makundi yote na kuifanya Geita kuwa eneo salama.
No comments:
Post a Comment