HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, May 18, 2023

TGNP WATOA MAFUNZO KWA WATENDAJI 45 WA KATA, WAASWA KUPANGA BAJETI ZENYE JICHO LA KIJINSIA

MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) watoa mafunzo kwa watendaji 45wa kata sita kutoka Mkoa wa Dar es Salaam na Shinyanga.

Akizungumza leo Mei 18, 2023, wakati wa kufungua mafunzo hayo Mtafiti na Mchambuzi kutokaTGNP Zainabu Mmari akimwakilisha Mkurugenzi amesema kuwa bajeti za taifa, mipango, taratibu na mikakati yote inatakiwa kuwa na mtizamo wa kijinsia kwa kulenga makundi yote yafaidi rasilimali za nchi.

Amesema kuwa lengo la kutoa mafunzo hayo ni kuwa na uelewa wa pamoja na kushirikishana uzoefu na kuhakikisha mipango na bajeti zinakuwa kwa mrengo wa kijinsia.

"Na kuangalia yatokanayo na mafunzo ya mwaka jana wameweza kwenda kutumia mbinu na kuweza kutambua mbinu zinazotakiwa katika kupanga bajeti zenye mrengo wa kijinsia na makundi maalumu hasa kwenye madawati yanu na kuwapa elimu viongozi wengine wa serikali za mitaa na Kata.

Na je ni vitu gani vimefanyika kutokana na semina ya mwaka jana, na hili TGNP tunalifanya ili tuweze kujifunza ni kitu gani kimefanyika vizuri katika kata na sehemu nyingine havijafanyika ili wengine waweze kutekeleza kulingana na mafunzo wanayoyapata." Amesema

Amesema kuwa watabadilishana uzoefu wa watendaji wa kata moja na nyingine, pia wataangalia kwa namna gani kata zimefanya vizuri na kuweza kuiga yale mazuri na kuangalia changamoto zinazowakabili.

Zainabu amesema kuwa bajeti za Halmashauri zikipangwa kwa kushirikisha makundi yote zitaleta Tanzania yenye usawa, huru na watu wake waweze kufurahia matunda nchi lakini pia kwenye mipango, bajeti na mikakati yote inakuwa katika mrengo wa kijinsia kuanzia ngazi ya chini kabisa, ya familia ya kijiji ya kata na hatimaye Wilaya, halmashauri na bajeti ya kisekta na taifa kwa ujumla.

Akizungumzia mwenendo wa mafunzo hayo ya kila mwaka Zainabu amesema kuwa wameanza kuona viashiria mbalimbali vinatekelezwa na serikali kutokana na kutoa mafunzo kwa watumishi wa serikali kuanzia ngazi ya chini.

Kwa Upande wa mtendaji kutoka Wilaya ya Kishapu, amesema kuwa katika kata yake wameweza kupanga bajeti inayolenga makundi yote kwa upande wa walemavu amesema kuwa wameweza kututengeneza miundombinu inayowasaidia watu wenye ulemavu katika majengo ya Serikali ili na wao waweze kunufaika na rasilimali za serikali.

Kwa kufanya hivyo wameweza kushilikishwa na kuwatia moyo walemavu na wao wameweza kushiriki katika shughuli za maendeleo.

Amesema mafunzo hayo yameweza kuwasaidia katika utengaji wa bajeti katika ngazi mbalimbali ili kuleta manufaa kwa jamii.

Amesema mwazoni kabla ya mafunzo hayo walikuwa wanatenga bajeti ambazo hazina jicho la kijinsia kwa kuwa kwa sasa tumeweza kusogeza huduma karibu na jamii ambazo zinaweza kusaidia jinsia zote kupata huduma hizo bila kutumia nguvu nyingi na bila kupoteza muda mwingi ambao ungesaidia katika kufanya shughuli za kimaendeleo.

Akizungumzia kuhusiana na mahitaji mbalimbali ya kijinsia Mtoa Mada  Iddi Rajabu Mohamed amesema kuwa wanaume walikuwa na mzigo mkubwa wa kuhudumia jamii hivyo kwa sasa kila mtu anaweza kuhudumia jamii bila kikwazo chochote.

Mafunzo haya yameanza kuzaa matunda mema hasa kwenye bajeti hizi zinazotengwa, hata ukiangalia shule kwa sasa wameweka huduma ya maji na sehemu ya kujisitiri kwa wanafunzi wa kike pale wanapokuwa katika kipindi cha hedhi."

Amesema hayo ni matokeo ya mafunzo yanayotolewa na TGNP na viongozi mbalimbali wa serikali wameanza kuelewa na kupanga bajeti ambazo zinalenga makundi yote.

Akizungumzia mapungufu katika bajeti kwa kundi fulani katika kuleta maendeleo amesema kuwa ni viongozi wa ngazi mbalimbali kukosa uelewa na ndio wanaochelewesha maendeleo katika maeneo yao.

Pia amesema kuwa serikali haikuweka kipaumbele masuala ya bajeti za kijinsia yanayoleta maendeleo ya kwa miaka ya kadhaa ya nyuma.

Afisa Mtendaji wa Mabwepande Othman Mtono amesema kuwa mafunzo hayo yatamwezesha kupanga bajeti yenye mrengo wa kijinsia kuanzia katika familia yake hadi kufikia kwenye kata kwani italeta chachu katika jamii.

Akizungumzia faida walizozipata amesema kwa sasa hakuna mradi unaopita bila kuzingatia masuala ya kijinsia kwa kuwa masuala ya kijinsia ni masuala mtambuka na yanaleta maendeleo katika eneo husika.

"Kwa sasa hivi hatuwezi kutekeleza mradi, au kujenga hospitali bila kuangalia makundi maalaumu hasa walemavu, kuwa na miundombinu inayowawezesha na kufaidi matunda mema ya nchi kupitia bajeti zinazopangwa." Amesema Mtono.

Amesema katika kata yake wanazingatia na umiliki wa ardhi pia wanashirikisha jinsia zote ili kila Mwanamke na mwanaume waweze kupata ardhi.

Kwa upande wa mtendaji kata wa Saranga, Ester Nyambo amesema kuwa halmashauri zinawashirikisha katika upangaji wa bajeti ili waweze kuwashirikisha wananchi kupitia mikutano ya maeneo wanayoishi.

Amesema kuwa mambo mengi wamekuwa wakishiriki wanaume lakini kwa sasa wameanza kuona na ushiriki wa wanawake umekuwa mwingi pia katika mikutano wanawake wamekuwa wakichangia hoja za kuleta huduma za maendeleo.
Mtafiti na Mchambuzi kutoka Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Zainabu Mmari akizungumza wakati wa kufungua mafunzo kwa watendaji wa kata kutoka mkoa wa Dar es Salaam na Shinyanga Wilaya ya Kishapu. Mafunzo hayo yamefanyika jijini  Dar es Salaam leo Mei 18, 2023.
Mtoa mada, Iddi Rajabu Mohamed akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo wakati wa mafunzo ya watendaji wa kata 45 jijini Dar es Salaam leo Mei 18, 2023.


Baadhi ya watendaji wa kata wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Mei 18, 2023 wakati wa mafunzo ya watendaji wa kata wa wilaya za Dar es Salaam na Shinyanga.






Baadhi ya watendaji wa kata wakisikiliza mtoa mada  jijini Dar es Salaam leo Mei 18, 2023 wakati wa mafunzo ya watendaji wa kata wa wilaya za Dar es Salaam na Shinyanga.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad