TAASISI zisizo za serikali, zimeipongeza serikali kwa kuwa na bajeti nzuri ambayo itawawezesha kutimiza majukumu yake sambamba na kuwainua Watanzania.
Aidha, zimeomba uwekezaji zaidi katika miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa na wa kufua umeme ili kuweza kutoa huduma kwa watanzania.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Taasisi za Kampuni ya EY Tanzania na Multi-choice Tanzania (DSTV) wakati wa mkutano wa uliondaliwa na kampuni hiyo kuangalia mabadiliko ambayo yamefanywa na serikali kwenye bajeti kuu ya mwaka 2022/2023 na fursa mpya zilizoletwa na bajeti hiyo.
Meneja Mkaazi wa Kampuni ya EY Tanzania, Joseph Sheffu amesema bajeti hiyo inavutia kwa watanzania kwa sababu serikali imeondoa ushuru kwenye malighafi za kutengeneza mbolea, maziwa , vifungashio, mbegu za majani kwa ajili ya malisho, vifaa vya jeshi, mafuta ya kipikia, pembejeo za kilimo na vitu vingine.
Amesema bajeti hii itapunguza gharama za uzalishaji, itaongeza ajira na kuvutia uwekezaji hapa nchini.
Anasema bajeti Kwa ujumla imekuja katika kipindi ambacho kinachangamoto, hali ya uchumi duniani imeshuka, Na hali ya uchumi wa Tanzania pia ilishuka.
Anasema bajeti imeweka matarajio kuwa hali ya uchumi itakuwa Kwa asilimia 5.3, asilimia hii ipo juu ya ukanda wa Kati wa Africa.
Aidha, amesema Mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway (SGR), Mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere na kufufua Shirika la ndege la Tanzania (ATCL), maeneo hayo bado yanahitaji uwekezaji.
Amesema kama maeneo hayo yote yatafanyiwa kazi itachochea ukuaji wa uchumi na biashara na itawezesha serikali kutekeleza majukumu yake.
Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa Multi-Choice Tanzania (DSTV), Jackline Woiso ameipongeza Serikali kwa kuongeza bajeti ya kilimo kutoka asilimia 40 hadi 155, akisema ni ongezeko kubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
Alisema hii itawanufaisha watu wanaojihusisha na sekta ya kilimo hasa wale wa sekta za uvuvi, wafugaji, nishati na biashara.
“Pia tunafurahi kuona serikali inapunguza tozo ya miamala ya fedha kwa njia ya simu katika kutuma na kutoa tozo,” amesema Woiso.
Katika mijadala ya bajeti ya sasa inayoanza kutumika Julai Mosi mwaka huu, serikali imepunguza tozo za kutuma na kutoa hadi kiwango cha juu cha miamala ya kiwango cha Sh 4,000 kutoka Sh 7,000 za sasa.
Amesema hatua hiyo ya serikali itawavutia Watanzania wengi zaidi nchi nzima kutumia miamala ya pesa kwa njia ya simu.
Pia aligusia ushirikishwaji wa fedha akisema umesababisha kupunguzwa kwa Kodi ya VAT kwenye huduma za kifedha ambazo zitavutia makampuni ya simu na taasisi nyingine za fedha kupanua huduma zake za kibenki za mawakala katika maeneo yasiyo na taasisi za fedha.
"Bado tunayo mambo yanayoweza kutozwa ushuru, lakini hatuyazingatii," alisema huku akisisitiza serikali kuangalia maeneo mengine ambayo inaweza kutozwa kodi mbali na makampuni ya simu.
Akizungumzia mabadiliko ya fedha, Mkurugenzi Mshiriki wa EY, Huduma za Ushauri wa Kodi, Beatrice Melkiory amesema wakati wa mapitio ya bajeti kwamba ukusanyaji wa kodi ni njia bora ya kuongeza mapato.
Amesema iwapo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) itakuwa na usimamizi mzuri wa kodi, hii inaweza kuongeza ulipaji kodi na kisha Serikali kufikia lengo na kupata mapato zaidi.
Ameshauri mfumo wa kodi kuhakikisha mifumo ya Ushuru inaendana na sheria za kodi na si vitendo, ili kuwapa walipa kodi muda wa kutosha wa kutuma maombi ya marejesho yao ya kodi.
Amesema pia kulikuwa na haja ya kuanzisha kodi kwa wachimbaji wadogo wa madini ili kuiwezesha mamlaka ya mapato TRA kupata mapato zaidi na kufikia malengo ya serikali.
Monday, June 20, 2022

Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment