Na Mwandishi wetu, Malabo
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania imezishauri nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) kuwa na
mpango mkakati wa pamoja katika kupambana na masuala ya ugaidi na
majanga ya kibinadamu.
Akitoa pendekezo la Tanzania katika
Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika
uliomalizika jana usiku Malabo, Equatorial Guinea, Waziri wa Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb)
ambaye alimwakilishwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.
Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania inapendekeza Umoja wa Afrika uwe na
mpango mkakati utakaosaidia kuhakikisha kuwa nchi wanachama wanakwenda
pamoja lakini pia kusaidiwa kujengewa uwezo wa kupambana na vitendo vya
kigaidi.
“Hakuna nchi hata moja inaweza kusema iko salama kwani
vikundi vya kigaidi viko sehemu mbalimbali hivyo kwa kutumia mpango
mkakati wa umoja na mshikamano ni rahisi kukabiliana na ugadi…..kwa hiyo
ujumbe wetu Tanzania kwa (AU) ni kwamba twende pamoja katika kutokomeza
ugaidi,” amesema Balozi Mulamula
Balozi Mulamula ameongeza kuwa
Mkutano huo pia umetoa tamko la pamoja la kuimarisha utekelezaji wa
mikataba mbalimbali iliyopitishwa miaka mingi pamoja na kuhakikisha
Baraza la Amani na Usalama linakuwa na mpango maalum wa kufuatilia
nyendo za kigaidi na kuzitokomeza.
“Baraza la Amani na Usalama
pia litasaidia katika kuimarisha amani na usalama kupitia ‘stand by
force’ ili kuweza kuingilia na kusaidia kuzuia machafuko pindi
yanapojitokeza na kutokomeza vitendo kama hivyo vya kigaidi,” aliongeza
Balozi Mulamula
Akielezea kuhusu Mkutano wa 15 wa Dharura wa
Wakuu wa Nchi na Serikali, Balozi Mulamula alisema kuwa Tanzania
imeziomba nchi wanachama kuimarisha ushirikiano na utekelezaji wa pamoja
wa utoaji wa huduma za kibinadamu ikiwemo tahadhari za mapema ambazo
zinahitaji kupitiwa upya, kuendelezwa na kuimarishwa kwa ajili ya kupata
utabiri na tafsiri sahihi ya majanga yatakayotokea na kuyafanyia kazi
ipasavyo.
Tanzania pia imeuomba Umoja wa Afrika kuwa na
ushirikiano na utekelezaji wa pamoja katika utoaji wa huduma za
kibinadamu hasa jukumu la kuhifadhi wahamiaji na wakimbizi.
Aidha,
mkutano wa 15 na 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali uliridhia
kuzizuia nchi nne ambazo kushiriki mikutano ya Umoja wa Afrika kutokana
na Mabadiliko ya Serikali yasiyozingatia misingi ya Katiba ikiwemo
mapinduzi ya kijeshi nchi hizo ni Mali, Burkina Faso, Guinea na Sudan.
Kwa
upande wake, Rais wa Cameroon na Mwenyekiti wa Baraza la Amani na
Usalama, Mhe. Paul Biya amezitaka nchi wanchama wa Umoja wa Afrika
kushughulikia masuala ya kigaidi kwa umoja na mshikamano kwani bila
kufanya hivyo mambo hayo hujenga na kuchochea itikadi kali hasa miongoni
mwa vijana ambao ni idadi kubwa ya watu katika Bara la Afrika.
“Zaidi
ya asilimia 60 ya idadi ya watu barani Afrika ni vijana. Kwa hiyo ni
lazima nchi wanchama wa Umoja wa Afrika kujitahidi kuweka mazingira
mazuri ya ushirikishwaji wa vijana na wanawake katika michakato ya amani
na maendeleo katika ngazi ya kitaifa, kikanda na bara,” amesema Mhe.
Biya.
Wakuu wa Nchi na serikali katika Mkutano wa 16 wa Dharura
waliridhia kwa pamoja kuwa kila mwaka tarehe 31 Januari kuwa siku ya
Amani na maridhiano Barani Afrika na Rais wa Angola Mhe. João Lourenço
atakuwa kinara ‘champion’ wa masuala ya amani.
Rais
wa Equatorial Guinea, Mhe. Teodoro Obiang Nguema Mbasogo akihutubia
katika Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa
Afrika (AU) uliomalizika jana usiku Jijini Malabo, Equatorial Guinea
Mwenyekiti
wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Bw. Moussa Faki Mahamat akihutubia
katika Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa
Afrika (AU) uliomalizika jana usiku Jijini Malabo, Equatorial Guinea
Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata
Mulamula ambaye amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa
Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) akifuatilia mkutano huo
ulimalizika jana usiku Jijini Malabo, Equatorial Guinea
Balozi
wa Tanzania nchini Ethiopia ambaye anawakilisha pia Umoja wa Afrika,
Mhe. Innocent Shiyo (mwenye tai nyekundu), Mkurugenzi wa Idara ya Afrika
katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Balozi Naimi Aziz pamoja na watumishi wengine waandamizi wa Serikali
wakishiriki katika mkutano
Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata
Mulamula katika picha ya pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia
ambaye anawakilisha pia Umoja wa Afrika, Mhe. Innocent Shiyo, Mkurugenzi
wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Afrika Mashariki, Balozi Naimi Aziz pamoja na watumishi wengine
waandamizi wa Serikali
Sehemu
ya Wakuu wa Nchi na Serikali pamoja na Wawakilishi wa Wakuu wa Nchi na
Serikali wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ufunguzi wa mkutano wa
Mkutano wa 16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika
(AU) ulimalizika jana usiku Jijini Malabo, Equatorial Guinea
Wakuu
wa Nchi na Serikali pamoja na Wawakilishi wa Wakuu wa Nchi na Serikali
wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ufunguzi wa mkutano wa Mkutano wa
16 wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).
Mkutano huo ulimalizika jana usiku Jijini Malabo, Equatorial Guinea
No comments:
Post a Comment