Na. Damian Kunambi, Njombe
Mkuu
wa Wilaya ya Ludewa Andrea Tsere amewaagiza Viongozi wote wa ngazi ya
kata na vijiji kutoa elimu kwa wafugaji wa ng'ombe juu ya zoezi la
uvishaji hereni kwa mifugo hiyo ili kuweza kutambua idadi yao katika
wilaya hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake
mkuu huyo ameongeza kuwa hereni hizo zitasaidia kujua afya ya
mifugo,uhitaji wa maeneo ya malisho na kupunguza migogoro ya wakulima na
wafugaji hivyo amewataka wafugaji kuonyesha ushirikiano wao ili
kufanikisha zoezi hilo.
Amesema katika zoezi hilo kwa asilimia
kubwa limegharamiwa na serikali hivyo kwa upande wa wafugaji watapaswa
kugharamia hereni ambayo gharama yake haipungui shilingi 1500.
"Wafugaji
mnapaswa kuunga mkono zoezi hili kwakuwa lina faida kubwa sana kwenu,
kwani changamoto nyingi zinazohusiana na mifugo zitakwenda kumalizika",
Amesema Tsere.
Ameongeza kuwa endapo ng'ombe atavaa hereni
atakuwa ameunganishwa katika mfumo wa computer ambao utawezesha kujua
afya yake, eneo alilopo na hata ikitokea anaibiwa inakuwa rahisi
kupatikana.
Sanjari na hilo pia amewataka wafugaji wa ng'ombe
kufugia mifugo yao kwenye mazizi badala ya kuwaacha milimani
wakijichunga wenyewe kitu ambacho huleta uharibifu wa miundombinu ya
barabara, maji na mfugaji hupoteza mavuno mengi yanayotokana na ng'ombe.
Amesema
mifugo hiyo inapokuwa peke yake porini inakosa uangalizi wa karibu hasa
wanapokuwa na watoto (Ndama) kwani ndama hao hupoteza maisha kwa
kutumbukia katika mitaro na magonjwa mbalimbali.
"Kuacha ng'ombe
porini tunapoteza mazao ya mifugo yetu, mbolea na hata maziwa ambayo
tungeweza kuyatumia kwa afya ya binadamu tunayaacha yananyonywa na
sungura huko maporini", Amesema Tsere.
No comments:
Post a Comment