Wataalamu
wa magonjwa ya moyo na wazibuaji wa mishipa ya damu ya moyo wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimfanyia mgonjwa upasuaji mgumu
(Complex Percutaneous Coronary Intervention – PCI) wa kuzibua mshipa wa
moyo uliokuwa umeziba kwa asilimia 99 na hivyo kushindwa kupitisha damu
vizuri kwa njia ya tiba mtandao (Telemedicine). Wataalamu kutoka
Shirika la madaktari Afrika waliopo Hospitali ya Central jimbo la
Virginia nchini Marekani walikuwa wanatoa maelekezo ya jinsi ya kuzibua
mshipa huo kwa wenzao wa JKCI waliopo nchini Tanzania.
Wataalamu
wa magonjwa ya moyo na wazibuaji wa mishipa ya damu ya moyo wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja mara baada
ya kumaliza kumfanyia mgonjwa upasuaji mgumu (Complex Percutaneous
Coronary Intervention – PCI) wa kuzibua mshipa wa moyo uliokuwa umeziba
kwa asilimia 99 na hivyo kushindwa kupitisha damu vizuri kwa njia ya
tiba mtandao (Telemedicine). Wataalamu kutoka Shirika la madaktari
Afrika waliopo Hospitali ya Central jimbo la Virginia nchini Marekani
walikuwa wanatoa maelekezo ya jinsi ya kuzibua mshipa huo kwa wenzao wa
JKCI waliopo nchini Tanzania.
Picha na JKCI
……………………………………………………………….
Na Mwandishi Maalum – Dar es Salaam
Kwa
mara ya kwanza wataalamu wa magonjwa ya moyo na wazibuaji wa mishipa ya
damu ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamefanya
upasuaji mgumu (Complex Percutaneous Coronary Intervention – PCI) wa
kuzibua mshipa wa moyo uliokuwa umeziba kwa asilimia 99 na hivyo
kushindwa kupitisha damu vizuri kwa njia ya tiba mtandao
(Telemedicine).
Upasuji
huo uliochukuwa muda wa saa moja umefanyika leo kwa kutumia mtambo wa
Cathlab (Catheterization Laboratory) Carto 3 System 3d & Mapping
Electrophysiology system ambapo wataalamu kutoka Shirika la madaktari
Afrika waliopo Hospitali ya Central jimbo la Virginia nchini Marekani
walikuwa wanatoa maelekezo ya jinsi ya kuzibua mshipa huo kwa wenzao wa
JKCI waliopo nchini Tanzania.
Akizungumza
mara baada ya kumaliza kufanya upasuaji huo Daktari bingwa wa magonjwa
ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Peter Kisenge alisema
wameweza kuzibua mshipa ambao ulikuwa umeziba kwa kiasi kikubwa kwa
kufuata maelekezo ya moja kwa moja ambayo yalikuwa yanatolewa kwa njia
ya mtandao wa zoom kutoka kwa wenzao waliopo nchini Marekani.
“Tangu
tumeanza kufanya upasuaji mdogo wa kuzibua mishipa ya damu kwa njia ya
tundo dogo linalotobolewa kwenye paja au mkono kwa kutumia mtambo wa
Cathlab mwaka 2014 Madaktari Afrika kutoka nchini Marekani ndiyo
waliokuwa wanatuelekeza na kutusimamia hadi tumeweza kufanya upasuaji
huu sisi wenyewe”,.
“Hata
leo wametuelekeza kwa njia ya mtandao jinsi ya kufungua mshipa huu
ambao ulikuwa umeziba kwa kiasi kikubwa kwani wenzetu hawa wanautaalamu
mkubwa zaidi kuliko sisi . Iwapo atatokea mgonjwa mwenye tatizo kama
hili tutaweza kumfanyia upasuaji kama tulivyofanya kwa mgonjwa huyu”,
alisema Dkt. Kisenge.
Mtaalamu
huyo wa uzibuaji wa mishipa ya damu ya moyo alisema miaka ya nyuma
upasuaji kama huo ulikuwa unafanyika nje ya nchi, lakini kutokana na
kuwepo kwa vifaa vya kisasa pamoja na wataalamu wa kutosha hivi sasa
huduma kama hizo zinatolewa hapa nchini katika Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI).
“Kama
mgonjwa huyu angetibiwa nje ya nchi gharama za matibabu zingekuwa ni
zaidi ya shilingi milioni 20 lakini mgonjwa huyu ametibiwa hapa nchini
kwa gharama ya shilingi milioni sita , kwa kuwa mgonjwa huyu amejisajili
na mfuko wa Taifa wa bima ya afya (NHIF) gharama zote za matibabu
zimelipwa na bima hii. Ninawashauri wananchi wajiunge na NHIF kwani
pindi watakapoumwa watalipiwa gharama za matibabu”, alisisitiza Dkt.
Kisenge.
Naye
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI Khuzeima Khanbhai ambaye
alishiriki katika upasuaji huo alisema tukio hilo ni la kihistoria kwa
kushirikiana na Madaktari Afrika waliopo nchini Marekani wameweza
kuzibua mshipa ulioziba kwa njia ya mtandao ingawa kuna tofauti ya muda
kwao ni saa sita usiku na Tanzania ni saa moja asubuhi wamekubali
kusaidia kumfanyia upasuaji mgonjwa.
“Unapofanya
upasuaji wa aina hii kuna njia mbili ambazo ni mshipa wa kwenye paja au
mkononi za kupitisha vifaa ili uweze kuufikia moyo”,. Kwa kuwa uzibuaji
huu ulikuwa ni mgumu tulitumia njia ya kwenye paja tukapitisha vifaa na
kuzibua mshipa huo, tunavyofanya upasuaji wa aina hii mgonjwa anakuwa
macho tunazungumza naye anachomwa sindano ya ganzi katika eneo husika
hii inatusaidia kuwa na mawasiliano ya moja kwa moja na mgonjwa”,.
“Wagonjwa
wenye matatizo ya kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo ni wengi kwa wiki
tunachunguza na kutibu wagonjwa kati ya 50 hadi 60 na kwa mwaka huu
huyu ni mgonjwa wa 1499. Kuna wagonjwa ambao wanakujakama wana tatizo
la gesi tumboni lakini baada ya vipimo wanaonekana mishipa yao ya damu
ya moyo imeziba”, anasema Dkt. Khuzeima.
Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi
alisema wamekuwa wakifanya kambi maalum za upasuaji mdogo ambao ni mgumu
wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo na Madaktari Afrika waliopo nchini
Marekani lakini kutokana na tatizo la Ugonjwa wa UVIKO- 19 madaktari hao
wameshindwa kuja nchini.
Prof.
Janabi alisema kuwepo kwa mtambo wa mpya wa Cathlab kumewasaidia
kupata maelekezo kutoka kwa wataalamu wa nje ya nchi wenye utaalamu wa
juu zaidi ya jinsi ya kufanya upasuaji ambao wataalamu waliopo nchini
hawawezi kuufanya.Wagonjwa wenye matatizo hayo walikuwa wanapelekwa nje
ya nchi lakini kwa msaada wa wataalamu wenzao wanaweza kuwatibu wagonjwa
hao hapa nchini.
“Zoezi
hili limeenda vizuri na siku ya Kesho au kesho kutwa mgonjwa atakuwa
ameruhusiwa na leo hii baada ya masaa 6 ataanza kutembea mwenyewe .
Ninaishukuru sana Serikali kwa uwekezaji mkubwa wa tiba ya magonjwa ya
moyo uliofanyika katika Taasisi hii”, alishukuru Prof. Janabi.
Kwa
upande wake mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji huo Mzee Owiti Wataye
alishukuru kwa huduma ya matibabu aliyoipata na kusema alikuja katika
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) akitokea Hospitali ya rufaa ya
Kanda ya Bugando akiwa na maumivu makali kwenye kifua upande wa kushoto
pia shingo na mgongo vilikuwa vinamuuma sana.
“Nilikuja
hapa nikiwa na maumivu makali ya kifua, shingo na mgongo shida hii
imekuwa ikinisumbua kwa muda wa miaka miwili, baada ya kuzibuliwa
mshipa wa moyo kwa sasa najisikia vizuri ingawa bado niko kitandani
lakini maumivu yamepungu kwa kiasi kikubwa”, anasema Mzee Wataye.
No comments:
Post a Comment