HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, October 24, 2021

JESHI LA POLISI RUVUMA LATOA MAFUNZO KWA MADEREVA WA MAGARI YA SERIKALI

Mkuu wa kikosi cha usalama Barabarani(RTO)Mkoa wa Ruvuma Salum Morimori akiongea jana wakati wa mafunzo ya siku moja kwa madereva wa magari ya Serikali mkoani humo yaliyofanyika katika Ofisi za kikosi cha usalama barabarani Msamala katika Manispaa ya Songea,katikati Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Joseph Konyo.
Baadhi ya madereva wa magari ya Serikali mkoa wa Ruvuma wakimsikiliza Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Joseph Konyo(hayupo pichani)wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa madereva hao yenye lengo la kuwakumbusha wajibu wao na kutii sheria za barabarani.
Kamnda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Joseph Konyo akiongea na madereva wa magari ya Serikali mkoani humo wakati wa mafunzo kwa madereva hao yenye lengo la kuwakumbusha majukumu yao hususani suala la kutii na kuzingatia sheria baada ya kubainika kuwa wao ni kati ya madareva wasiozingatia sheria na kutii alama za barabarani.

 Na Muhidin Amri, Songea

JESHI la Polisi mkoa wa Ruvuma kupitia kikosi cha usalama barabarani,limeendesha(limetoa) mafunzo  kwa madereva wa  idara mbalimbali za Serikali wakiwemo madereva wa  vikosi vya ulinzi na usalama vilivyopo katika mkoa huo.

Mafunzo hayo  yana lengo la kuwakumbusha uzalendo na kutii sheria,kanuni na taratibu za usalama barabarani kutokana na kuwa vinara wa kuvunja sheria kwa makusudi na chanzo cha ajali nyingi.

Akifungua mafunzo hayo jana,Kamanda wa Polisi mkoani Ruvuma Kamishina msaidizi wa Polisi Joseph Konyo, amewataka madereva hao kuacha tabia ya kuendesha magari kwa mwendo kasi kwa kuwa ni hatari  kwa maisha yao na  viongozi  wanao waendesha.

Amesema, madereva wanatakiwa kutambua kuwa magari ya Serikali yanatokana na fedha za wananchi, hivyo wana wajibu ya kutunza ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kuleta tija iliyokusudiwa ya kuboresha huduma na kuharakisha maendeleo.

“ukiwa unaendesha gari la Serikali kimsingi wewe ni mtumishi wa umma,kwa hiyo unawajibika kwa namna yoyote kulinda mali ya umma na viongozi unaye mwendesha”amesema Rpc Konyo.

Amesema, baadhi ya madereva wa magari ya Serikali wanatumia vibaya nafasi hiyo kwa kukiuka sheria  za barabarani makusudi ikiwemo mwendo kasi na kupita kwenye maeneo yenye alama kama vile vivuko kwa watembee kwa miguu bila kuchukua tahadhari.

Aidha amesema,wakati mwingine madereva wa Serikali wamekuwa watu wenye dharua kwani hata wanaposimamishwa na askari wa usalama barabarani hawataki kusimama,hivyo kuleta taswira mbaya kwa madereva wa magari binafsi na jamii.

Amesema,kitendo cha kutosimama na kuvunja sheria za barabarani kwa makusudi kimekuwa kero kwa watumiaji wengine na kinachafua sana  baadhi ya taasisi,kwa hiyo amewataka kubadilika na kuwa mfano mzuri kwa jamii.

Kamanda Konyo amesema, ni matumaini ya Serikali kupitia mafunzo yanayotolewa na Jeshi la Polisi madereva watabadilika na kuepuka kufanya mambo ya ovyo ambayo ni chanzo cha ajali na kuleta madhara makubwa kwao na watu wengine wasiokuwa na hatia.

Amesema, Jeshi la Polisi kikosi cha usalama  barabarani kwa kushirikiana na vyombo vingine vikiwemo vyombo vya Habari  vitaendelea kutoa elimu kwa madereva na watumiaji wengine wa barabara juu ya  matumizi sahihi ya alama  za barabarani,kuheshimu na kutii sheria.

Kwa upande wake Mkuu wa kikosi cha usalama barabarani mkoa wa Ruvuma Salum Morimori amesema,madereva wa serikali wanatakiwa kuwa jicho na kioo kwa watu wengine kwa kutii sheria zilizopo badala ya kuwa watu wa ovyo.

Amesema, madereva ni watu  muhimu kwa maisha ya  kila siku ya viongozi wa Serikali,kwa hiyo wana wajibu wa kuhakikisha wanaepusha ajali na madhara mengine  kama vifo kwa viongozi .

Kwa mujibu wa Morimori,madereva wakizingatia sheria hakutakuwa na vifo wala uharibifu wa mali za Serikali na kusistiza kuwa, Jeshi la Polisi litawachukulia hatua kali madereva wazembe bila kujali anaendesha taasisi ipi ya Serikali.

Ametaja makosa yanayofanywa mara kwa mara na madereva wa Serikali ni mwendokasi,kutosimama kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na kutoheshimu alama zilizowekwa, jambo linalochangia kutokea kwa ajali nyingi na kuleta madhara kwa watu wasiokuwa na hatia.

Amesema, kama wataendesha magari kwa kuzingatia  sheria na kuheshimu alama za barabarani,basi watabaki salama wao na viongozi wanaowaendesha na kulinda magari ya Serikali yanayonunuliwa kwa fedha nyingi.

“madereva wa Serikali mmekuwa mfano mbaya sana kwa madereva wengine na jamii inayowazunguka,hamtaki kutii sheria wala kuheshimu alama za barabarani,sasa leo nawaambia hakuna mtu aliye juu ya sheria,sisi kama Jeshi  tutawachukulia hatua hata kama  uko na kiongozi kwenye gari”amesema Morimori.

Akiongea kwa niaba ya wenzake,Geofrey Cloudius kutoka ofisi ya Katibu Tawala mkoa wa Ruvuma amesema, mafunzo hayo ni muhimu sana kwani yamewakumbusha mambo mengi ya kuzingatia wawapo barabarani.

Amesema, ni kweli madereva wa Serikali ndiyo vinara wa kuvunja sheria za usalama barabarani, na amewataka madereva wenzake kubadilika na kutii sheria na kuzingatia alama zilizowekwa ili kuokoa maisha yao,viongozi wanaowabeba pamoja na kulinda magari ya umma.

Cloudius, amelishukuru Jeshi la Polisi kutoa mafunzo hayo kwani yatawasaidia madereva wengi wa Serikali sio kuzingatia sheria tu,lakini hata kuepusha vifo kwa watu wasiokuwa na hatia.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad