Na Said Mwishehe, Michuzi TV
UBALOZI wa Serikali ya Ufaransa nchini Tanzania umetoa Sh.bilioni 1.7 kwa ajili ya kusaidia vikundi vya wanawake, wasichana na vjana kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha hasa katika sekta ya kilimo.
Kwa mujibu wa ubalozi huo wa Ufaransa fedha hizo ambazo zimetolewa na Serikali yao zitakwenda kusaidia makundi hayo kupitia mashirika manne ambayo yamekuwa yakijihusisha na shughuli mbalimbali za kilimo endelevu pamoja na kusaidia wanawake.
Akizungumza leo Aprili 19,2021 jijini Dar es Salaam, Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Fr'de'ric Clavier amesema wametoa fedha hizo ili kusaidia wanawake na wasichana kwa ajili ya kutekeleza mradi wa 'Empowerment through Agroecology na permaculture Gape' na kwamba Ufaransa itaendelea kusaidia eneo la usawa wa kijinsia na mabadiliko ya tabianchi na kukabiliana nayo.
Amesema katika kusaidia eneo hilo Serikali ya Ufaransa nchini Tanzania imeamua kuleta mradi huo ambao ni wa miaka miwili unaojulikana kama GAPE wenye thamani ya Sh.1,669,561,299."Lego kubwa ni kuwahamasisha wasichana 2000 ambao ni sawa na asilimia 90 na wavulana asilimia 10 katika kilimo cha mboga mboga."
Ameongeza fedha hizo zitakwenda kusaidia katika Mkoa ya Tabora katika Wilaya ya Nzega ,Mkoa wa Dodoma katika Wilaya Kongwa na Zanzibar na mradi huo ni muendelezo wa mradi wa kwanza uliokuwa umepewa jina la Agroecology .
Amesisitiza utunzaji huo na usaidizi kwa wakulima wadogo kwa ajili ya kilimo hai na kwamba Serikali ya Ufaransa itaendelea kusaidia Serikali ya Tanzania katika mapinduzi ya kilimo cha kisasa ili kuwa na kilimo endelevu kitakachofikia malengo.
Balozi Clavier amesema asilimia 80 ya wakulima wadogo ni wanawake ambao wanapitia wakati mgumu na mazingira magumu ya kupata ardhi kwa ajili ya kilimo na hata wakiuza mazao yao hawapati kinachostahili.
Hivyo katika kuondoa changamoto hizo, Ubalozi wa Ufaransa unasaidia mashirika manne ya FCS Trust, Msichana Initiative, PPIZ na SAT ambayo yote yanafanya kazi kwa ajili ya kuwasaidia wanawake na wasichana na hasa katika kilimo endelevu kwa lengo la kuongeza uzalishaji, wngi na ubora."Programu hii ina malengo ya kuhakikisha kunakuwa a uhakika wa upatikanaji wa chakula."
Kwa upande wa wawakilishi wa mashirika hayo wametoa shukrani kwa Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania kw uamuzi wake wa kutoa fedha hizo kwa ajili ya kusaidia makundi hayo ili yaweze kuondokana na changamoto za kimaisha.
Wamesema kupitia mradi huo wa GAPE uliojikita kusaidia wasichana na vijana utakwenda kuwanufaisha walengwa moja kwa moja.
Aidha Mkurugenzi wa Shirika la Msichana Initiative Rebbeca Gyumi amesema mradi huo utakwenda kuwanufaisha wanawake, vijana na wasichana wapatao 2000 katika mikoa ya Dodoma, Tabora na Zanzibar na wao wamepewa dhamana hiyo ya kuhakikisha mradi unatekelezwa kikamilifu.





No comments:
Post a Comment