TANZANIA imekuwa ni nchi ya mfano kusini mwa jangwa la Sahara kwa kufanya vizuri katika usajili wa matukio muhimu ya binadamu na takwimu ambayo ni vizazi, vifo, ndoa na talaka.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju ametoa pongezi hizo kwa niaba ya Serikali kwa Wafanyakazi wa Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) kwa juhudi na uwajibikaji uliopelekea kuifikisha nchi kuwa sehemu ya kujifunza kwa nchi nyingine za Afrika.
Pongezi hizo zimetolewa hii leo wakati akifungua kikao cha 23 cha Baraza la Wafanyakazi kinachofanyika Jijini Arusha.
Tayari Nchi ya Ethiopia wameanza kutekeleza mkakati wa usajili wa matukio muhimu na Takwimu baada ya kujifunza kutoka Tanzania, ni ukweli usiyopingika kwa sasa nchi yetu tunajivunia kwa sifa hiyo." Alisema Bw. Mpanju.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Kaimu Kabidhi Wasii Mkuu na Mtendaji Mkuu wa RITA Bi. Emmy Hudson amesema kuwa kuhudi zinazofanywa na Serikali kwa kuboresha Mifumo ya Usajili pamoja na marekebisho ya Sheria kwa pamoja vimeonesha matokeo chanya licha ya kukabiliwa changamoto ya janga la dunia la ugonjwa wa corona linalosababishwa na virusi vya Covid 19.
"Kwa upande wetu tulifanikiwa kuwapokea jirani zetu kutoka Nchi ya Uganda waliyokuja kujifunza kwetu kuhusu masuala ya usajili wa vizazi, vifo, ndoa na talaka, kwa kweli kama nchi tulijipanga vizuri na mapema kwa kufuata maelekezo ya wataalam wetu wa afya na hivyo tukaendelea kutoa huduma kabla na hata wakati wa janga hilo, hivyo tuna kila sababu ya kujivunia kwa kuitangaza Tanzania Kimataifa."Alisema Bi. Hudson.
No comments:
Post a Comment