HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 20, 2021

HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA YAZINDUA IDARA YA MAGONJWA YA SARATANI, WAZIRI GWAJIMA AWAPONGEZA

 


Charles James, Michuzi TV

SERIKALI imepongeza juhudi kubwa zinazofanywa na Taasisi ya Hospitali ya Benjamin Mkapa iliyopo jijini Dodoma katika kuwahudumia na kuboresha afya za watanzania hasa waishia mkoani Dodoma na Kanda ya Kati kwa ujumla.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima wakati akizindua Idara ya Magonjwa ya Saratani, Huduma za Patholojia na Mkataba wa Huduma kwa Watena leo jijini Dodoma.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Dk Gwajima ameipongeza Hospitali ya Benjamin kwa namna ambavyo imekua mstari wa mbele katika kuwahudumia watanzania pamoja na kuzindua mkataba wa huduma kwa wateja huku akizitaka Hospitali zingine, Vituo vya Afya kuiga mfumo huo ambao utawezesha kupata maoni yatakayoweza kuwasaidia kutoka kwa wananchi.

Dk Gwajima amesema kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia tafiti za Saratani (IARC) zinaonesha kuwa Tanzania kuna ongezeko la wagonjwa wapya wa saratani wapatao 5,000 na inakadiriwa ifikapo 2030 kutakua na ongezeko la wagonjwa kwa asilimia 50 hivyo kitendo cha kuzinduliwa kwa Idara hiyo ya Saratani katika Hospitali ya Benjamin ni muendelezo wa Serikali katika kupambana na ugonjwa huo hatari duniani.

Waziri Gwajima amewataka watoa huduma wote wa afya nchini kutenga muda wao katika kutoa elimu ya ugonjwa wa saratani ili kuwawezesha wananchi kuwa na uelewa mpana wa ugonjwa huo na siyo kusubiri hadi hali kuwa mbaya.

" Magonjwa ya Saratani yanatibika iwapo mgonjwa atawahi katika vituo vya afya vinavyotoa huduma hizo, zaidi ya asilimia 75 ya wagonjwa hufika katika vituo vya afya wakiwa tayari wameshachelewa sana na kuwawia vigumu madaktari kutibu na kuponya ugonjwa huo.

Uzinduzi wa Idara hii hapa Benjamin na kwenye Hospitali zingine hautokua na maana kama hatutokua tukitoa elimu ili kuwafanya wananchi kuwa kwa wataalamu kabla ya kuchelewa lakini pia nitoe rai kwa watanzania wenzangu kuwa na utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara," Amesema Waziri Gwajima.

Kwa upande mwingine Waziri Dk Gwajima amesema kuwepo kwa kitengo cha Patholojia katika Hospitali ya Benjamin ni faraja pia katika kuharakisha matibabu kwani hapo awali ilibidi sampuli zipelekwe Dar es Salaam ili kubaini kama ni Saratani.

Akizungumzia uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin, Dk. Alphonce Chandika amesema umri unaoathirika zaidi na Magonjwa ya Saratani ni kati ya miaka 50 hadi 69 kwa wanawake hasa Saratani ya Mlango wa Kizazi na kwa upande wa wanaume wanaoathirika ni kuanzia miaka 70 hasa kwa Saratani ya Tezi Dume.

Dk Chindika ameishukuru Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk John Magufuli kwa uwekezaji mkubwa wa vifaa vya kisasa na upatikanaji wa wataalamu wabobezi ambao kwa kiasi kikubwa wamewezesha huduma za kibingwa kupatikana katika eneo la Kanda ya Kati.

Dk Chindika amesema tafiti zinaonesha zaidi ya asilimia 66 ya Saratani zinazuilika endapo wananchi wangeepuka viashiria hatarishi kama uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe kupita kiasi, kuepuka unene, kuepuka matumizi ya vyakula vya mafuta, kuepuka mionzi ya jua hasa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi pamoja na kupima afya mara kwa mara.

" Septemba 2019 Hospitali ya Benjamin ilianzisha Idara ya Magonjwa ya Saratani baada ya kununua mashine ya kisasa inayowezesha kuchanganya dawa za saratani (Chemotherapy Compounding Hood) ambapo dawa za kuanzia tulizipata Hospitali ya Ocean Road na baada ya hapo tuliendelea kupata kutoka MSD.

Katika kipindi cha Januari na Desemba 2020 Idara ta Saratani tumehudumia wagonjwa 814 wagonjwa wapya wakiwa 531 na wagonjwa marudio ni 283 ambapo wagonjwa 192 wametibiwa hapa kwa dawa na wagonjwa 339 wamepelekwa Ocean Road kwani walihitaji kupata matibabu ya mionzi ambayo kwa sasa hatuna," Amesema Dk Chandika.

Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima akizindua Idara ya Saratani katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma leo.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima akizungumza wakati wa uzinduzi wa Idara ya Saratani katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dk Alphonce Chandika akizungumza wakati wa uzinduzi wa Idara ya Saratani katika Hospitali hiyo leo jijini Dodoma.
Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Josephat Maganga akizungumza katika uzinduzi wa Idara ya Saratani katika Hospitali ya Benjamin Mkapa leo jijini Dodoma.
Wadau wa afya na watumishi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma wakifuatilia uzinduzi wa Idara ya Saratani katika Hospitali hiyo leo.
 






No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad