HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 1, 2019

NAMPATIA MKANDARASI MILION 279 ILI AMALIZE MRADI WA MAJI JIBONDO -NAIBU WAZIRI AWESO

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii

Wananchi wa Kijiji cha Jibondo Wilaya ya Mafia wamehakikishiwa kupata maji safi na salama ndani ya muda mfupi baada ya kukamilika kwa ulazaji wa mabomba chini ya bahari yatakayopeleka maji kwenye Kijiji hicho wenye thamani ya Bilion 1.9

Mradi huo wa maji unaopeleka maji Jibondo uliibuliwa na wananchi mwaka 2004 na kuwekwa katika mpango wa vijiji 10 chini ya Programu ya maendeleo ya sekta ya maji.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Jibondo, Aweso amesema mradi huu umetakiwa umalizike mwishoni mwa mwaka huu ila mkandarasi ameshindwa kuendelea na kazi kutokana na madai ya malipo.

Aweso amesema, mkandarasi ameleta maombi ya milion 279 ambaoo ameahidi atakapokabidhiwa fedha hizo atafikisha maji katika Kijiji cha Jibondo.

"Ni mara tatu nafika Mafia ila mara ya pili nafika hapa Kijiji cha Jibondo na nilipokuja mara ya kwanza niliwaahidi mtapata maji na mradi ndio huo ambapo umebakia hatua ndogo ya kulaza mabomba,"amesema Aweso.

" Mkandarasi amesema, akipewa Milion 279 anamaliza mradi huu na wananchi wanaanza kupata maji safi na salama, na mimi namwambia nampatia hiyo hela kesho atapatiwa Milion 100 (mia moja) na Jumatatu aje na Mkurugenzi wake tujue tunafanyaje kumpatia fedha zingine zilizobaki,"

Aweso ameeleza kuwa, lengo la awamu ya tano inayoongozwa na serikali ya Mapinduzi chini ya  Rais Dkt John Pombe Magufuli ni kumtua mama ndoo kichwani, na hilo litakamilika hivi karibuni baada ya mradi wa maji kufika katika Kijiji cha Jibondo.

Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Maji Vijijini RUWASA Mhandisi Ndolimana Kijiga amesema mradi huu umejengwa na mkandarasi Elegence Developers chini ya usimamizi wa ofisi yao pia mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya.

Amesema, kumekuwa na changamoto za utekelezaji wa mradi huu ambapo ni pamoja na fedha kutokupatikana kwa wakati.

"Mradi huo umetekelezwa kwa awamu tatu, awamu ya kwanza ilifanyika kati ya mwaka 2015 na 2016 na kazi iliyofanyika ni kufanya utafiti wa maji ardhinina kuchimba kisima kina cha mita 40 kwenda chini ambacho uwezo wake ni kutoa maji lita 10,000 kwa saa na pili ni kufanya usanifu wa mradi na nwisho ni ujenzi wa mradi wenyewe ulioanza kutekelezwa machi 16 2018," amesema Kijiga.

Amesema, lengo la mradi huo ni kuhakikisha wananchi wa Kijiji cha Jibondo zaidi ya 1809 wanapata majj safi na salama yenye kutosheleza na kuzuia magonjwa yanayisababishwa na ukosefu wa maji safi na salama ikiwemo na kuwapunguzia adha ya kufuata maji zaidi ya mita 400 na gharama kubwa.

"Tayari tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 75,000 kwa siku lipo katika hatua za mwisho (asilimia 90), tumeshajenga Vizimba vya kuchotea maji zaidi kilichobaki ni ulazaji wa mabomba tu,

Wananchi wa Kijiji cha Jibondo wameonesha furaha kubwa baada ya Kuhakikishiwa kupata maji safi na salama wakiwa na  adha ya muda mrefu na kuishia kununua maji kwa bei kubwa kutoka Kisiwa Kikubwa.

Naibu Waziri Aweso ameendelea na ziara yake ya kutembelea miradi mbalimbali ya maji Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na wananchi wanapata maji safi na salama.

Aweso aliongozana na wataalamu mbalimbali wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam DAWASA.
  Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akizungumza na wanakijiji wa Jibondo katika mkutano na kuwaahidi kufanikisha kukamilika kwa mradi wa maji kwa kumlipa mkandarasi kiasi cha Shiling Milion 279 ili akamilishe mradi huo uliofikia hatua ya ulazaji wa mabomba chini ya bahari.
 
 Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akipokea taarifa ya mradi wa Maji kutoka kwa Kaimu Meneja Mamlaka ya Maji Vijijini RUWASA  Wilaya ya Mafia, mradi huo unathamani Bilion 1.9 utakaoondoa kero ya maji kwa wakazi 1,809.
 Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akikagua moja ya kizimba kitakachotumika kuchotea maji kwa wananchi wa Jibondo pindi utakapokamilika. 
 Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akizungumza na moja ya watendaji wa Wizara ya maji kwa njia ya simu akitoa maombi ya kupatiwa kiasi cha Shiling Milion 279 ili mkandarasi wa mradi wa maji wa Jibondo apatiwe na kukamilisha kwa haraka zaidi wananchi waanze kupata maji safi na salama
 Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akizungumza na wahandisi, watendaji wengine baada ya kuwasili kwenye Kijiji cha Jibondo alipotembelea kukagua mradi wa maji ulipofikia
 Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akiwa katika ziara ya kukagua mradi wa maji wa Jibondo akiongozana na watalaamu mbalimbali.
 
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akikagua tanki la maji lenye uwezo wa kuhifadhi maji Lita 75,000 kwa siku alipotembelea mradi wa maji  wa Kijiji cha Jibondo wenye thamani ya Bilion 1.9 unaotarajia kumaliza hivi karibuni.
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akisalimiana na wanakijiji wa Jibondo baada ya kutembelea kijiji hicho na kukagua mradi wa maji.
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akimpa zawadi moja ya wakina mama wa Kijiji cha Jibondo baada ya kuwatembelea na kuangalia mradi wa maji ulipofikia.
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akiwa katika picha ya pamoja na Wanakijiji wa Jibondo wakifurahia ujio wake.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad