HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 19, 2019

WAZIRI MKUU AFUNGA SOKO LA NDUTA

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amefunga soko la wakimbizi na wananchi lililoanzishwa nje ya kambi ya Nduta iliyopo wilayani Kibondo mkoani Kigoma. Hatua hiyo imekuja baada ya soko hilo kubainika kuwa  chanzo cha  wakimbizi kutoka nje ya kambi kiholela na kushiriki katika kufanya matukio ya kiharifu.

Waziri Mkuu ametangaza uamuzi huo leo (Jumanne, Februari 19, 2019) wakati akizungumza na watumishi wa umma katika ya Halmashauri ya Kibondo. ”Vitendo vya uhalifu wilayani Kibondo vikiwemo vya utekaji wa watoto vimeongezeka na kusababisha hofu na taharuki miongoni mwa wananchi.”

Waziri Mkuu amesema ni vema halmashauri hiyo ikaandaa utaratibu wa kutoa vibali vitakavyowaruhusu Watanzania kupeleka bidhaa ndani ya kambi hivyo. Kadhalika, Waziri Mkuu amewataka wananchi waliopewa dhamana ya kufanya kazi kwenye kambi za wakimbizi wawe waadilifu na wasimamie sheria.

“Nafahamu tunao watendaji wetu ambao wapo kambini kusimamia shughuli mbalimbali za wakimbizi,  tekelezeni wajibu wenu ipasavyo na si vinginevyo.” Baada ya kuzungumza na watumishi wa umma wa Halmashauri ya Kibondo, Waziri Mkuu alikwenda wilayani Kakonko na kukagua mradi wa maji Muhange. Pia Waziri Mkuu ameweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa makao makuu ya Halmashauri ya wilaya ya Kakonko unaotarajiwa kugharimu sh. bilioni 4.5. 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia wananchi wakati alipowasili kwenye eneo la Mradi wa Maji wa  Muhange wilayani Kakonko kukagua mradi huo, Februari 19, 2019. Kulia ni mkewe Mary na kushoto ni Mbunge wa Buyungu, Mhandishi Christopher Chiza. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Mke wa Waziri Mkuu, Mama Mary Majaliwa akiwasalimia wananchi wa kijiji cha  Muhange wilayani Kakonko wakati Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipokagua Mradi wa Maji kijijini hapo, Februari 19, 2019. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim  Majaliwa akizungumza na wananchi baada ya kakagua Mradi wa Maji wa Muhange wilayani Kakonko, Februari 19, 2019.  Wengine kutoka kushoto ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamadi Masauni, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Brigedia Jenerali Mstaafu, Emmanuel Maganga, Mbunge wa Buyungu Mhandisi Christopher Chiza, Mke wa Waziri Mkuu, Mama Mary Majaliwa, Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Profesa Joyce Ndalichako na kulia ni Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhandisi Stella Manyanya. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi Diwani wa Kata ya Muhange wilayani Kakonko, Ibrahim Katunzi jumla ya shilingi milioni moja kwa ajili ya Mradi wa Maji na Zahanati katika Kata hiyo, Februari  19, 2019. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad