HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, January 28, 2019

Naibu Waziri Shonza Awapongeza Waandaaji wa Mbio za Riadha Mirerani

Na Lorietha Laurence-WHUSM,Mirerani.
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni,  Sanaa na Michezo  Mhe. Juliana Shonza   amewapongeza waandaji na waratibu wa mbio za riadha Mirerani (Mirerani Marathon) na kuahidi kuwa serikali itashirikiana nao kwa ukaribu kuhakikisha malengo yaliyokusudiwa katika kuendeleza mchezo huo yanafanikiwa.
Hayo ameyasema jana Mji Mdogo wa Mirerani, wakati wa ufunguzi wa mbio fupi zilizoandaliwa na Mratibu Charles Mnyalu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo benki ya CRDB na Shirika la Bima la Zanzibar.
Mhe. Juliana Shonza ameeleza kuwa kupitia mbio hizo  za riadha kwa kiasi kikubwa zitasaidia  katika kutangaza fursa zinazopatikana Mirerani yakiwemo madini ya Tanzanite.
“Kupitia mashindano haya ya riadha yatasaidia katika kuutangaza mji huu wa Mirerani ambao ni mji pekee duniani ambapo madini ya Tanzanite yanapatikana, na hivyo kufungua fursa ya utalii wa madini nchini” amesema Mhe. Juliana Shonza.
Aidha aliwasihi  Maafisa Michezo kutokaa ofisini na badala yake kutoka nje na kushirikiana na wadau katika kusaka na kuendeleza vipaji mashuleni  ili kuwa na wachezaji wazuri watakaowakilisha nchi katika mashindano mbalimbali.
Vilevile Mhe. Shonza aliongeza kwa kueleza kuwa sera ya michezo inaeleza kuwa michezo ni suala jumuishi hivyo ni jukumu la wadau kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kuwa inakuzwa na kuendelezwa.
Naye Mratibu wa mbio hizo Bw. Charles Mnyalu amesema kuwa lengo la mbio hizo ni kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. John magufuli za kulinda rasilimali madini ya Tanzanite ikiwemo kuzungushia ukuta machimbo ya mirerani yaliyopo Wilayani Simanjiro.
Mashindano ya riadha Mirerani (Mirerani Marathon) yalihusisha mbio za kilomita 3, 5 na 21, ambapo washindi katika kilomita 21 walikuwa ni Bw. Faraji Damasi kwa upande wa wanaume huku wanawake waliongozwa na Failuna Matanga.
 Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza (Katikati) akiponyeza kitufe kuashiria kuanza kwa mashindano ya riadha yaliyofanyika jana Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
 Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza (katikati) akimaliza mbio fupi za kilomita 5 wakati wa ufunguzi wa ponyeza wa mashindano ya riadha yaliyofanyika jana Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
 Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza akiongea na washiriki wa mbio fupi za riadha zilizofanyika jana Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
 Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza(kulia) akimpa mkono wa pongezi mshindi wa riadha za kilomita 21 kwa upande wa wanawake Bi. Failuna Matanga katika mashindano ya riadha yaliyofanyika jana Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza(kulia) akimpa mkono wa pongezi mshindi wa riadha za kilomita 21 kwa upande wa wanaume Bw. Faraji Damas katika mashindano ya riadha yaliyofanyika jana Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.(Picha na Lorietha Laurence-WHUSM,Mirerani).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad