AFISA Tarafa wa Itiso Remidius Emmanuel ametangaza vita kwa watu wote waliovamia maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya Malisho katika Tarafa hiyo iliyopo wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma.
Remidius amesema hayo mapema wiki hii katika mkutano maalumu wa kujibu kero mbalimbali katika kijiji cha Gwandi na kuhusisha Wafugaji kutoka kata ya Zajilwa.
Akisoma taarifa mbele ya Afisa Tarafa, Katibu wa Chama Cha Wafugaji Wilaya ya Chamwino Bw. Reginaldo Lubeleje alitaja baadhi ya Changamoto wanazokumbana nazo ikiwa ni pamoja na ukosefu wa malisho,njia za mifugo, upungufu wa Majosho ya Mifugo, Mahusiano madogo kwa baadhi ya Viongozi wachache wa Serikali na Chama cha Wafugaji.
Imeelezwa kuwa baadhi ya maeneo katika Tarafa ya Itiso yalitengwa kabisa kwa ajili ya Wafugaji lakini yamevamiwa na Wakulima wakubwa na baadhi ya maeneo hayo ni pamoja na Mbuga ya Yobo, Uliuli,Dongo, Jelesa, Mazuguni na Haneti hizi mbuga zilitengwa kwa ajili ya malisho ila maeneo hayo yamevamiwa na wakulima wakubwa.
Akieleza mafanikio yao katibu wa chama cha wafugaji Iti amesema kuwa; chama hicho kimefanikiwa kuwaunganisha Wafugaji wote bila kujali Ukabila, dini na Itikadi ya mtu, mbali na kuweza kutatua baadhi ya matatizo yao wenyewe wamefanikiwa pia kushiriki katika vikao mbalimbali vilivyo husisha Makundi ya Wafugaji aidha wamempongeza Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Vumilia Nyamoga kwa kuendelea kuwashirikisha katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya Wilaya ya Chamwino.
Akijibu kero hizo Afisa Tarafa Remidius Emmanuel amesema kuwa, uwezekano wa kuibuka kwa migogoro ya Wakulima na Wafugaji wakati mwingine hutokana na uzembe wa baadhi ya viongozi wanaoshindwa kutimiza wajibu wao.
Amesema kuwa; "Sasa unakuta kiongozi anafahamu kabisa kwamba haya maeneo yametengwa kwa ajili ya malisho ya mifugo, alafu anaona yanavamiwa alafu yeye amenyamaza tuu, na ninazo taarifa kuna baadhi ya viongozi wa Serikali za Vijiji ambao wameshiriki kuuza maeneo hayo, Wajiandae kuyarejesha kabisa na zoezi hili litafanyika Tarafa nzima.Kwa hiyo kama kuna watu wamejimilikisha maeneo hayo wambieni wayarejeshe haraka.Watatueleza nani aliwauzia na ni kwa utaratibu upi? na katika hili sitorudi nyuma, ni jukumu letu viongozi kutatua migogoro na sio kuwa sehemu ya Migogoro" Amesem Remidius.
Hata hivyo amewaeleza kuwa licha ya juhudi za Serikali katika kutatua kero ya Majosho ya mifugo lakini amewataka Wafugaji kupokea ushauri kutoka kwa wataalamu wa Mifugo ili kuepuka Magonjwa mbalimbali yanayoweza kuipata mifugo yao.
Aidha amesema kuwa, "Ni kweli ipo Changamoto ya Majosho kwa ajili ya Mifugo yetu, lakini baadhi ya Serikali za Vijiji na Kata wamefanikiwa kutatua kero hii kwa kuwatumia Mawakala na Makundi ya wafugaji lakini nasisitiza ili kufanikisha taratibu hizo nimewaelekeza kushirikisha Wataalamu wetu wa Halmashauri, lakini ninazo taarifa pia baadhi yetu sisi Wafugaji bado hatuna muamko wa kupeleka Mifugo yetu katika Majosho yaliyopo, niombe uongozi wa Chama cha Wafugaji kuhimiza umuhimu wa kutekeleza ushauri wa Kitaalamu ili Mifugo yetu isishambuliwe na magonjwa" Amesema Remidius.
Na amesema kuwa suala la mahusiano ni muhimu kwa makundi yote katika Tarafa hiyo na,ataendelea kuwahimiza viongozi kuimarisha mahusiano na makundi yote ikiwemo Wafugaji, na amewashukuru wananchi kwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za Maendeleo.
"Juzi nimeshuhudia Wafugaji wa Kijiji cha Nayu kata ya Dabalo kwa hiari yao mwenyewe wameamua kuchangia ujenzi wa ofisi ya Serikali ya Kijiji hicho nimefurahi sana" Ameongeza
Hata hivyo Afisa Tarafa ameziagiza Serikali za vijiji vyote katika Tarafa ya Itiso kupitia kamati husika kusimamia suala la njia za Mifugo, huku akisisitiza kwamba kukosekana kwa njia hizo kumechangia pia uharibifu wa miundombinu ya barabara.
Na amehitimisha kwa kusema kuwa wafugaji na Wakulima wote wanategemeana na yeye kama kiongozi wa Tarafa hiyo ataendelea kusimamia mipango mizuri inayotoa haki kwa makundi yote kuishi bila migogoro na kuwataka wafugaji pia kutoa ushirikiano katika jamii kwa kuheshimu sheria na taratibu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuepuka migongano kwa kuingiza mifugo katika mashamba halali ya Wakulima hatua ambayo imekuwa ikijitokeza kwa baadhi ya maeneo.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Chama cha wafugaji kanda ya kati Neema Ally amempongeza Afisa Tarafa kwa kuonyesha dhamira ya kutatua Changamoto zinazowakabili wafugaji hao na kuhimiza umuhimu wa serikali za vijiji kuendelea na utaratibu wa mipango itakayo ainisha maeneo ya malisho na huduma nyingine za mifugo ili kuondokana na migogoro inayoweza kujitokeza baina ya Wafugaji na wakulima.
Afisa Tarafa wa Itiso Remidius Emmanuel akizungumza na Wafugaji katika mkutano maalumu wa kujibu kero mbalimbali kijiji cha Gwandi na kuhusisha Wafugaji kutoka kata ya Zajilwa.
Mwenyekiti wa Chama Cha Wafugaji kanda ya kati, Neema Ally akizungumza na wafugaji wakati wa mkutano huo uliofanuka katika kijiji cha Gwandi kata ya Zajilwa.
Baadhi ya wafugaji wakiwasilisha kero zao mbele ya Afisa Tarafa
No comments:
Post a Comment