HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 7, 2018

UWT YAWAGEUKIA WADAIWA SUGU BENKI YA WANAWAKE

*Yataka waliokopa warejeshe mkopo haraka, wakishindwa wachukuliwe hatua

Na Said Mwishehe, Globu ya Jamii
MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT)kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM), Gaudentia Kabaka  amewataka wateja wanaodaiwa na Benki ya Wanawake Tanzania(TWB), kuhakikisha wanalipa marejesho yao ya mikopo mara moja na ikiwezekana ndani ya siku saba.

Akizungumza leo katika Makao makuu ya UWT  Dar es Salaam, Kabaka amesema UWT inaungana na taarifa ya Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya wanawake  Tanzania (TWB) Beng'i Iasa ya  kutaka wadaiwa sugu wa benki hiyo walipe marejesho ya mikopo ndani ya siku saba.

"Sisi umoja wa Wanawake Tanzania, na wanawake wote kwa ujumla nchini hatutakubali na hatuko tayari kabisa kuona watu wachache wakiwemo hata wanawake wenzetu wakitumia benki hii kwa kujinufaisha wao wenyewe.Waliochukua mkopo wahakikishe wanalipa ili wengine nao wakope,". alisema.

Ameongeza UWT wanapenda kuona mikopo hiyo inarejeshwa kwa wakati na kufafanua TWB ndiyo benki pekee inayoweza kumkopesha mama mjasiriamali mdogo.Pia ni miongoni mwa benki tatu tu zilizopo duniani ambazo ni maalum kwa ajili ya wanawake.Mbali ya hii ya hapa kwetu ya TWB, moja ipo Pakistan na nyingine India.

"UWT tunatoa rai kwa wakopaji wote na tunatoa tamko, hao ambao wamekopeshwa na hawajarudisha mikopo kwa wakati wachukuliwe hatua za haraka na stahiki ikiwemo kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria mapema iwezekanavyo ili kuhakikisha wanalipa mikopo yao yote kwa manufaa na uhai wa benki yetu na kwa manufaa ya wanawake wote nchini.

"Wadaiwa sugu ni 7065 ambao ni wengi sana hasa kutokana na fedha wanayoihodhi ambazo ni kiasi cha Sh. bilioni 6.79. Tungependa kuona mikopo hii inarejeshwa kwa wakati.Tunaendelea kufuatilia na tunatamani tungepata hiyo orodha ya hao wadaiwa sugu," amesema Kabaka.

Ameongeza kuwepo kwa benki hiyo ni maombi na kilio cha muda mrefu cha wanawake nchini tangu uhuru kupitia Jumuiya ya CCM kuzaliwa. Ni kilio cha Kina bibi Titi Mohammed na mama Sophia Kawawa wakati wa uhai wao wakiwa wenyeviti wa UWT kwa nyakati  tofauti na kilio cha wenyeviti wengine waliofuata hadi sasa.

"Napenda kuwaambia jambo hili  kama Mwenyekiti wa UWT nalifuatilia kwa karibu sana kwa kuwa ni miongoni mwa maagizo yaliyotolewa na Mwenyekiti wetu, Rais Dk.John Magufuli wakati wa Mkutano wetu Mkuu uliofanyika Desemba 8, 2017 mjini Dodoma", amesema.

Amesema uongozi mpya wa UWT umekaa na benki ya wanawake kuangalia namna gani benki itawafikia wanawake wengi na kwa riba nafuu zaidi. 
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania(UWT) kupitia CCM, Gaudentia Kabaka (katikati) akizungumza leo jijini Dar es Salaam kuhusu kuunga mkono taarifa ya Benki ya Wanawake Tanzania(TWB) inayotaka wadaiwa sugu wa benki hiyo kulipa mkopo ndani ya siku saba.Wakwanza kushoto ni Katibu Mkuu UWT, Amina Makilagi na kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo, Bara Eva Kiwhele. (Picha na Said Mwishehe)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad