HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 7, 2018

RAIA WA ZAMBIA, WENZAKE KORTINI KWA KWA TUHUMA ZA UTAKATISHAJI FEDHA

 Na Karama Kenyunko, Blogu ya Jamii

RAIA wa Zambia na wenzake sita wamepandishwa katika kizimba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na tuhuma za kula njama, wizi na utakatishaji wa fedha.

Hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo leo na Wakili wa Serikali, Mwanaamina Kombakono akisaidiana na Wakili wa Serikali mwandamizi Mutalemwa Kishenyi imewataja watuhumiwa hao ni Kirby Ng'andu, Meneja uendeshaji wa kampuni ya Zambia Cargo and Logistic, Robert Christopher na Wakala wa usafirishaji, Isihaka Ngubi, Cathbert Mlugu mlinzi, Mrisho Mindu, Karani Giften John na Maulid Said.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi imedaiwa, kati ya Januari 26 na Februari 2 mwaka huu, huko katika kampuni ya Zambia Cargo and Logistics iliyopo Dar es Salaam,washtakiwa wote kwa pamoja walikula njama ya kutenda kosa la wizi.

Imeendelea kudaiwa, siku na mahali hapo, washtakiwa hao  waliiba katoni 700 za korosho zilizobanguliwa  zenye thamani ya USD 54180 ambazo ni sawa na Sh.120,563,909,53, mali ya Barabara Trading Tanzania Ltd.

Wakili Mwanaamina amedai  kuwa, siku na mahali hapo, watuhumiwa hao wote pia walijihusisha na muamala unaohusiana na katoni hizo 700 za korosho zenye thamani hiyo ya fedha huku wakijua kuwa, mali hiyo ni zao lililotokana na kosa la wizi.

Hata hivyo, washtakiwa wote wamekana kutenda makosa hayo na wamerudishwa rumande kwa kuwa shtaka la utakatishaji wa fedha halina dhamana, wakili Kishenyi amedai kuwa, upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho kutwa, Machi 9 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad