HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, December 1, 2017

WIZARA YA AFYA YATOLEA UFAFANUZI KUHUSIANA NA UZINDUZI WA MKAKATI WA KONDOM

Kumekuwa na taarifa mbalimbali, hamaki na kejeli zinazoenea katika mitandao ya kijamii kuhusiana na taarifa iliyotolewa tarehe 27 Novemba 2017, Mnazi Mmoja kwenye uzinduzi wa Mkakati wa Taifa wa Kondom kuhusu mpango wa Serikali kununua na kusambaza kondom 500,000,000 katika kipindi cha miaka mitatu 2018 hadi 2020.

Tunapenda kuukumbusha umma wa Watanzania kwamba maambukizi ya VVU na UKIMWI bado ni tatizo katika nchi yetu. Takriban watu 1,400,000 wanakadiriwa kuwa na VVU. Hivyo katika mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI Serikali inaendeleza afua mbalimbali ili kuzuia maambukizi mapya. 

Asilimia 40% ya maambukizi mapya yanatokea miongoni mwa vijana wenye umiri wa miaka 15-24. Aidha makundi maalum kama vile wanaojidunga madawa ya kulevya, wanaofanya biashara ya ngono na wale wanaoamiiana wa jinsia moja wako katika hatari kubwa ya kupata maambukizi.  Makundi mengine ya walio katika hatari ni waendesha magari ya masafa marefu, wavuvi na wananchi wa kwenye migodi.

Wizara inatekeleza afua mbalimbali ikiwa ni pamoja na ushauri nasaha na kupima uwepo wa VVU, na kisha kuanza tiba na matunzo, pamoja na kutoa dawa za kufubaza kwa watakao kuwa na maambuzi ya VVU. Kuna afua pia za kuzuia maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto, kutoa elimu ya VVU/UKIMWI na afya uzazi kwa vijana, elimu kuhusu VVU/UKIMWI kwa jamii na tohara kwa wanaume. 

Matumizi ya kondom ni moja wapo ya afua katika kuzuia maambukizi mapya. Hata hivyo utafiti wa viashiria vya Malaria na UKIMWI wa mwaka 2011/12 umebaini kuwa kuna matumizi duni ya kondom, kwani ni asilimia 27 tu ya watu wenye wenza zaidi ya mmoja waliokiri kutumia kondom mara ya mwisho walipofanya ngono. Hivyo Serikali itaendelea kununua na kusambaza kondom kwa lengo la kuzuia maambukizi ya VVU, magonjwa ya ngono na mimba zisizo tarajiwa ikiwa ni mojawapo ya afua hizo za kudhibiti maambukizi ya VVU.
Tunasisitiza kuwa Wizara na wadau wake inaendelea kutoa elimu ya kondom sambamba na elimu ya kusubiri kufanya ngono kwa wale ambao hawajaanza na wale ambao wameanza lakini wanapaswa kusubiri (Abstinence) na elimu ya kuwa waaminifu kwa mwenza mmoja aliye mwaminifu na anaejua hali yake ya maambukizi ya VVU (Be faithfull). 

Hivi sasa nchini kuna vyanzo vya upatikanaji wa kondom vya aina tatu. Kwanza ni kondom zinazopatikana kupitia sekta ya umma  ambazo husambazwa na Serikali kwa wananchi bila malipo. Pili, kuna kondom zinazosambazwa na wadau ambazo zinauzwa kwa bei ya chini kwa kuwa wadau wamechangia. Mfano kondom za Salama na Dume, na chanzo cha tatu ni kondom za kibiashara ambazo zinauzwa kwa bei ya kati na ya juu.

Kondom za sekta ya umma husambazwa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya na huduma za mkoba ngazi ya jamii, Kondom za wadau na zile za biashara husambazwa katika maduka ya dawa, maduka ya bidhaa mbambali, baa na nyumba za wageni.

Kwa mwaka 2016/17 Serikali iliboresha kondom zinazopatikana kupitia ya sekta ya umma kwa kuipa kifungashio kipya na jina la ZANA, ambapo kondom 36,916,911 zilisambazwa. Kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2018 hadi 2020 Serikali kwa kushirikiana na Mfuko wa Dunia wa kudhibiti malaria, UKIMWI na Kifua Kikuu inatarajia kununua kondom za kiume takribani 500,000,000. 

Kondom hizi zitasambazwa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya na katika maeneo hatarishi yanayoaminika kuwa na watumiaji wengi. Aidha, kwa vile imebainika kuwa watu ambao hawaumwi hawaendi vituo vya afya kwa  ajili  ya kuchukua kondom tu na hivyo kupelekea kutofikia walengwa, usambazaji na ugawaji huu utalenga maeneo ambayo
Kunamatukio ambayo yanaendana na ngono na yana walengwa wa afua za kondom. Maeneo haya ni kama baa, nyumba za kulala wageni, maeneo yenye mikusanyiko ya magari ya masafa marefu, maeneo ya uvuvi na migodini.

Aidha ikumbukwe kwamba nchi yetu ina sera sheria, mila, desturi na maadili yetu kama watanzania,  Hivyo kondom zote haziruhusiwi kusambazwa bila kufuata miongozo ya Wizara, ili kulinda zisifike kwa wasiolengwa.

Hivyo basi, iwapo tunataka kuzuia na kumaliza maambukizi ya VVU na UKIMWI ifikapo 2030 tunapaswa kama nchi kuwekeza katika kuzuia maambukizi mapya. Matumizi ya kondom, ununuzi wa vifaa tiba, vitendanishi, dawa za ARV na za magonjwa nyemelezi ni afua muhimu. Tunaomba wanahabari na wananchi waunge mkono juhudi hizi kwa kuwa tunahitaji watanzania wenye afya bora na uwezo wa kuzalisha ili kuijenga Tanzania ya Viwanda.

Imetolewa  na:
KATIBU MKUU  - AFYA

30 Novemba, 2017

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad