HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, November 8, 2017

TRA YATOA SEMINA ELEKEZI KWA WAAJIRIRWA WAPYA 400

Naibu Mkurugenzi Rasilimali Watu wa Mamlaka hiyo, Bw. Ulimbakisya Masomelu akiwaeleza Waajiriwa wapya wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) juu ya kuwa waadilifu na kutekeleza majukumu yao kikamilifu wakati wa Semina Elekezi ya Siku Kumi iliyoanza leo 08 Novemba, 2017 katika Chuo cha Kodi (ITA) Kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Waajiriwa wapya 400 walioajiriwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakipokea elimu ya Semina Elekezi toka kwa Maafisa Utumishi wa TRA kuhusu namna ya kutekeleza majukumu yao kwa weledi wakati wa ufunguzi wa Semina hiyo ya Siku Kumi iliyoanza leo katika Chuo cha Kodi (ITA) kilichopo Jijini Dar es Salaam, 08 Novemba, 2017. (PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA,TRA).

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeanza kutoa Semina elekezi ya siku 10 kwa Waajiriwa wapya 400 waliopata fursa ya kupata ajira katika Mamlaka hiyo kwa lengo la kuwajengea uwezo watendaji hao wakati wanapoenda kuanza majukumu ya kukusanya mapato kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Mafunzo hayo yamefunguliwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Chuo cha Kodi cha TRA (ITA), Profesa Isaya Jairo na yanatarajiwa kukamilika baada ya siku kumi na kuwawezesha waajiriwa hao kumudu majukumu ya kukusanya mapato nchini kwa uadilifu.

Akiongea wakati wa Semina hiyo, Naibu Mkurugenzi Rasilimali Watu wa Mamlaka hiyo, Bw. Ulimbakisya Masomelu alisema kwamba, lengo la kubwa la kuwapatia mafunzo waajiriwa hao ni kuhakikisha kwamba TRA inakuwa na nguvu kazi kubwa ya rasilimali watu katika kutekeleza majukumu yake.

Bwana Masomelu ameeleza kwamba, TRA ina majukumu makubwa ya kukusanya mapato nchi nzima na huo ni utaratibu wake wa kuwapatia mafunzo waajiriwa wake kwani mafunzo hayo yanawawezesha waajiriwa hao kuijua mamlaka hiyo jinsi inavyofanya kazi, ikiwemo mgawanyo wa majukumu (Organization Structure) pamoja na maadili ya utumishi.

“Lengo la kuwapatia semina hii elekezi waajiriwa wetu wapya ni kuwawezesha waweze kutambua dhima kubwa ya Mamlaka ya Mapato Tanzania ambayo ni kukusanya mapato, waweze kutambua pia maadili ya utumishi ili wanapoenda kutekeleza majukumu yao waweze kutekeleza kulingana na maadili ya kiutumishi, lakini pia waweze kujua mgawanyo wa majukumu ya TRA katika vitengo vyao”, alisema, Masomelu.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Mafunzo wa Mamlaka ya Mapato Tanzania, Bi. Pendo Mandia amesema kwamba, waajiriwa hao katika muda wao wote wa mafunzo ya siku kumi watapitishwa katika maeneo mbalimbali ili waweze kuyajua vizuri majukumu yao, ambapo baadhi ya mambo watayofanya ni pamoja na kufahamishwa juu ya muundo wa vitengo vyao, Sheria za Mamlaka ya Mapato, kufahamu Mkataba wa Huduma kwa Mlipakodi, kufahamu maadili na mwenendo wa utumishi wa umma.

Ameongeza kuwa, pamoja na hayo yote, waajiriwa hao wapya mara baada ya kukamilisha taratibu zote za ajira katika mamlaka hiyo watakula kiapo cha uadilifu kabla ya kuanza kutekeleza majukumu yao. Kwa upande wao baadhi ya waajiriwa hao wapya wameonyesha nyuso za furaha ya kupata ajira TRA na kuahidi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa pamoja na kuzingatia maadili ya utumishi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad