HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 28, 2017

MWANZA WAZINDUA MWONGOZO WA UWEKEZAJI WA MKOA

MKOA wa Mwanza umefanya Uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji ambao umeandaliwa na Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF).


Mwongozo huo ni sehemu ya ripoti tatu zilizotokana na agizo la mkoa wa Mwanza la kutaka kuwekewa pamoja taarifa sahihi zinazogusa uwekezaji mkoani humo ili kurahisisha na kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje.

Ripoti nyingine ni Fursafiche katika Viwanda (Industrialization Potentials Report), na Ripoti ya Fursa za Uwekezaji (Investment Opportunities Report) .

Akizungumza katika uzinduzi huo uliohudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, Mashirika ya Umma, Sekta binafsi na mashirika ya kimataifa, Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella, alisema walilazimika kuwatafuta wataalamu wa ESRF, kuwasaidia kuweka pamoja fursa zote za mkoa katika mpangilio mmoja unaobainisha fursa zilipo.

Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella akitoa hotuba ya uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa huo uliondaliwa na ESRF kwa chini ya ufadhili wa UNDP katika hafla fupi iliyofanyika katika viwanja vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa jijini Mwanza.

Alisema katika kukabiliana na changamoto hizo waliiomba Taasisi hiyo kufanya utafiti na uchambuzi wa kina ili kubaini fursa za uwekezaji zilizopo katika Mkoa huo na ndio wakatoka na ripoti tatu ikiwa Mwongozo huo.

Alisema kazi hiyo ilifanyika kwa miezi 4 kwa msaada wa kifedha kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kuanzia mwezi Julai 2017 hadi Novemba 2017.

Mongela alisema: wawekezaji wamekuwa wakipata taabu namna ya uoanishaji wa taarifa zinazotolewa kwao kutoka mamlaka moja hadi nyingine.
Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida akitoa taarifa kuhusu uandaaji wa Mwongozo wa Uwekezaji mkoani Mwanza ulioandaliwa na taasisi yake katika hafla fupi ya uzinduzi wa mwongozo huo uliofanyika jijini Mwanza.

Alisisitiza katika hotuba yake kuwa wawekezaji walikuwa wanapata majibu tofauti katika maswali yao walipofika katika mkoa huo kutoka kwa watendaji tofauti ambao ilikuwa lazima kuwaona ili kukamilisha nia yao ya kuwekeza .

Alisema kutokana na hali hiyo waliomba ESRF kuwasaidia kuweka pamoja takwimu zote na kuwavutia wawekezaji kwa kuwa na majibu ya maswali muhimu wanayotakiwa kuyajua kabla ya kuwekeza.

Mongela alisema kwamba mwongozo uliotengenezwa unakwenda sanjari na dira ya maendeleo ya Tanzania na kuwataka wawekezaji wa kigeni na nchini kuwekeza katika mkoa huo.
Mkuu na Mtaalamu wa Miradi kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania, Bw. Amon Manyama akitoa salamu za UNDP katika hafla fupi ya uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliofanyika kwenye viwanja vya ofisi za Mkuu wa Mkoa huo jijini Mwanza.
Alisema wakiwa katikati ya nchi za Afrika Mashariki, zenye soko la watu wapatao milioni 230, Mwanza ni sehemu muhimu na njema kabisa kwa uwekezaji.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa kazi waliyopewa Dkt. Tausi Kida, Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF) alisema pamoja na kukabidhi mwongozo huo, Ripoti zote zilithibitishwa na Mkoa Septemba 15, 2017 katika warsha maalum iliyoandaliwa na Mkoa (Validation Workshop).


Tayari ESRF imeshandaa na kuzindua Mwongozo kama huo Mkoani Simiyu mwanzoni mwa mwaka huu.

ESRF imeshakamilisha kuandaa Miongozo ya Uwekezaji katika Mikoa ya Mara na Kilimanjaro ambayo inatarajiwa kuzinduliwa ndani ya wiki mbili zijazo. Miongozo hii itasaidia sana katika kupata Mwongozo wa Uwekezaji wa Taifa utakaoonyesha fursa zilizopo nchini na katika kila mkoa.” Alisema Dkt Kida.

Mshiriki Mtafaifiti wa ESRF, Dkt Hoseana Lunogelo, akiwasilisha fursa za uwekezaji mkoani Mwanza walizoziona wakati wa kuandaa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa huo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa mwongozo huo jijini Mwanza.

Miongozo hiyo ya Uwekezaji, alisema Dkt. Kida inaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016 – 2021) unaosisitiza ujenzi wa Tanzania ya Viwanda ili kuifikisha nchi katika uchumi wa kati ifikapo 2025.

Pamoja na kutoa maelezo ya kazi Dk Kida alishukuru uongozi wa mkoa wa Mwanza na taasisi zake mbalimbali kwa kuwezesha ukusanyaji wa takwimu na kuandaa muongozo huo.

“Kwa namna ya pekee napenda kuushukuru Uongozi wa Mkoa wa Mwanza chini ya Mkuu wa Mkoa Mheshimiwa John Mongella, Katibu Tawala wa Mkoa – Kamishna wa Jeshi la Polisi Bw. Clodwing Mtweve na viongozi wengine wa mkoa na wilaya zote kwa kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wataalamu wetu wakati wanapita kutafuta maoni, taarifa na takwimu mbalimbali za kutayarishia Mwongozo huu.” Alisema Dkt. Kida na kuwashukuru pia Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa ufadhili wa fedha.
Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella (wa tatu kulia), Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (katikati), Mkuu wa Idara ya Maarifa na Ubunifu wa ESRF Bi. Margareth Nzuki (wa pili kulia), Mkuu na Mtaalamu wa Miradi kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania, Bw. Amon Manyama (wa tatu kushoto), Mtafiti Mshiriki wa ESRF, Dkt. Hoseana Lunogelo (wa pili kushoto) Watafiti vijana kutoka ESRF Bw. Mussa Martine (kushoto) pamoja na Bw. Joseph Nyampepela Ngonyani (kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja huku wakiwa wameshika nakala za Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Mwanza.

“Napenda kuishukuru timu yangu ya ESRF ikiongozwa na Bi. Margareth Nzuki, Mkuu wa Idara ya Maarifa na Ubunifu kwa kuratibu na kuongoza zoezi zima, watafiti washiriki kuanzia na Dkt. Hoseana Lunogelo, Prof. Haidari Amani na Prof. Samuel Wangwe kwa kupitia mwongozo huu.” Alisema na kuwashukuru watafiti vijana waliojitoa kwa nguvu zote kufanikisha kazi hiyo.

Aliwataja vijana hao kuwa ni Bw. Mussa Martine, Bw. Joseph Nyampepela Ngonyani pamoja na Bw. Hafidhi Kabanda .

“Aidha, natambua mchango mkubwa aliotoa marehemu Abdallah Hassan katika uandaaji wa Mwongozo huu.” Alisema.

Aidha alisema kazi hiyo ilifanyika kwa kushirikisha wadau kutoka Sekretarieti ya Mkoa; Halmashauri zote za mkoa wa Mwanza, yaani Mwanza Mjini, Magu, Kwimba, Sengerema, Buchosa, Ukerewe, Ilemela na Misungwi; pamoja na wadau kutoka Sekta binafsi.
Mwenyekiti wa Shirikisho la wenye Viwanda nchini (CTI), Dkt. Samuel Nyantahe akitoa neno la shukrani kutoka CTI wakati hafla ya uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliofanyika katika viwanja vya ofisi za Mkuu wa Mkoa Mwanza.

Aidha Mkurugenzi huyo aliutaka mkoa kutosita kuwatumia pale wanapohitaji msaada wa kitaalam katika utekelezaji wa Mwongozo na hata kusaidia katika kufanya upembuzi yakinifu (Feasibilty Study) na kuandaa Business Plans kwa baadhi ya fursa ambazo Mkoa utapenda kuwekeza.

Naye Amon Manyama, Mkuu na Mtaalamu wa Miradi kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania akizungumza alipopewa nafasi aliwahimiza wananchi wa mwanza kutumia fursa zilizopo kuwekeza badala ya kuwaachia wageni pekee.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI), Leodegar Tenga akisisitiza jambo kwenye hafla ya uzinduzi wa Mwomgozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliondaliwa na ESRF chini ya ufadhili wa UNDP jijini Mwanza.

Alisema kwamba shirika lake litaendelea kushirikiana na Mwanza katika kuhakikisha kwamba Jiji hilo linaipiku Dar Es Salaam katika uchumi kwa kusaidia kupata wawekezaji wenye uhakika kutoka hata ughaibuni.

Alisema Mwanza ikiwa katikati ya Afrika Mashariki ina kila nafasi ya kukua kwa kasi na wao kama UNDP watahakikisha kwamba wanatoa ushauri wa namna ya kujenga uchumi kwa kutumia sekta binafsi na namna ya kushirikiana na taasisi za kitafiti kama ESRF.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni Mbunge wa Ilemela jijini Mwanza, Mh. Angelina Mabula akizungumza kwa niaba ya Wabunge wa jijini humo mara baada ya uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa huo uliofanyika katika viwanja vya ofisi za Mkuu wa mkoa wa Mwanza.Picha juu na chini ni mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella (wa tano kulia) na Mkurugenzi wa Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida (wa sita kushoto) kwa pamoja wakizindua Mwongozo wa Uwekezaji mkoani Mwanza iliyoandaliwa na ESRF na kufadhiliwa na UNDP. Wanaoshuhudia tukio hilo ni Mkuu na Mtaalamu wa Miradi UNDP Tanzania, Amon Manyama (wa nne kushoto), Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI) Dkt. Samuel Nyantahe (wa tano kushoto), Kamishna wa Jeshi la Polisi Bw. Clodwing Mtweve (wa pili kulia) pamoja na viongozi wa madhehebu ya dini na wa mkoa wa Mwanza katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella na meza kuu wakionyesha nakala za Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa huo baada ya kuzinduliwa rasmi katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella katika picha ya pamoja na Wakuu wa wilaya za jiji la Mwanza huku wakiwa wameshika nakala za Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliondaliwa na ESRF chini ya ufadhili wa UNDP.
Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella katika picha ya pamoja na taasisi za sekta binafsi yakiwemo mabenki na mifuko ya jamii mara baada ya uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza.
Picha juu na chini ni Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella katika picha ya pamoja na wawekezaji wa jijini Mwanza mara baada ya kuzindua Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni Mbunge wa Ilemela jijini Mwanza, Mh. Angelina Mabula (wa kwanza kushoto) akifurahi jambo wakati wa uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliondaliwa na ESRF na kufadhiliwa na UNDP.
Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mh. John Mongella (wa tatu kushoto), Kamishna wa Jeshi la Polisi Bw. Clodwing Mtweve (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (wa tatu kulia), Mkuu na Mtaalamu wa Miradi kutoka Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania, Bw. Amon Manyama (wa pili kulia), Kiongozi wa dhehebu ya dini Kiislamu pamoja na Mwenyekiti wa Shirikisho la wenye Viwanda nchini (CTI), Dkt. Samuel Nyantahe wakati wa uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Mwanza.
Mshiriki Mtafaifiti wa ESRF, Dkt Hoseana Lunogelo (wa kwanza kushoto), Mkuu wa Idara ya Maarifa na Ubunifu wa ESRF, Margareth Nzuki (katikati) na Mtafiti Mshiriki Bw. Joseph Nyampepela Ngonyani wakifuatilia shughuli mbalimbali zilizokuwa zikijiri kwenye uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Mwanza ulioandaliwa na ESRF na kufadhiliwa na UNDP.
Wakuu wa Wilaya za Mikoa ya Mwanza walioshiriki uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza.
Pichani juu na chini ni baadhi ya wadau kutoka sekta binafsi na serikali waliohudhuria uzinduzi wa Mwongozo wa Uwekezaji wa mkoa wa Mwanza uliondaliwa na ESRF na kufadhiliwa na UNDP ambapo uzinduzi huo umefanyika katika viwanja vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad