HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, August 7, 2017

OFISI YA TAKWIMU YA TAIFA YA KANUSHA TAKWIMU ZILIZOTOLEWA NA GEOPOLL.

1.      Hivi karibuni kumekuwa na takwimu zinazotolewa na Kampuni ya GeoPoll yenye Ofisi ya Kanda ya Afrika Mjini, Nairobi Kenya. Takwimu hizo ambazo hutolewa kwa njia ya mitandao ya kijamii, zinahusu ukusanyaji wa taarifa za Televisheni na Redio nchini kwa idadi ya watazamaji na zinatolewa kila baada ya miezi mitatu.

2.      Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inapenda kuujulisha umma kuwa takwimu hizo sio Takwimu Rasmi (Official Statistics) kwa kuwa hukusanywa kwa mfumo ambao hautambuliwi na NBS kwa mujibu wa kifungu cha 20 cha Sheria ya Takwimu ya mwaka 2015.

3.      Takwimu Rasmi kama ilivyofafanuliwa katika kifungu cha 20 cha Sheria ya Takwimu ni takwimu ambazo zimetolewa kwa kufuata Misingi ya utoaji Takwimu Rasmi (Fundamental Principles of Official Statistics) na utolewaji wake umeratibiwa na NBS. Hivyo basi, takwimu zinazotolewa na taasisi au mtu yeyote  zitatambuliwa kuwa  Takwimu Rasmi  iwapo tu  zitakidhi vigezo vinavyotolewa na  kusimamiwa na NBS.

4.      Kwa mantiki hiyo, takwimu zinazotolewa na mtu au taasisi yoyote  bila kufuata au kukidhi vigezo vinavyotolewa na NBS kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu, hazitambuliwi kuwa ni Takwimu Rasmi na kwa maana hiyo haziwezi  kutumika katika kupanga mipango ya maendeleo ya nchi.

5.      NBS inaitaka Kampuni ya GeoPoll kufuata taratibu zilizoainishwa katika Sheria ya Takwimu, kwa kuwa takwimu zinazotolewa na kampuni hiyo hazijakidhi vigezo vya Takwimu Rasmi na zinapotosha umma na kuleta  mkanganyiko kwa wadau pamoja na  kuathiri mahusiano ya kiutendaji baina ya  vyombo  vya habari hapa nchini.
Kuhusu Ofisi ya Taifa ya Takwimu.

Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ni taasisi ya Umma iliyoanzishwa kwa Sheria ya Takwimu ya Mwaka 2015. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, NBS imepewa mamlaka ya kutoa, kusimamia na kuratibu upatikanaji wa takwimu rasmi kwa ajili ya matumizi ya Serikali na wadau wa takwimu.

Aidha, kifungu cha 6 cha Sheria hiyo ya takwimu, kinaipa NBS jukumu la kutoa na kusimamia Miongozo na Viwango vya utoaji wa Takwimu Rasmi.

Imetolewa na: Mkurugenzi Mkuu, Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Dar es Salaam.
07 Agosti, 2017.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad