WAZIRI wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi amewaasa
watumishi wa mahakama kushughulikia vitendo vya rushwa kwani vinaipatia mahakama
taswira hasi na kuzitaka tume za mahakama na maadili kuchunguza vitendo vya
ukiukwaji wa maadili na kuchukua hatua stahiki.
Waziri Kabudi, amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati
akizungumza na watumishi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani juu ya
mustakabali wa taasisi hiyo, ikiwa ni mara yake ya kwanza kufanya ziara tangu alipoteuliwa kuwa
Waziri.
Amesema, majaji na mahakimu mara nyingi, wamekuwa
wakihusishwa na vitendo vya rushwa hivyo, na kuchangia kuwepo kwa kutokuwa na
imani kwa wananchi wanaokuwa na shida ,mbali mbali katika taasisi hizo, hasa
wale wenye kesi.
‘’Pamoja na mabadiliko
makubwa katika mahakama bado kumekuwa na changamoto ya uadilifu hususan vitendo
vya rushwa na uwajibikaji ambavyo vimeleta taswira hasi kwa wananchi
wanaotafuta haki na kusababisha ushiriki mdogo,’’alisema Profesa Kabudi.
Ameongeza, watendaji wanapaswa kubuni mbinu mbali mbali za
kuweza kubadili taswira hiyo kwa kuwachukulia hatua za kinidhamu wanaokiuka
maadili na kusogeza huduma kwa wananchi.
Kwa mujibu wa Profesa Kabudi, mahakama inanafasi kubwa ya
kuchangia maendeleo ya nchi na kwamba jambo wanalopaswa kufanya ni kuimarisha
utendaji kazi na kutokomeza rushwa.
Kwa upande wake, Kaimu Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma
alisema kuwa wataendelea kutumia sheria kwa ajili ya kuwainua wananchi wengi
kwa lengo la kukuza uchumi.
Profesa Juma alisema majaji na mahakimu ni sehemu ya jamii
ambao wanapaswa kushiriki kustawisha wanaqnchi ili kutokomeza umasikini.
Akiwasilisha ripoti kuhusu mahakama, Mtendaji Mkuu wa
mahakama, Hussein Katanga alisema kuwa idadi ya majaji imeshuka kutoka 100 hadi
80 huku uhitaji wake ukiwa ni kati ya 100 hadi 120.
Katanga alisema majaji 20 wameacha kazi kwa sababu
mbalimbali ikiwemo kustaafu na kwamba uhitaji huo unachangia kasi ya kuongezeka
kwa ufunguaji mashauri.
No comments:
Post a Comment