HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, June 29, 2017

RAIS DKT. MAGUFULI ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUFUATIA KIFO CHA DKT. TONIA KANDIERO

Dkt. Tonia Kandiero

“Kwa mshituko na masikitiko makubwa nimepokea taarifa za kifo cha Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) katika Kanda ya Afrika Kusini Dkt. Tonia Kandiero aliyefariki dunia ghafla jana usiku tarehe 28 Juni, 2017 akiwa ofisini kwake huko Pretoria Afrika Kusini”

Hii ni kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli aliyoitoa leo tarehe 29 Juni, 2017 Ikulu Jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya kupokea taarifa za kifo cha Dkt. Tonia Kandiero ambaye kabla ya kuteuliwa kushika wadhifa wa Mkurugenzi Mkuu wa AfDB katika Ofisi za Kanda ya Afrika Kusini mwishoni mwa mwaka 2016 alikuwa Mwakilishi wa AfDB Tanzania.

“Nitamkumbuka Dkt. Tonia Kandiero kama mchapakazi hodari aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi yetu, nikiwa Waziri wa Ujenzi nimeshirikiana nae kwa karibu kufanikisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo kwa nchi yetu ambayo imefadhiliwa na AfDB, ametoa mchango mkubwa kufanikisha ujenzi wa madaraja na barabara za Dodoma – Iringa, Dodoma – Babati, Namtumbo – Tunduru – Mtambaswala, Arusha – Taveta – Voi na pia alitoa mchango mkubwa katika kufanikisha miradi mingine ambayo ipo mbioni kutekelezwa ikiwemo ujenzi wa barabara ya Bagamoyo – Tanga – Mombasa, Mbinga – Mbambabay na Tabora - Katavi”.

Kufuatia kifo cha Dkt. Tonia Kandiero Mhe. Rais Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Rais wa AfDB Dkt. Akinwumi Adesina, familia ya Dkt. Tonia Kandiero, wafanyakazi wote wa AfDB, ndugu, jamaa na marafiki wote walioguswa na msiba huu.

Dkt. Magufuli amemuombea marehemu Dkt. Tonia Kandiero apumzishwe mahali pema peponi, Amina.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
29 Juni, 2017

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad