HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, April 20, 2017

DODOMA WAPONGEZA UBORESHAJI HUDUMA ZA NHIF

 Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Dodoma, Salome Manyama akipokea cheti cha ushiriki wa Maonesho ya Mifuko ya Uwezashaji kutoka kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
 Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Antony Mavunde akimsikiliza Meneja wa NHIF, Mkoa wa Dodoma Salome Manyama alipotembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya Mifuko ya Uwezeshaji.
 Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Antony Mavunde akisaini kitabu cha wageni katika banda la NHIF.
 Ofisa wa NHIF, Enock Humba akitoa elimu kwa wananchi waliofika bandani hapo.
Maofisa wa NHIF, Grace Michael na Enock Humba wakihudumia wananchi waliofika bandani hapo kupata ufafanuzi wa mambo mbalimbali yanayohusu huduma za Mfuko.


Na Grace Michael, Dodoma
Wananchi wa Mkoa wa Dodoma wamepongeza mpango unaotekelezwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unaojulikana kama Toto Afya Kadi kwa kuwa ni msaada mkubwa kwa watoto chini ya umri wa miaka 18.

Mbali na mpango huo, wamesema kuwa hatua kubwa ya uboreshaji wa huduma za matibabu uliofikiwa na Mfuko huo kwa sasa unatoa hamasa kwa Watanzania kujiunga na huduma zake na kunufaika nazo.

Hayo wameyasema kwa nyakati tofauti mjini hapa wakati wa maonesho ya Mifuko ya Uwezeshaji ambayo yalizinduliwa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa ambayo yatahitimishwa Aprili 22, mwaka huu.

“Kwa kweli NHIF kwa sasa tunawapongeza sana hasa kwa kuwa na madirisha mengi ambayo yanamwezesha kila mwananchi kujiunga na kutumia huduma za Mfuko huu…awali Mfuko ulihudumia watumishi wa Umma tu lakini kwa sasa tunashukuru na tunawapongeza kwa hili,” alisema Bw. Sebastian Kingu.

Akizungumzia huduma za matibabu mmoja wa wanachama waliotembelea banda la Mfuko, Bi. Prisca Peter alisema kuwa Mfuko umekuwa mkombozi mkubwa wa afya za wananchi wengi na imesaidia kwa kiasi kikubwa hasa wanachama wake wanapopatwa na maradhi yanayohitaji fedha nyingi.

“Mimi binafsi niushukuru sana Mfuko huu maana mpaka sasa katika familia yangu tumepata huduma ya upasuaji tena mkubwa ambao bila Mfuko ingeleta shida kubwa ndani ya familia lakini kwa kuwa tunahudumiwa na Mfuko tulipata matibabu vizuri kabisa bila kutoa hata shilingi moja,” alisema Bi. Prisca.

Alipotembelea banda hilo, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Antony Mavunde alisema kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanafikiwa na utaratibu huu wa kupata huduma kupitia Bima za Afya hivyo akautaka Mfuko kuongeza kasi ya utoaji elimu na uhamasishaji kwa wananchi.

Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umekuwa ukishiriki shughuli mbalimbali zinazofanyika kwa wananchi kwa lengo la kuwafikia Watanzania wengi na kutoa huduma bora ya matibabu.

Katika maonesho hayo, Mfuko unatoa elimu na kuhamasisha wananchi kujiunga na Mfuko kupitia makundi yaliyowekwa ili wanufaike na huduma za matibabu.

Akizungumzia hilo, Meneja wa NHIF, Mkoa wa Dodoma Bi. Salome Manyama alisema kuwa Mfuko umejipanga kuhakikisha unatoa huduma nzuri na bora zaidi kwa wanachama wake lakini pia kuhakikisha unahamasisha wananchi kujiunga ili wanufaike na huduma zinazotolewa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad