HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, February 15, 2017

TAKUKURU YAWABURUZA MAHAKAMANI WATUMISHI WA WIZARA YA ELIMU MANISPAA YA ILALA

 Watuhumiwa wa ubadhilifu wa fedha wakifikishwa katika mahakama ya Hakimu mkazi kisutu jijini Dar es Salaam
  
Na Karama Kenyunko, Globu ya Jamii.
Watumishi  wanne wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi akiwemo Mkurugenzi na Mhasibu wamepandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwana mashtaka saba yakiwemo ya ubadhirifu na ufujaji wa fedha na kuisababishia wizara hasara ya zaidi ya milioni 41.
Akisoma hati ya mashtaka, Mwendesha Mashtaka, wakili wa serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB), Emmanuel Jacob aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Mkurugenzi  Bakari Issa, Mhasibu Emmanuel Mayuma, Mkurugenzi  Msaidizi Hellen Lihawa na Mhasibu Msaidizi Mbarouk Dachi.
Mbele ya Hakimu Mkazi, Wilbard Mashauri ilidaiwa kuwa washtakiwa hao kwa makusudi na kwa nia ya kudanganya walitumia malipo ya tarehe 16 Julai 2014 kwa jina la Emanuel Mayuma ambayo ilikuwa na taarifa ya uongo kuonyesha kuwa zaidi ya sh. Milioni 18.4 zilikuwa ni malipo kwa ajili wanafunzi waliohudhuria  mafunzo ya michezo  yaliyokuwa yamedhaminiwa na  British Council huku wakijua siyo kweli.
Aidha watumishi hao wanadaiwa kufanya ubadhirifu na ufujaji wa fedha kati ya Agosti 30 na Septemba 10 mwaka 2014 na kujipatia kiasi hicho cha milioni 18 ambazo zilikuwa ni kwa ajili ya mpango wa walimu kwa mafunzo ya kadi za michezo  zilizofadhiliwa na British Council.
Mhasibu Mayuma anadaiwa peke yake kuwa, kati ya Agosti 10 na Septemba 2014 wizarani hapo alitumia vibaya kiasi cha shilingi milioni 31.7 alizokuwa amekabidhiwa kwa ajili ya kugaramia mpango wa matumizi ya kadi za michezo. 
Katika hatua nyingine watuhumiwa hao wote wanadaiwa kushindwa kutumia madaraka yao vibaya na kuisababisha wizara ya Elimu hasara  zaidi ya shilingi milioni 18.4/- wakati Mhasibu Mayuma aliisababishia wizara hiyo hasara ya shilingi milioni 41.2.
Hata hivyo washtakiwa wamekana mashtaka na wako nje baada ya kuweka dhamana ya shilingi milioni 50 kila mmoja na kuleta wadhamini wawili wa uhakika. Aidha washtakiwa hao hawaruhusiwi kusafiri nje ya  Dar es Salaam bila kupata kibali cha mahakama.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 1, upelelezi bado haujakamilika.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad