Watuhumiwa wa ubadhilifu wa fedha wakifikishwa katika mahakama ya Hakimu mkazi kisutu jijini Dar es Salaam
Na Karama Kenyunko, Globu ya Jamii.
Watumishi wanne wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi
Stadi akiwemo Mkurugenzi na Mhasibu wamepandishwa katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu wakikabiliwana mashtaka saba yakiwemo ya ubadhirifu na ufujaji wa
fedha na kuisababishia wizara hasara ya zaidi ya milioni 41.
Akisoma hati
ya mashtaka, Mwendesha Mashtaka, wakili wa serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (PCCB), Emmanuel Jacob aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Mkurugenzi
Bakari Issa, Mhasibu Emmanuel Mayuma, Mkurugenzi
Msaidizi Hellen Lihawa na Mhasibu Msaidizi
Mbarouk Dachi.
Mbele ya Hakimu
Mkazi, Wilbard Mashauri ilidaiwa kuwa washtakiwa hao kwa makusudi na kwa nia ya
kudanganya walitumia malipo ya tarehe 16 Julai 2014 kwa jina la Emanuel Mayuma
ambayo ilikuwa na taarifa ya uongo kuonyesha kuwa zaidi ya sh. Milioni 18.4
zilikuwa ni malipo kwa ajili wanafunzi waliohudhuria mafunzo ya michezo yaliyokuwa yamedhaminiwa na British Council huku wakijua siyo kweli.
Aidha
watumishi hao wanadaiwa kufanya ubadhirifu na ufujaji wa fedha kati ya Agosti 30
na Septemba 10 mwaka 2014 na kujipatia kiasi hicho cha milioni 18 ambazo
zilikuwa ni kwa ajili ya mpango wa walimu kwa mafunzo ya kadi za michezo zilizofadhiliwa na British Council.
Mhasibu
Mayuma anadaiwa peke yake kuwa, kati ya Agosti 10 na Septemba 2014 wizarani
hapo alitumia vibaya kiasi cha shilingi milioni 31.7 alizokuwa amekabidhiwa kwa
ajili ya kugaramia mpango wa matumizi ya kadi za michezo.
Katika hatua
nyingine watuhumiwa hao wote wanadaiwa kushindwa kutumia madaraka yao vibaya na
kuisababisha wizara ya Elimu hasara zaidi ya shilingi milioni 18.4/- wakati Mhasibu
Mayuma aliisababishia wizara hiyo hasara ya shilingi milioni 41.2.
Hata hivyo
washtakiwa wamekana mashtaka na wako nje baada ya kuweka dhamana ya shilingi
milioni 50 kila mmoja na kuleta wadhamini wawili wa uhakika. Aidha washtakiwa
hao hawaruhusiwi kusafiri nje ya Dar es
Salaam bila kupata kibali cha mahakama.
Kesi hiyo
imeahirishwa hadi Machi 1, upelelezi bado haujakamilika.
No comments:
Post a Comment