HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, February 17, 2017

PROFESA MBARAWA ATEMBELEA NA KUKAGUA KIVUKO CHA MV KILAMBO MKOANI MTWARA

 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasaliano Mhe. Profesa Makame Mbarawa (katikati) akimsikiliza Mkuu wa Kivuko cha MV Kilambo kinachomilikiwa na TEMESA Jaston Mbawala wakati wa ziara ya kikazi aliyoifanya mkoani Mtwara. Kulia kwa Waziri ni Mhandisi Samwel Chibwana wa TEMESA Mtwara.
 Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mkoa wa Mtwara Mhandisi Saidi Mongomongo akimuelezea jambo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Profesa Makame Mbarawa alipotembelea kivuko cha MV Kilambo kilichopo mkoani Mtwara kinachotoa huduma mto Ruvuma mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Profesa Makame Mbarawa akikagua injini ya kivuko cha MV Kilambo kinachotoa huduma mto Ruvuma kati ya Kilambo, Tanzania na Namoto, Msumbiji. Picha na Alfred Mgweno, TEMESA

Na Alfred Mgweno, TEMESA Mtwara.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Profesa Makame Mbarawa ametembelea na kukagua kivuko cha MV Kilambo kilichopo Mkoani Mtwara mpakani mwa Tanzania na Msumbiji. Kivuko hicho kinavusha magari, abiria na mizigo kati ya Kilambo upande wa Tanzania na Namoto Msumbiji.

Akiwa katika ziara hiyo Profesa Mbarawa aliambatana na viongozi mbalimbali wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano mkoani hapa. Profesa Mbarawa  alikaribishwa na Mkuu wa Kivuko hicho Jaston Mbawala, Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wa Mkoa wa Mtwara Mhandisi Saidi Mongomongo, Mhandisi  Msaidizi wa Kivuko Samwel Chibwana pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ukodishaji Mitambo na Huduma za Vivuko Mhandisi Japhet Y. Maselle.

Akiwa kivukoni hapo, Profesa Mbarawa alipata wasaa wa kusikiliza baadhi ya  changamoto zinazokikumba kivuko hicho ambapo Mhandisi Saidi Mongomongo alitaja changamoto hizo kuwa ni upungufu wa maji nyakati za kiangazi, ubovu wa maegesho ambayo husababisha magari makubwa kunasa wakati yanatoka au kuingia ndani ya kivuko pamoja na kukosekana kwa boti ndogo za uokoaji ambazo zingesaidia wakati wa dharura.

Baadae Profesa Mbarawa alipata fursa ya kuongea na watumishi walio chini ya Wizara yake katika kikao kilichofanyika ofisi ya Mkuu wa mkoa huku akiwataka watumishi  kuendelea kushirikiana na serikali, kufanya kazi kwa kasi na uadilifu kwa kuzingatia weledi. Pia aliwataka watumishi kujenga tabia ya kujitoa kwa ajili ya nchi yao.


Profesa Mbarawa alikuwa kwenye ziara ya kikazi ya siku moja mkoani humo kwa nia ya kutembelea na kukagua utendaji kazi wa taasisi zilizo chini ya wizara yake.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad