HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 28, 2017

MEYA ILALA AFUNGUA RASMI DARAJA LA BONYOKWA-KINYEREZI

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko, akihutubia wananchi baada ya kufungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.
Mbunge wa Viti Maalumu, Anatropia Theonesti (Chadema) akihutubia wakati wa ufunguzi wa daraja hilo
Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko, akikiwa amekata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.

Mwandishi wetu
MSTAHIKI MEYA wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko jana alifungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.

Awali akizungumza katika hafla hiyo Mhandisi wa Manispaa ya Ilala ndugu Benjamin Maziku alisema  daraja hili limejengwa kwa takribani mwaka mmoja na kugharimu Tsh.million  478 hadi kukamilika kwake leo hii. Ujenzi wa daraja hili umesua sua kwa siku nyingi kutokana na sababu mbali mbali lakini kutokana na usimamizi imara wa Mstahiki Meya wa Ilala Mhe. Charles Kuyeko sasa historia imebadilika.

Meya Kuyeko akizungumza na umati wa wananchi waliokusanyika kushuhudia ufunguzi huo amewasitiza kulilinda na kulitunza vyema daraja hilo kwani limejengwa kwa kodi zao.

Awali, Meya akitoa historia ya daraja hilo amesema kuwa, waliokuwa wanatakiwa kujenga daraja hilo ni wakala wa Barabara Tanzania (Tanroad) lakini kutokana na kusuasua kwao, Mimi (Meya)  niamua kuingilia kati kwa Manispaa kutenga Fedha kujenga daraja la muda ili kuwasaidia wananchi wa Bonyokwa kuondokana na atha ya kuwa Kisiwa hususani wakati wa Mvua.

Kuyeko ambaye pia ni Diwani wa kata ya bonyokwa amewaambia wananchi hao waliofurika kwenye uzifunguzi huo kuwa huo ni mwanzo tu wa utekelezaji wa ahadi zake katika kutatua kero za wananchi na wapiga kura wake. "Nawahakikishia kuwa hamtajutia kunipa kura zenu kwani daraja hili imekuwa kero ya miaka nenda rudi lakini Mimi nimeimaliza kwa muda mfupi kwa kushirikiana na watendaji wangu hivyo mtarajie mengi kabla mwaka huu kuisha hata daladala zitakuwa zinafika hadi kisiwani".

Mbali na hayo,Meya amewaahidi wananchi hao muda mfupi ujao atatatua kero ya maji na barabara kama ambavyo aliahidi kutekeleza wakati wa kampeni.

Ufunguzi huo ulihudhuliwa na viongozi mbali mbali wa kiserikali na kisiasa akiwemo mbunge wa Viti Maalum Mhe. Anatropia Theonest, madiwani wa kata mbalimbali na viongozi wa vyama vya siasa.

Akitoa salam kwa niaba ya viongozi wa vyama vya siasa, Dk.Makongoro Milton Mahanga mbunge wa zamani jimbo la Segerea ambaye kwa sasa ni, Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Ilala alisema, "Tangu niwe kiongozi sijawahi kuona kiongozi mahiri kama Meya Kuyeko. 

Ameweza kuwaunganisha viongozi wa Manispaa yake na kuwa kitu kimoja, na hadi sasa ameshafanya vitu vingi ambavyo awali vilishindikana nakupongeza sana Meya Kuyeko.

Dkt. Mahanga  aliwasisitiza wananchi kuwaamini viongozi wanaotokana na UKAWA kwani ni wazuri jifunzeni kwa Kuyeko mambo makubwa anayoyafanya. Kwa niaba ya Chadema nampongeza sana Meya Kuyeko kwa kukiwakirisha vyema  chama kwa wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Chadema Jimbo la Segerea ndugu Gango Kidera aliwataka wananchi wa Bonyokwa  waendelee kumwamini na kumuunga mkono Meya Kuyeko, Baraza lake la Madiwani kwani amekuwa mfano bora kwa kutekeleza ahadi zake zinazotokana na ilani na Sera za Chadema/UKAWA. 

Chadema imemtuma Kuyeko kuwatumikia wananchi wa Bonyokwa na Manispaa nzima ya Ilala kwa kuhakikisha anatatua kero zao kwa spidi ya mwendokasi na leo tumeona anatenda kwa maslahi ya wananchi. Nakupongeza sana Meya Kuyeko, alisema Kidera

Viongozi wengine waliozungumza katika ufunguzi huo ni Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Anatropia Theonest ambaye aliwapongeza wananchi wa Bonyokwa kwa kumchagua Kuyeko, wananchi wa Bonyokwa mlifanya maamuzi sahihi kuchagua Chadema kwa sababu bila Chadema Meya Kuyeko tusingempata. 

Anatropia pia alimpongeza Meya Kuyeko kwa kuendelea kutatua kero za wapiga kura wa Bonyokwa siku hadi siku na Ilala kwa ujumla. UKAWA kwa Manispaa ya Ilala chini ya Meya Kuyeko imeleta matumaini makubwa kwani wakazi wa Manispaa wapatao 1,415,443 walikuwa wamekata tamaa kabisa kwani viongozi waliopita walishindwa kutatua kero za wananchi, hivyo UKAWA chini ya Meya Kuyeko ni mfariji mkuu wa wananchi, alisema Anatropia.

Diwani wa Buguruni Mhe. Penza wa CUF akizungumza kwa niaba ya Madiwani wa Ilala alisema ilani ya UKAWA imeweka vipaumbele kwenye Barabara, maji, afya, elimu, na masoko na mitaji hivi vyote vinafanyika.

Meya Kuyeko aliwashukuru wananchi kwa kuendelea kumwamini na kumpa ushirikiano wa karibu hali ambayo inampa ari ya kuwatumikia kwa nguvu zake zote. Pia amekishukuru chama chake Chadema, viongozi, Madiwani na watendaji wote wa Manispaa ya Ilala wakiongozwa na Mkurugenzi kwa kumpa ushirikiano wa hali na Mali katika kuwatumikia wananchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad