HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 20, 2023

Mradi wa Umeme wa Upepo wa Zanzibar wapamba moto

 

 


Na Mwandishi wetu

Zanzibar. Mradi wa umeme wa upepo wa Zanzibar unazidi kupamba moto baada ya kampuni ya Aseel Oilfield Services Limited ya Dubai na Sany Renewable Energy ya China kutembelea maeneo yanayoweza kuwa na shamba ambayo yatazalisha nishati hiyo Makunduchi na Bambi.

Mradi huo wenye thamani ya Dola za Kimarekani 340 milioni (Sh bilioni 800 za Kitanzania) unatarajia kuanza utekelezaji wake mara baada ya kusainiwa kwa mkataba wa manunuzi wa Umeme (PPA) kati ya kampuni ya Aseel Oilfield Services Limited na Wizara ya Maji,Nishati na Madini ya Zanzibar.

Mradi huo unatarajia kuzalisha MW 20 na 200 kwa Meneja wa kampuni ya Sany Renewable Energy, Hebren James.

Bw James alisema kuwa ushirikiano na kampuni ya b Aseel Oilfield Services ni hatua muhimu katika kusaidia na kuimarisha ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

"Ushirikiano huu umekuja kutokana na Mkataba wa Makubaliano (MoU) uliotiwa saini kati ya Aseel Oilfield Services Limited na serikali ya Zanzibar mwezi Julai mwaka huu . Kama moja ya wazalishaji wakuu wa mitambo ya upepo duniani,” alisema Bw. James.

Alisema kuwa mradi huo unatarajia kukamilika ndani ya miezi 18 mara baada ya kusainiwa kwa mkataba wa manunuzi wa umeme baina ya kampuni ya Aseel Oilfield Services na serikali ya Zanzibar.

Alisema kuwa mradi huo utachangia kwa kiasi kikubwa kukidhi mahitaji mengi ya umeme ya Zanzibar.

Wakati wa ziara hiyo, timu kutoka Aseel Oilfield Services Limited na Sany Renewable Energy walitathmini kwa makini maeneo yanayoweza kutumika kwa ajili ya shamba la upepo katika maeneo ya Bambi na Malindi. Lengo la msingi lilikuwa kutambua maeneo yenye uwezo wa juu zaidi wa kuzalisha nishati ya upepo, kuhakikisha ufanisi na ufanisi wa shamba la upepo la siku zijazo.

Baada ya kufanya ziara hiyo, viongozi wa kampuni hizo mbili walikutana na Katibu Mkuu Kiongozi wa Zanzibar Bw Joseph Kilangi pamoja na wakurugenz na timu ya ufundi waandamizi na wahandisi wa Wizara ya Maji, Nishati na Madini na kuwasilisha matokeo ya ziara hizo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na maafisa wa Aseel Group of Companies, Bw. Iman Al-Jabry, ambaye ni mwenyekiti wa kampuni na Bw. Saeed Al-Jabry ambaye ni mkurugenzi mkuu.

Majadiliano haya yalilenga jinsi gani ya kufanikisha mradi huo wenye tija kwa Zanzibar.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Nishati na Madini wa Zanzibar Bw, Shaib Hassan Kaduara alisema kuwa wamefurahishwa na mkakati wa mradi huo na kuzipongeza kampuni hizo kwa kuonyesha dhamira ya dhati kuufanikisha.

“Kwa kweli nimefarijika sana kuona jitihada za mradi wa umeme wa upepo kupitia kampuni hizi mbili. Tunaamini mdardi huu utafanikishwa na kuchangia uchumi,” alisema Bw Kuduara.

Pia, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Bw. Shaaban Ali Othman na Katibu Mkuu Kiongozi, Joseph J. Kilangi, walitoa shukrani kwa juhudi za mashirikiano zinazofanywa na sekta binafsi na taasisi za serikali katika kuleta maendeleo endelevu.




Katibu Mkuu Kiongozi wa Zanzibar Bw Joseph J. Kilangi (wa sita kulia) akipokea picha ya mfano ya mtambo wa umeme wa upepo kutoka kwa Bw. Hebren James, Meneja wa kampuni ya Sany Renewable Energy (wa tano kushoto) mara baada ya kukagua maeneo yanayoweza kujengwa kwa ajili ya mradi wa nishati ya umeme upepo. Wengine katika picha ni viongozi mbalimbali wa kampuni ya Aseel Oilfield Services na mwakilishi kutoka Wizara ya Maji, Nishati, na Madini.

Waziri wa Maji, Nishati na Madini wa wa Zanzibar Bw. Shaib Hassan Kaduara (wa tatu kushoto) akisalimiana na maofisa wa kampuni za Aseel Oilfield Services Limited na Sany Renewable Energy mara baada ya majadiliano kuhusiana na mradi wa umeme wa upepo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad