HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, September 17, 2022

UMADIDO Wajenga nyumba kwaajili ya mshindi wa shindano la 'The Royar tour'

 Na. Sifa Stanley, DODOMA

MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri aupongeza Umoja wa Madereva Bodaboda Dodoma (UMADIDO) kwa kujenga nyumba kwaajili ya mshindi wa shindano la “the Royar tour”.

Pongezi hizo alizitoa leo alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba iliyojengwa kwaajili ya mshindi wa shindano la Pikipiki linalojulikana kama the Royal Tour, nyumba imejengwa katika Kata ya Iyumbu katika Wilaya ya Dodoma.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kuwa wazo walilokuwa nalo na walilolifanyia kazi ni wazo zuri ambalo linamanufaa kwa waendesha pikipiki wote maarufu kama bodaboda wote na kwa taifa.

“Nyinyi sio bodaboda tena, nyinyi ni Maafisa Usafirishaji na Rais mwenyewe aliwapandisha hadhi nyinyi ni maafisa kwa sasa. Kwahiyo, kwa jambo hili mlilofanya ni jambo zuri sana niwapongeze sana kwa jambo hili. Lakini pia niwashauri mtengeneze logo kwaajili ya umoja wenu ili hiyo logo itumike kuwatangaza huko na itatumika kuwaingizia kipato pia”, alisema Shekimweri

Naye, Keneth Chimoti Mwenyekiti wa UMADIDO alieleza namna nyumba hiyo itakavyotumika kuwasaidia maafisa usafirishaji kutoa huduma zao na kuhamasisha utekelezwaji wa ujenzi wa jengo la kitega uchumi kwaajili ya maafisa usafirishaji.

“Tunataka kufanya kazi yetu iwe nzuri hivyo, tukaamua kuja na mradi wa ujenzi wa jengo la kitega uchumi lenye urefu wa ghorofa nane. Sasa wakati tunaendelea na huu mpango tukakubaliana kuwa tuwe na jambo la hamasa ili tuhamasishe ujenzi, tulipozungumzia jambo la hamasa tukakubaliana kuwa tuandae mashindano ya Pikipiki nchi nzima, na mshindi wa kwanza atapata zawadi ya nyumba hii. Mshindi wa pili atazawadiwa bajaji, mshindi wa tatu atazawadiwa pikipiki na mshindi wanne hadi wa kumi watazawadiwa fedha kiasi cha shilingi laki tano” alisema Chimoti.

Shindano la Pikipiki la the Royal Tour ni shindano ambalo limeandaliwa na UMADIDO lenye lengo la kuhamasisha Maafisa Usafirishaji kwenye ujenzi wa jengo la kitega uchumi litakalo kuwa na urefu wa ghorofa nane na litajengwa katika Kata ya Iyumbu wilayani Dodoma.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad