HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, August 13, 2022

KINANA AFAFANUA KUHUSU RAIS SAMIA...WANAOSEMA NI RAIS WA KATIBA SIO WAKWELI, WASISIKILIZWE

 

Said Mwishehe-Michuzi TV- Zanzibar

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana amefafanua hatua kwa hatua namna ambavyo Rais Samia Suluhu Hassan amepatikana, huku akieleza kuwa wanaodai uwepo wake madarakani ni kutokana na Katiba tu, sio kweli.

Amesema Rais Samia amepita kwenye mchakato wote kwa mujibu wa Katiba na amepigiwa kura kama ilivyo kwa mgombea urais na kubwa zaidi Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilimpima kwa sifa zote ambazo anatakiwa kuwa nazo kiongozi wa nchi.

Kinana ametoa ufafanuzi huo leo Agosti 13,2022 alipokuwa akizungumza na wana CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja visiwani Zanzibar kwenye Kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na kutekeleza vema Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2020/2025.

“Nataka niseme na vizuri Watanzania wakajua tangu Rais Samia achukue uongozi wa taifa letu kuna kauli nimekuwa nikisikia kuwa Rais Samia ni Rais wa Katiba. Kauli hii ina ukweli lakini haina ukweli.

“Inaukweli kweli kwasababu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kila chama kitaweka mgombea na mgombea mwenza na Katiba inasema mgombea Mwenza na mgombea wanafasi moja ya kupiga kampeni ya chama chao na kila Chama kinatakiwa kuwa na Mgombea Mwenza,”ameeleza Kinana.

Aidha amesema CCM hakikumchagua Mgombea mwenza kwa kucheza bahati nasibu ya kutumbukiza halafu uangalie nani kapata nani kakosa bali wameweka sifa, kwa kuangalia uwezo, kukubalika , anafaa ,uwezo wa kufanya kampeni, anaweza kuleta kura nyingi.

Na mwisho wanajiuliza iwapo mgombea kwa sababu yoyote atakuwa hayupo au ameondoka madarakani je mgombea mwenza atamudu nafasi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vigezo vyote hivyo vilipimwa kwa Samia.

“Anaweza ndio , ana mudu, ndio, anajua kazi yake ndio, anaweza kufanya kampeni ndio, anaweza kumsaidia mgombea na kuleta kura ndio. Mwisho iwapo mgombea kwasababu yoyote ataondoka madarakani kwa njia za kidunia au zake Mwenyezi mungu anaweza kuchukua nafasi hiyo wana CCM tukajiridhisha ndio anaweza.

“Kwa hiyo kwa wale wanaosema huyu ni Rais wa Katiba si kweli , Rais Samia Suluhu Hassan alipimwa kabla ya kupewa hiyo nafasi, bahati nzuri mimi nilikuwa Katibu Mkuu wa Chama, nilishiriki vikao vya awali mwaka 2015 na wengine walikuwepo kwenye vikao, hayo maswali yote tulupojiuliza tukasema anaweza ,ana mudu hiyo kazi, anaongeza kura, ana uzoefu, anakifahamu Chama Cha Mapinduzi lakini kama anahitajika kuwa Rais anaweza.

“Sasa unaposema Rais Samia ni Rais wa Katiba hakuchaguliwa sio kweli lakini kubwa zaidi Rais anapopigiwa kura na mgombea mwenza anapigiwa kura na kabla haijafika muda wa kupiga kura iwapo mgombea mwenza Mwenyezi Mungu atamchukua uchaguzi utasimmamishwa.”

Ameongeza “Kwa nini usimamishwe? Kama kweli yeye ni Rais tu wa Katiba tuendeee kupiga kura mambo yaishe .Mwaka 2005 tulikuwa na Mgombea mwenza wa CHADEMA Jumbe Rajab Jumbe mwenyezi Mungu alimchukua , uchaguzi ulisimamishwa, kwanini ulismamishwa?

"Kwasababu na yeye ana nafasi muhimu hawezi Rais wa nchi akapigiwa kura au mgombea akapigiwa kura kama mgombea mwenza hayupo.Nataka nilifafanue hili hao wanaosema Rais Samia ni Rais wa Katiba hawasemi kweli.

"Rais Samia ni Rais aliyetokana na mchakato wa uchaguzi Mkuu , alipopigiwa kura Rais Magufuli na Samia alipigiwa kura hapo hapo kama Rais aliyemtangulia angekuwa ameondoka madarakani kwa kujiuzulu au kwasababu nyingine yoyote angekuwa Rais lakini kwasababu za Mwenyezi Mungu Rais Samia amechukua dhamana.

"Kwanini basi uchaguzi wa Chadema mwaka 2005 ulisimamishwa? Kwasababu wote wawili Mgombea Urais na Mgombea mwenza wanatokana na utaratibu wa Katiba uliowekwa kwa hiyo Rais Samia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wale wanaosema ni Rais wa Katiba wana ajenda yao, msiwasikilize."

Amesisitiza wanaosema Rais Samia ni wa Katiba hawasemi kweli huku akieleza kuhusi upande wa pili kweli ni Rais wa Katiba kwani Katiba inasema hivi kila Chama kitateua mgombea na mgombea mwenza.Rais au mgombea anatokana na matakwa ya Katiba ya Jamhurii ya Muungano wa Tanzania

"Mgombea mwenza ni matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano , kwa hiyo anateuliwa Samia kuwa mgombea mwenza ambaye baadae amekuwa Rais kutokana na matakwa ya Katiba kwa hiyo Rais Magufuli ni Rais wa Katiba.Mgombea unapendekezwa na Chama chako, uakwenda kwa wananchi lakini hupigiwi kura peke yako unapigiwa na mgombea mwenza."

Amefafanua zaidi wa hiyo wanaosema Rais Samia ni Rais wa Katiba hawasemi ukweli." Rais Samia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Nchi ya Marekani Rais wa sasa ni Rais wa 46 , katika marais 46 waliowahi kufariki kabla ya muda wao walikuwa marais nane baadae wakachukua wagombea wenza ambao wakawa marais.

"Hatujawahi kusikia wakiambiwa ni marais wa Katiba, lakini hapa Tanzania wanaotaka kukoroga mambo wanakwambia Rais Samia ni Rais wa Katiba,"amesema Kinana alipokuwa anatoa ufafanuzi kuhusu Rais Samia.



Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana akizungumza wakati wa kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan lililoandaliwa na CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, na kufanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B.


Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana, akipokea matembezi ya wana CCM ya kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, yaliyofanyika Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja. (Picha zote na Fahad Siraji wa CCM).


Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana, akiteta jambo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini, Iddi Ali Ame, wakati wa kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, lililoandaliwa na CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja na kufanyika Mahonda, Wilaya ya Kaskazini B, mkoani humo.


Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana, akisalimiana na viongozi mbalimbali wakati akiwasili Afisi Kuu ya CCM, Mkoa wa Kaskani Unguja kulipofanyika kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, Wilaya ya Kaskazini B, mkoani humo.



Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana, akiwa na viongozi wengine wa Chama wakifuatilia kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, lililoandaliwa na CCM katika Mkoa huo na kufanyika Mahonda, Wilaya ya Kaskazini B, mkoani humo.



Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, akizungumza wakati wa kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan lililoandaliwa na CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, na kufanyika Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja. Mgeni rasmi katika kongamano hilo alikuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana.

Vijana wakifuatilia kongamano la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, lililoandaliwa na CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja lililofanyika Mahonda, Wilaya ya Kaskazini B, mkoani humo. Katika kongamano hilo Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Kanali Mstaafu Abdulrahman Kinana, alikuwa mgeni rasmi.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad