HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, July 31, 2022

WIZARA YA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM, KWENDA NA VIPAUMBELE NANE, BAJETI YA 2022/23: WAZIRI DKT.GWAJIMA

 


Na MJJWM, DA ES SALAAM

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima, amesema katika Bajeti ya 2022/23, Wizara yake inatazamiwa kwenda na Vipaumbele 8 vitakavyotumia Jumla ya Bil. 43.3 iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Juni. 30. 2022 jijini Dodoma.

Dkt. Gwajima ametoa ufafanuzi huo Julai, 30, 2022 wakati akizungumza na Waandishi wa vyombo mbali mbali vya Habari.

Waziri Dkt. Gwajima amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na kuratibu afua za kukuza usawa wa kijinsia, uwezeshaji wanawake kiuchumi na kiuongozi na kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake, watoto na wazee. Kukuza ari ya jamii kushiriki katika kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo iliyoibuliwa ngazi ya jamii sambamba na kutambua na kuratibu makundi maalum wakiwemo wafanyabiashara ndogondogo (Machinga) ili kuboresha mazingira ya biashara zao.

Dkt. Gwajima amesema maeneo mengine ya vipaumbele ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika Taasisi ya Ustawi wa Jamii, Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru na Vyuo vya Maendeleo ya Jamii, halikadhalika kuratibu utoaji wa huduma za msingi kwa watu wenye mahitaji maalum, huduma za usuluhishi wa migogoro ya ndoa na familia na huduma ya msaada wa kisaikolojia kwa manusura wa majanga mbalimbali na makundi mengine yenye uhitaji katika jamii.

“Ndugu wanahabari mbali na maeneo hayo Serikali kupitia Wizara hii itaratibu na kuwezesha upatikanaji wa huduma za ustawi wa jamii kwa wazee, kuratibu na kusimamia afua za upatikanaji wa haki za mtoto, ulinzi na malezi chanya ya watoto sambamba na kuimarisha ushiriki na mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika maendeleo ya Taifa” alisisitiza Waziri Dkt. Gwajima.

Kuhusiana na fedha za Utekelezaji Waziri Dkt. Gwajima, amesema jumla shilingi za kitanzania zipatazo Bilioni 43.4 zimetengwa kwa ajili ya kuwezesha uendeshaji wa ofisi na utekelezaji wa miradi wa maendeleo.

Waziri Dkt. Gwajima amesema wizara itatumia kiasi cha Tsh 160,200,000/= kuhamasisha jamii katika kujenga moyo wa kujitolea, uzalendo na kushiriki katika shughuli za maendeleo huku kiasi cha fedha 107,100,000/ = ili kuandaa Mwongozo pamoja na kuwajengea uwezo viongozi wa Machinga kwa mwaka 2022/23.

Ameongeza kuwa Jumla ya shilingi Bilioni 45 zimetengwa kwa ajili ya kundi Machinga ili kuendeleza ujenzi wa miundombinu kwenye masoko na kuwawezesha kupata mitaji ya kuendeleza biashara zao, aidha maeneo mengine ya Vipaumbele aliyoyataja na fedha zitakazotumika ni pamoja na kiasi cha Shilingi 5,300,000,000/= kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia kwenye vyuo vilivyo chini ya Wizara.

“Shilingi 24,950,000 zimepangwa kutumika ili kukamilisha Mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia pamoja na Mkakati wake, Shilingi 15,940,000 zitatumika kusambaza Mwongozo wa Majukwaa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi” “Shilingi 81,200,000 imepangwa kutumika kutekeleza ahadi za nchi kuhusu Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa katika eneo la Haki za Kiuchumi kwa Wanawake amesema Dkt. Gwajima

“Kiasi cha Shilingi 600,000,000 zimetengwa, kwa ajili ya kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake wajasiriamali pamoja na mwanamke mjasiriamali mmoja mmoja, “Wizara imetenga kiasi cha Shilingi 168,980,000. kwa ajili ya kuratibu afua za kukuza usawa wa kijinsia na kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake” 23 “Shilingi 119,630,000 kwa ajili ya kampeni ya "Twende Pamoja, Ukatili Tanzania Sasa Basi" yenye lengo la kujenga uelewa kwa jamii kuhusu usawa wa kijinsia na kupinga ukatili, amezidi kufafanua Waziri Dkt. Gwajima

Katika hatua nyingine kwa mwaka huo huo wa fedha jumla ya shilingi za kitanzania 123,080,000 zimetengwa kwa ajili ya kuzindua madawati ya Jinsia kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu na Kati, ilihali Shilingi 94,510,000 zikiwa zimetengwa kuwezesha utoaji wa elimu ya malezi kwa njia ya kieletroniki yaani (Parenting Education Application)”

Dkt. Gwajima ameendelea kufafanua kwamba, kwa mwaka wa fedha 2022/23 Wizara kwa kushirikiana na wadau itaendesha Kampeni kubwa ya jamii ya kupinga na kutokomeza ukatili inayoenda kwa jina la Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii (SMAUJATA), ambapo takriban ni watu 8,000 wameshajiunga nchi nzima hadi kufikia Julai 29, 2022.

Awali akimkaribisha Waziri kuzungumza na waandishi wa habari, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Bw. Amon Mpanju, alisema jukumu kubwa la Wizara ni kwenda kuweka msukumo wa utekelezaji wa bajeti hiyo iliyopitishwa Juni, 30, 2022 na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad