HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, July 9, 2022

WAZIRI MULAMULA: WAFANYABIASHARA CHANGAMKIENI FURSA ZA MASOKO KATIKA JUMUIYA ZA KIKANDA

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akimkabidhi cheti mshiriki wa Maonesho ya Bukoba kutoka nchini Burundi kwa kufanya vuzuri katika maonesho hayoWAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula ametoa rai kwa Wafanyabiashara wa Tanzania kuchangamkia fursa za masoko zinazopatikana katika Jumuiya za Kikanda ambazo Tanzania ni mwanachama kama vile Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na fursa zitokanazao na Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA)

Waziri Mulamula ametoa rai hiyo wakati akizungumza na wafanyanyabisha kwenye maadhimisho ya kilele cha Maonesho ya Bukoba “Bukoba Expo" yaliyofanyika katika Viwanja ya CCM mjini Bukoba. Maonesho hayo yaliyobebwa na kauli mbiu isemayo “Biashara, viwanda na utalii ni fursa ya uwekezaji Mkoani Kagera”.

Akizungumza na wafanyabiashara wakati wa akifunga maonesho hayo Waziri Mulamula alieleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inayo dhamira ya dhati ya kukuza uchumi wa nchi kupitia biashara na uwekezaji kwa kudumisha ushirikiano na nchi jirani na kutafuta fursa za masoko kwa bidhaa zinazozalishwa nchini. Aliongeza kusema wakati Serikali inafanya hayo ni vyema sekta binafsi ikaunga mkono juhudi hizo za Serikali kwa kuchangamkia fursa za masoko zinazopatikana katika Jumuiya za Kikanda ili kujiongezea tija zaidi katika shughuli zao.

Mtakumbuka kuwa Tanzania pamoja na kuwa mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki pia ni mwanachama wa SADC na hivi karibuni tumeridhia mkataba wa Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (Africa Continental Free Trade Area-AfCFTA). Eneo Huru la Biashara la Afrika ni soko kubwa kuliko masoko yote yaliyoanzishwa ulimwenguni kwa kuwa na uwingi wa nchi wanachama zinazofikia 55. Soko hili linakadiriwa kuwa na idadi ya watu wapatao Bilioni 1.3 na Pato ghafi la Taifa (GDP) lenye jumla ya Dola za Marekani trilioni 3.4 na fursa za uchumi unaokua kwa kasi. Alieza Waziri Mulamula

Akizungumzia kuhusu maonesho hayo Waziri Mulamula ameleeza kuwa ubunifu wa waandaji umeakisi maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha Mkoa wa Kagera na wananchi wake wanapata maendeleo kwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchumi, biashara na uwekezaji kwa kutumia fursa zilizopo katika Mkoa huo na nafasi ya Kijiografia ya Mkoa kwa kupakana na nchi za Rwanda, Burundi na Uganda.

Kwa upande wake mratibu na mwandaaji wa Maonesho ya Bukoba Bw. William Rutta ameeleza kuwa maonesho hayo ambayo yamewavutia washiriki zaidi ya 350 wakiwemo wajasiliamari, wafanyabiashara, Taasisi za serikali na washiriki kutoka nchi za Burundi, Uganda, na Congo yametembelewa na wateja zaidi ya 10,000.

Aidha Bw. Rutta amebainisha malengo ya amonesho hayo kuwa ni pamoja na kuweka mwendelezo wa wiki ya uwekezaji ya Kagera ya mwaka 2019, kuunganisha wafanyabiashara na wananchi wote kushiriki katika shughuli za kuzalisha, mali, kuendeleza utalii na kubadilishana teknolojia ya uzalishaji na kuhamasisha utalii kwa kuandaa safari katika mbuga za wanyama asili za Burigi, Ibanda kyerwa, Runanyika Karagawe, Hifadhi ya Rubondo, Seregeti na vivutio vya asili kama fukwe za ziwa Victoria. Lengo lingine ni uboreshaji wa mazingira kwa kuhamasishwa upandaji miti aina ya palm tree katika mji wa Bukoba.

Waziri Mulamula kwenye maadhimisho ya kilele cha maonesho hayo pamoja na wajumbe wengine aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Meja Jenerali, Charles Mbuge, Mkuu wa Wilaya ya Bukoba Mhe. Moses Machali na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kagera Bi. Costansia Guhiye.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiwasili kwenye maadhimisho ya kilele cha Maonesho ya Bukoba “Bukoba Expo” yaliyofanyika katika viwanja vya CCM Bukoba mjini.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akiangalia bidhaa za mmoja wa washiriki wa maonesho ya Bukoba
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akizungumza na mmoja wa washiriki wa Maonesho ya (Bukoba hayupo pichani)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad