HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, June 9, 2022

BENKI YA MWALIMU KUKOPESHA WAFANYAKAZI VIFAA VYA UJENZI

Kaimu Mkurungezi Mkuu wa benki ya Mwalimu, Abdallah Kirungi (Kushoto) akiwa na Mkurungezi wa Kampuni ya Wasambazaji na wauzaji wa vifaa vya ujenzi ya Wahenga (JMF) Fatna Senzota katika hafla ya uzinduzi wa bidhaa mpya ya Jenga na Mwalimu
Kushoto ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Biashara na Masoko benki ya Mwalimu Sabina Mwakasungura, Kaimu Mkurungezi mkuu wa benki  hiyo,  Abdallah Kirungi, Mkurungezi wa Kampuni ya Wasambazaji na wauzaji wakubwa wa vifaa vya ujenzi (FMJ), Fatna Senzota pamoja na Mshauri wa Kampuni ya (FMJ ) Wema Muhama katika hafla ya uzinduzi wa bidhaa mpya ya Jenga na Mwalimu
Mkurungezi wa Kampuni ya Wasambazaji na wauzaji vifaa vya ujenzi ya Wahenga(JMF) Fatna Senzota akizungumza na waandishi wa habari katika hafla ya uzinduzi wa bidhaa mpya ya jenga na mwalimu benki.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Biashara na Masoko benki ya Mwalimu, Sabina Mwakasungura akizungumza wakati wa hafla ya Uzinduzi wa bidhaa mpya ya Jenga na Mwalimu Benki.

Na Mwandishi wetu
BENKI ya Mwalimu Commercial PLC, imesema imejipaga kuwakopesha wafanyakazi vifaa vya ujenzi ili waweze kufikia malengo ya kumiliki nyumba na kuboresha makazi yao.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa bidhaa yao mpya ya Jenga na Mwalimu Benki kwa kushirikiana na kampuni ya Wasambazaji na Wauzaji wa Vifaa vya ujenzi ya Wahenga (FMJ),Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Biashara na Masoko wa Benki hiyo, Sabina Mwakasungura amesema, Katika kuendana na kasi ya serikali ya awamu ya sita ya Rais Samia Suluhu Hassan Katika kuboresha maisha ya watumishi imeona kuna umuhimu kuunga juhudi kwa kutoa mikopo ya vifaa vya ujenzi.

Amesema mkakati huo utasaidia watumishi wa umma na binafsi kunufaika kwakuwa huduma hizo zitatolewa kwa bei nafuu na zenye tija.

Amesema Benki hiyo katika kuendana na mpango mkakati wa miaka mitano imelenga kuboresha huduma zenye ubunifu na ufanisi katika kuwafikia wateja huku moja ya maeneo yaliyopewa kipaumbele ni kuwa na bidhaa zinazolenga moja kwa moja watumishi wa kada zote ili wajiinue kiuchumi na kuleta tija ndani ya jamii.

"Benki yetu imelenga katika utoaji wa huduma za kibenki ambazo ni nafuu salama na zinazopatikana popote na wakati wowote kwa njia ya kidigitali pamoja na Mwalimu Mobile, Mwalimu wakala na Mwalimu Card Visa," amesema Sabina.

Ameongeza kuwa huduma hizo zinawezesha wateja waliosambaa mikoa yote kufanya miamala kwa urahisi bila usumbufu.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo, Abdallah Kirungi amesema, hadi sasa Benki hiyo ina matawi mawili Dar es Salaam na mengine tisa Katika mikoa ya Morogoro, Mbeya, Mwanza, Dodoma, Arusha, Rukwa, Kigoma, Mtwara na Arusha.

Amesema matarajio ya benki hiyo ni kuwa na vituo katika mikoa yote ifikapo mwaka 2025.

Amesema kama Benki wametoa fursa hiyo kwa wakopaji kukopa kiasi chochote ili mradi mteja awe na uwezo wa kulipa mkopo huo.

Naye, Mkurugenzi wa Kampuni ya Wasambazaji na wauzaji wa vifaa vya Ujenzi ya Wahenga ( JMF), Fatna Senzota ameipongeza Benki hiyo kwa wazo hilo na kuwashauri kuangalia kwa upana zaidi kutoa fursa hizo kwa sekta nyingine.

Amesema zipo shule binafsi na sekta nyinginezo ambazo watumishi wake wanahitaji mikopo ya bei nafuu ili waweze kuboresha maisha hivyo kufanya hivyo kutasaidia kuinua uchumi wa nchi na maisha ya jamii kwa ujumla.

" Ni wakati sasa kwa watumishi kutumia fursa hii ya hitaji lao kubwa la ujenzi kwa njia ya mkopo ambapo masharti yake ni nafuu na vifaa vyake ni bora," amesema Sabina.


Amesema kampuni hiyo imekuwa ikitoa huduma hiyo ndani na nje ya nchi kwa muda mrefu sasa na wana matumaini mkakati huu mpya utawafikia wengi na utasaidia wengi kuondokana na changamoto ya ukosefu wa makazi.

Pia, Mshauri wa Kampuni hiyo, Wema Muhama amesema, ni wakati sasa kwa watumishi kunufaika na bidhaa hizo ambazo tayari zipo sokoni na zinapatikana kwa bei nafuu.

Amesema tamaa yao kubwa ni kuona maisha ya watumishi na watanzania kwa ujumla yanabadilika kupitia mpango huo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad