HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, May 26, 2022

WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI YAOKOA BILIONI 9 KUPITIA WAFUNGWA WALIOTUMIKIA ADHABU ZAO NJE YA MAGEREZA, YAJIPANGA KUDHIBITI WANAORUDIA MAKOSA BAADA YA MSAMAHA WA RAIS

 


Na Mwandishi Wetu, MOHA, Morogoro.
ZAIDI ya shilingi Bilioni Tisa (9) zimeokolewa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya Huduma za Uangalizi kwa kuwasimamia wafungwa 5,000 nje ya magereza ambapo wangetumia zaidi ya shilingi bilioni nne kwa chakula kama wangebaki magerezani na kupitia shughuli mbalimbali zinazofanywa bila malipo wanapotumikia kifungo cha nje katika taasisi za umma nchini.

Akizungumza katika Mkutano wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi wa Mikoa wa Idara hiyo ya Huduma za Uangalizi, Mjini Morogoro, leo, Mkurugenzi wa Idara hiyo, Aloyce Musika alisema idara hiyo imefanikiwa kuokoa fedha hizo kupitia kazi mbalimbali zinazofanywa na wafungwa wa nje pindi wanapotumikia vifungo vyao.

Alifafanua kuwa kwa mwaka wafungwa 5,000 wanaotumikia vifungo vyao vya nje wanatumia zaidi ya shilingi bilioni nne kwaajili ya chakula kwa kima cha chini, kupitia kazi wanazo zifanya za usafi na mambo mengine Serikali ingeweza kuwalipa wafanyakazi zaidi ya shilingi bilioni tano kama wangelipwa kima cha shilingi elfu nne kwa mwaka.

Mkurugenzi Musika aliongeza kuwa, viongozi hao wa mkoa wana jukumu la kuimarisha ulinzi na usalama katika jamii kwa kuwasimamia wafungwa hao nje ya magereza, hivyo jukumu lao ni kuhakikisha Wafungwa hao wanapo tumikia vifungo vyao wanatakiwa kusimamiwa ipasavyo iliwasiweze kutumiwa kwa kurudia makosa mengine.

“Niwaombe viongozi waangalizi wa mikoa muwasimamie wafungwa hawa ipasavyo ilituweze kufanikisha adhima ya Serikali kwa kuaminisha kuwa watu wanaweza kutumikia vifungo vyao vya nje wakaweza kufanya shughuli kwaajili ya kuhudumia familia zao na kutumikia adhabu zao na kuiongezea Serikali fedha”, alisema Musika.

Pia Mkurugenzi Musika alisema kupitia idara yake wanajipanga kudhibiti wafungwa wanaorudia makosa baada ya msamaha wa Rais ambao anautoa mujibu wa sheria.

Aidha, Afisa Huduma za Uangalizi Mkoa wa Pwani, Subira Majengo alisema wafungwa wengi wa kifungo cha nje wanatumikia kifungo hicho kikamilifu na wengi wakimaliza vifungo vyao wanarudi katika jamii wakiwa wamebadilika na wanaendelea na maisha yao kama kawaida.

Hata hivyo, aliwaomba wafungwa wanaotikia vifungo vyao nje kuhakikisha wanakuwa funzo na mfano kwa jamii kuelezea kifungo cha nje kilivyo na kuhakikisha hawarudii makosa na wanafanya mambo yanayopendeza katika jamii.

Kwa upande wake mmoja wa wafungwa wanaotumikia kifungo cha nje, Katika Halmashauri ya Morogoro, Frolensia Makwaya alisema kifungo hicho kimemsaidia sana, kwa kuwa ameweza kuendelea na majukumu yake kwa kuwa anatumikia kifungo chake kuanzia saa kumi na mbili asubuhi na saa nne asubuhi anaendelea na kazi zake za kawaida.

Alisema kifungo hicho kimemfanya afanye kazi kwa uchungu ilikuweza kulea mtoto wake, ameiomba Serikali kuwasaidia na wafungwa wengine kuweza kupata nafasi ya kuhudumia familia zao kwa kuwa familia nyingi zinateseka.
Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Uangalizi, Aloyce Musika akizungumza katika Mkutano wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi wa Mikoa wa Idara hiyo, uliofanyika katika Hoteli ya Flomi, mjini Morogoro, leo. Amesema zaidi ya shilingi Bilioni Tisa (9) zimeokolewa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara hiyo kwa kuwasimamia wafungwa 5,000 nje ya magereza ambapo wangetumia zaidi ya shilingi bilioni nne kwa chakula kama wangebaki magerezani na kupitia shughuli mbalimbali zinazofanywa bila malipo wanapotumikia kifungo cha nje katika taasisi za umma nchini.
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Huduma za Uangalizi (Probesheni), Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Nsanze, akiwasilisha mada kuhusu taarifa ya utekelezaji wa idara hiyo katika Mkutano wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi wa Mikoa wa Idara hiyo, uliofanyika katika Hoteli ya Flomi, mjini Morogoro
Baadhi ya Viongozi wa Mikoa wa Idara ya Huduma za Uangalizi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, wakimsikiliza Mkurugenzi wa Idara hiyo (hayupo pichani) wakati alipokuwa anazungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi hao, unaofanyika katika Hoteli ya Flomi, mjini Morogoro
Afisa Huduma za Uangalizi, Mkoa wa Pwani, Subira Majengo akizungumza katika Mkutano wao wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi wa Mikoa wa Idara hiyo, uliofanyika katika Hoteli ya Flomi, mjini Morogoro.
Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Uangalizi, Aloyce Musika (katikati waliokaa), akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wakuu wa Idara wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, pamoja na Viongozi wa Mikoa wa Idara hiyo, baada ya kufunguliwa kwa mkutano wa Mwaka wa Utendaji wa Viongozi hao, unaofanyika katika Hoteli ya Flomi, mjini Morogoro, leo. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad