HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, March 10, 2022

WCF: TUNA WAJIBU WA KUHAKIKISHA TUNALINDA NGUVU KAZI YA TANZANIA

 Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umewahimiza waajiri kuchangamkia fursa ya punguzo la michango lililotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita kuanzia Julai Mosi 2021 ili kulinda nguvu kazi na kuongeza ari ya wafanyakazi wao.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi Dkt. John Mduma wakati akizungumza na wahariri baada ya Ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), 2022 uliofanyika Unguja, Zanzibar.

Dkt. Mduma amesema katika mafanikio ya siku 365 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, WCF inajivunia kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini kwa kukubaliwa kutoa punguzo la uchangiaji kutoka 1% kwa waajiri wa sekta binafsi hadi kufikia asilimia 0.6% na punguzo la riba (interest) la madeni ya nyuma ya michango kwa sekta zote kutoka asilimia 10% mpaka asilimia 2%.

Dkt. John Mduma amefafanua kuwa, moja ya wajibu wa WCF ni kulinda nguvu kazi ya wafanyakazi kuanzia matibabu ya Mfanyakazi aliyepata ajali au ugonjwa kutokana na kazi ili kuwawezesha Waajiri kuendelea kusimamia uzalishaji wakati wafanyakazi wao wakiendelea kuhudumiwa na WCF.

“Nakushukuru sana Mwenyekiti wa TEF kwa kutupa nafasi hii ya kuweza kushiriki kwenye hadhira hii ambayo kimsingi inatuwezesha kuufahamisha Umma kuhusu WCF inavyowajibika katika kulinda nguvu kazi ya Tanzania. Tunapenda kuwahimiza Waajiri wa Sekta Binafsi kuchangamkia fursa hizi za uboreshaji ikiwemo punguzo la uchangiaji na tozo ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima kati yao na wafanyakazi” Alisema Dkt. Mduma.

Dkt. Mduma pia alibainisha kuwa WCF inashirikiana kwa karibu na Taasisi ya Hifadhi ya Jamii Zanzibar, ZSSF ikiwemo kubadilishana mawazo na kupeana uzoefu juu ya masuala ya Fidia kwa Wafanyakazi.

“Sisi kama wabobezi karibu miaka saba sasa ya utekelezaji wa Sheria ya Malipo ya Fidia kwa Wafanyakazi, tumekuwa tukipeana uzoefu na kujadiliana nao ili nao waweze kuelekea kwenye upande huo.” 

Naye Mtaalamu wa Takwimu kutoka WCF, Bw. James Tenga aliwajulisha wahariri kuhusu masuala mbalimbali ya utekelezaji wa majukumu ya Mfuko huo ikiwa ni pamoja na taratibu za madai ya fidia kwa Mfanyakazi anapoumia, kuugua au kufariki kutokana na kazi ili aweze kulipwa fidia.

Amesisitiza pia umuhimu wa Mwajiri kujisajili katika Mfuko na kuwasilisha michango ya kila mwezi ambapo kwa sasa huduma zote za Mfuko huo hutolewa kwa njia ya mtandao ikiwemo uwasilishaji wa madai. 

Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), 2022 umefunguliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi Unguja, Zanzibar na unaongozwa na kauli mbiu isemayo “Uchumi wa Buluu na Mawasiliano ya Umma”.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, cheti cha shukrani kutokana na Mfuko huo kuwa miongoni mwa Taasisi zilizodhamini Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) unaofanyika mjini Unguja, Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akihutubia wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kwenye ukumbi wa Idrisa Abdulwakil, kisiwani Unguja, Zanzibar Machi 9, 2022.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akihutubia wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kwenye ukumbi wa Idrisa Abdulwakil, kisiwani Unguja, Zanzibar Machi 9, 2022
Waziri wa Habari na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Mhe. Nape Nnauye, akizungumza kwenye mkutano huo.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Tabia Maulid Mwita, akizungumza kwenye mkutano huo.Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, akisalimiana na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu ya Zanzibar, Bw. Charles Hillary.
Dkt. Mduma akizungumza na wajumbe wa TEF.
Mtaalamu wa Takwimu WCF, Bw. James Tenga, akiwasilisha mada kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Mfuko.
Mtaalamu wa Takwimu WCF, Bw. James Tenga, akiwasilisha mada kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Mfuko.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Bw. Deodatus Balile, akizungumza kwenye mkutano huo.
Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma (kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba wakibadilishana mawazo.
Baadhi ya wajumbe na wageni waalikwa wakifuatilia mkutano.

Baadhi ya wajumbe wa TEF wakibadilishana mawazo.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Elimu kwa Umma, WCF, Bi. Laura Kunenge (kulia) akimsikiliza Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Mfuko huo, Bi. Sarah Reuben.
Baadhi ya wajumbe wa mkutano wakifuatlia kwa makini
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (katikati) na viongozi waliokuwa meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wadhamini wa Mkutano huo.

 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad