HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, February 7, 2022

TaSUBa yatakiwa kwenda Kimataifa

 


Naibu Katibu Mkuu wa Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu ameitaka Taasisi ya Sanaa Utamduni na Bagamoyo (TaSUBa) kuweka malengo ya kwenda mbali zaidi na kua kituo cha mafunzo bora kilichotukuka duniani tofauti na ilivyo sasa ambapo TaSUBa inasemwa kuwa kituo cha mafunzo bora kilichotukuka Afrika Mashariki.

Ameyasema hayo leo tarehe 07, Februari 2022 alipotembelea Taasisi hiyo na kuzungumza na uongozi na watumishi na baadae kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo.

Amesema hakuna jambo lolote linaloshindikana ili Taasisi hiyo ishindwe kutambulika kimataifa kwa sababu mafunzo yanayotolewa na Taasisi hiyo ni ya kipekee sana.

”Mimi sioni kama kuna kitu kinachotushinda au kutukwanza tusiwe na viwango vya kimataifa katika mafunzo tunayotoa hapa kuhusu sanaa na utamaduni,” alisema Mhe. Yakubu.

Aidha Mhe.  Naibu Katibu Mkuu amesema angependa TaSUBa iongeze udahili wa wanafunzi kwa kuwa idadi iliyopo sasa ya wastani wa wanafunzi mia sita ni ndogo ikilinganishwa na uhitaji uliopo katika Jamii na upekee wa mafunzo yanayotolewa na Taasisi hio sambamba na ongezeko la kozi mbalimbali. Ameitaka TaSUBa kuongeza pia udahili wa wanafunzi kutoka nje ya nchi ili waweze kuwa mabalozi wazuri wa utamaduni na sanaa za kitanzania. 

“Katika kuongeza idadi ya wanafunzi, tuboreshe mazingira pia na miundombinu ili tuweze kudahili wanafunzi kutoka nje ya nchi na kama tuko peke yetu Afrika Mashariki ina maana hata kujitangaza kwetu kungefanyika kwa mapana zaidi,” alisema Mhe. Yakubu.

Ameitaka TaSUBa kwenda mbali zaidi kwa kutanua wigo wa mafunzo kwa kufungua kampasi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

“Ni wakati mwafaka sasa TaSUBa mkafikiria kuongeza wigo wa kutoa mafunzo haya kwa kuanzisha kampasi maeneo mbalimbali ya nchi kama Mwanza, Mtwara, Mbeya, Dodoma na maeneo mengine,” alisema Mhe. Yakubu.

Kwa upande wa kufanya tafiti na ushauri katika mambo yanayohusu sanaa na utamaduni ambayo pia ni kazi mojawapo ya chuo hicho cha sanaa Mhe. Yakubu ameitaka TaSUBa isibaki kufanya kazi zake Bagamoyo tu bali ijitanue na kufika katika maeneo yote ya nchi ili kubeba sura ya Tanzania. Alisisitiza kuwa sanaa na utamaduni ndio urithi wetu hivyo ni lazima tuwekeze sana katika utafiti ili tuweze kuitunza kwa vizazi vyetu na vizazi vijavyo. 

”TaSUBa ina monopoly katika eneo hili la sanaa na utamaduni kama ilivyo TANESCO na umeme wao, hivyo tulifanyie kazi eneo hili,” alisisitiza Mhe. Naibu Katibu Mkuu.

Naye Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo Dkt. Herbert Makoye ameishukuru Serikali kwa jitihada mbalimbali inazozifanya ili kuiboresha TaSUBa kwa upande wa miundombinu na vifaa vya kufundishia.

Naibu Katibu Mkuu Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu alipata wasaa wa kukagua na kuona madarasa ya uzalishaji wa muziki na upigaji vyombo na ala mbalimbali za muziki.

Naibu Katibu Mkuu Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu alipata fursa ya kukagua shughuli mbalimbali za uboreshaji miundombinu ya Taasisi (TaSUBa)

 

Viongozi na watumishi wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu alipokutana nao wakati wa ziara yake chuoni hapo.

Naibu Katibu Mkuu Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu akiongea na uongozi pamoja na watumishi wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) na kupokea changamoto zao mbalimbali na kuahidi kuzifanyia kazi.

Naibu Katibu Mkuu Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Said Yakubu akisaini kitabu cha wageni alipowasili katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) kwa ziara fupi tarehe 07 Februari, 2022.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad